Na John Gagarini, Kibaha
WAKAZI wa Mitaa ya Vikawe, Vikawe Shuleni, Vikawe Bondeni na Vikawe
wilayani Kibaha mkoani Pwani wamepatiwa ofa ya kutumia maji bure kwa
miezi mitatu baada ya huduma hiyo kuanza kupatikana ambapo mitaa hiyo
haikuwa na maji ya bomba tangu kuanzishwa kwake.
Maji hayo tayari yameshaanza kutoka yanatokana na chanzo cha maji cha
Ruvu Juu baada ya mitaa hiyo kutokuwa na maji kabisa ambapo awali
walikuwa wakitumia maji ya visima na mto .
Akizungumza na mabalozi, makatibu na viongozi wa Jumuiya za Chama Cha
Mapinduzi (CCM) kata ya Mkuza wilayani Kibaha wakati wa semina ya
viongozi hao iliyofanyika jana mjini Kibaha, Mbunge wa Jimbo la Kibaha
Silvestry Koka alisema kuwa maji yameanza kutoka kwenye mitaa hiyo
hivi karibuni.
“Wananchi hao wamepata ofa hiyo ya kutumia maji bure lakini baada ya
miezi mitatu wataanza kuyalipia maji hayo baada ya kukosa maji ya
bomba kwani kulikuwa hakuna maji kabisa na walikuwa wakichota maji
kwenye visima na mto ambapo baadhi walipoteza maisha kwa kukamatwa na
mamba walipokuwa wakichota maji mtoni,” alisema Koka.
Katika hatua nyingine Koka alisema kuwa mji wa Kibaha utaondokana na
tatizo kubwa la ukosefu wa maji baada ya mradi wa bomba kubwa kutoka
chanzo cha mto Ruvu kuanza.
Koka alisema kuwa kwa muda mrefu wa mji huo umekuwa ukikabiliwa na
changamoto kubwa ya ukosefu wa maji huku wakati mwingine maji yakiwa
yanatoka kwa mgao kutokana na chanzo kilichopo kutokuwa na uwezo wa
kutoa maji ya kutosha.
“Mradi huu kwa sasa uko kwenye hatua nzuri ambapo uchimbaji wa mtaro
utaanza muda wowote kuanzia sasa kwani taratibu zingine zimekamilika
na bomba litakalopitishwa litakuwa ni kubwa ambalo litapitisha maji
mengi,” alisema Koka.
Kwa upande wake katibu wa (CCM) Kibaha Mjini Abdala Mdimu alisema kuwa
utekelezaji wa miradi hiyo ni utekelezaji wa ilani ya chama ambayo ni
ahadi kwa wananchi ili kuboresha utoaji huduma.
Mdimu alisema kuwa chama kupitia kwa viongozi wake kitahakikisha ahadi
zote zinatekelezwa kwa wakati uliopangwa ili wananchi waondokane na
kero za huduma muhimu.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...