Kaimu Mkuu wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), Profesa Mohamed Janabi katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) akizungumza na waandishi wa habari leo baada ya taasisi hiyo kufanikiwa kuwafanyia upasuaji watoto 37.
Waandishi wa vyombo mbalimbali vya habari nchini wakimsikiliza Profesa Mohamed Janabi leo katika hospitali hiyo.
HOSPITALI ya Taifa Muhimbili (MNH) kupitia Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (Jakaya Kikwete Cardiac Institute (JKC) imefanikiwa kuokoa zaidi ya Shilingi mIlioni 800 baada ya kuwafanyia upasuaji wa moyo watoto 37 wenye matatizo ya moyo .
Operesheni hiyo imefanyika kuanzia Oktoba 10 hadi 19 mwaka huu kwa kushirikisha timu ya wataalam 18 kutoka nchini Italy na Marekani pamoja na madaktari bingwa wa magonjwa ya moyo kutoka taasisi hiyo.
Kaimu Mkuu wa taasisi hiyo Profesa Mohamed Janabi amewaeleza waandishi wa habari leo jijini Dar es salaam kwamba endapo wagonjwa hao wangetibiwa nje, kila mmoja yangegharimu kati ya Dola za Kimarekai 10,000 hadi 15,000, gharama ambazo Watanzania wengi hawawezi kuzimudu.
Kwa mujibu wa Profesa Janabi, changamoto inayowakabili ni upatikanaji wa damu na upungufu wa watalaam.
Alifafanua kwamba hivi sasa kuna orodha ya watu 500 ambao wanasubiri kufanyiwa upasuaji wa moyo, na kwamba desemba mwaka huu, wanatarajia kupokea wagonjwa wenye matatizo ya moyo kutoka nchini Zambia.
Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha Moyo cha Watoto, Dk. Edwin Shiran amesema watoto 17 wamefanyiwa upasuaji wa kufungua kifua na wengine 20 wamewekewa kifaa maalum kwa ajili ya kuziba matundu na kuzibua mishipa ambayo imezibana na kwamba kati ya hao watoto wawili wametokea Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).
Tangu Januari mwaka huu tayari wamekwishafanyiwa upasuaji wa moyo watoto 122 na watu wazima 132 .
Hongera Muhimbili kwa kuweza kuboresha huduma na kufikia hatua hii kubwa ya maendeleo, jambo la kupunguza safari za nje za matibabu ya wagonjwa wa moyo hasa watoto na kuweza kuokoa pesa zote hizi ni jambo la kujivunia. Madaktari wetu endeleza kazi nzuri ya kuimarisha matibabu ya wagonjwa hapa nchini.
ReplyDelete