Na Mohamed Saif

Imeelezwa kwamba huduma ya leseni za madini kwa njia ya mtandao itampunguzia gharama na adha za usafiri mmiliki wa leseni za madini kwa kumuwezesha kulipia ada za leseni yake pale alipo.

Hayo yameelezwa hivi karibuni na Afisa Madini Mkazi-Njombe, Samwel Ayubu alipokuwa akifungua mafunzo ya matumizi kuhusu huduma za leseni kwa njia ya mtandao yaani Online Mining Cadastre Portal (OMCTP) kwa wachimbaji wa madini mkoani Njombe.

Ayubu alisema kupitia mfumo wa zamani, wakati mwingine mmiliki wa leseni analazimika kusafiri umbali mrefu na kutumia ghrama kubwa na vilevile kupata usumbufu usio wa lazima pindi anapohitaji kuhuisha leseni yake ama pale anapokuwa na maombi ya leseni.

“Kwa kupitia huduma hii ya kielektroniki, mmiliki wa leseni ataweza kuepuka changamoto mbalimbali alizokuwa akikutana nazo wakati wa mfumo wa zamani wa uombaji leseni,” alisema Ayubu.

Alitaja manufaa mengine ambayo yanatokana na huduma hiyo kuwa ni kuongeza uwazi na kasi ya utoaji wa leseni za madini kwakuwa waombaji wa leseni wataingiza maombi ya leseni wao wenyewe na hivyo kupunguza tatizo la mlundikano wa maombi kwenye ofisi za madini.

Aidha, Afisa Madini Mkazi huyo aliwataka wachimbaji waliohudhuria mafunzo hayo kuwa mabalozi kwa wale ambao hawakupata fursa ya kuhudhuria mafunzo hayo.

“Kwa mafunzo mtakayoyapata hapa, nawaomba mkawe walimu kwa wenzenu ambao hawakufanikiwa kuhudhuria semina hii,” alisema. Alimalizia kwa kuwaasa wachimbaji hao kuhakikisha wanatembelea Ofisi ya Madini-Njombe kwa lengo la kupatiwa elimu zaidi kuhusu mfumo huo na vilevile kufika hapo kwa ajili ya kusajiliwa kwenye huduma hiyo.
Afisa Madini Mkazi- Njombe, Samwel Ayubu (kulia) akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mafunzo kwa wachimbaji Madini wa Mkoani Njombe kuhusu Huduma za Leseni kwa njia ya Mtandao (OMCTP) mjini Njombe. Wengine ni Maafisa kutoka Kitengo cha Leseni Mjiolojia Mwandamizi, Idd Mganga (kushoto) na Mhandisi Edward Mumba (katikati).
Watumishi wa Wizara ya Nishati wakiwa katika picha ya pamoja kwenye Ofisi za Madini-Njombe baada ya Mafunzo kwa wachimbaji madini mkoani humo. Watatu kutoka kushoto ni Afisa Madini Mkazi-Njombe, Samwel Ayubu kushoto kwake ni Idd Mganga na kulia kwake ni Mhandisi Edward Mumba.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...