Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki amemuagiza Kaimu Meneja Mkuu, Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO), Maselle Shilagi kuhakikisha anawapa chanjo Ng’ombe wote katika Ranchi 14 za Taifa ili kuwakinga na ugonjwa wa homa ya mapafu ulioanza kuathiri baadhi ya Ng’ombe katika Ranchi ya Kongwa.

Ndaki alitoa agizo hilo Disemba 11, 2020 alipofanya ziara ya kushtukiza katika Ranchi ya Kongwa iliyopo Mkoani Dodoma baada ya kupata taarifa ya mlipuko wa ugonjwa wa homa ya mapafu katika Ranchi hiyo.

Alisema kwasababu ugonjwa huo umekuja kwa ghafla hakuna haja ya kusubiri jitihada za haraka zichukuliwe kuudhibiti mapema kabla haujasambaa katika maeneo mengine na kusababisha madhara makubwa zaidi.

“Kwa kuwa tayari tuna dozi 9500 za chanjo ambazo zimefika hapa, namuagiza Kaimu Mkurugenzi ahakikishe anaanza kuwapatia chanjo ng’ombe hawa kuanzia leo na kufika kesho saa saba mchana nipate taarifa ya maendeleo ya uchanjaji kwa sababu ni jambo la dharura hivyo hatuwezi kusubiri sana, ili kama kuna mabadiliko mengine tuweze kuona ni hatua gani zinachukuliwa,” alisema Ndaki

Aliongeza kwa kusema kuwa hali ya ng’ombe katika ranchi hiyo bado ni nzuri na wakianza kupewa chanjo leo ugonjwa huo utadhibitiwa huku akiwataka kuendelea kuchukua tahadhari ikiwemo kuchanja ng’ombe wote waliopo katika Ranchi nyingine ili ugonjwa usiathiri afya za mifugo.

“Nafahamu kuwa katika hizi Ranchi pia wapo ng’ombe wa wafugaji binafsi, natoa maelekezo kuwa ng’ombe hao pia wapatiwe chanjo pamoja na ng’ombe wa maeneo ya jirani kwa sababu tukichanja ng’ombe wa kwetu tukaacha hao wengine tutakuwa hatujatibu tatizo,” alisisitiza Ndaki

Aidha, Ndaki alitumia fursa hiyo kuwaondoa hofu wafugaji wote waliopo katika maeneo ya Kongwa na sehemu nyingine kuwa wasiwe na wasiwasi kwa sababu serikali imeshaleta chanjo na zoezi la uchanjaji litaanza mara moja kudhibiti ugonjwa huo.

Kwa upande wake, Daktari wa Mifugo, Ranchi ya NARCO Kongwa, Dkt. Nickson Mbise alisema toka ugonjwa huo ulipoanza kuathiri Wanyama mpaka sasa wameshakufa ng’ombe watano (5) kati ya ng’ombe 9200 waliopo katika ranchi hiyo huku akisema chanzo kikubwa cha vifo hivyo ni homa ya mapafu.

 “Dalili za mwanzo tulizoziona ni ng’ombe kupumua kwa shida na wakati mwingine ng’ombe anakimbia hovyo kama ana kichaa, na tatizo lilivyoanza tulipata vifo vya ghafla vya ng’ombe wawili katika mazizi tofauti, tulipowachunguza tuligundua mapafu yao yalikuwa yameharibika hivyo tukagundua kuwa ni ugonjwa wa mapafu,” alisema Dkt. Mbise

Aliongeza kuwa ugonjwa huo umekuwa ukisumbua sana katika eneo hilo ndio maana huwa wanachanja mifugo mara mbili kwa mwaka, kila baada ya miezi sita lakini kwa wakati huu ugonjwa umelipuka ghafla hivyo wameshaagiza chanjo kutoka Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania kwa ajili ya kukabiliana na tatizo hilo.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel alisema kuwa atayasimamia maagizo yote aliyoyatoa Waziri na kuhakikisha yanatekelezwa kama alivyoagiza huku akisema kuwa kufuatia maagizo hayo wameshaleta katika Ranchi hiyo dozi za chanjo 9500 kwa ajili ya kuchanja ng’ombe hao.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki (wa kwanza kushoto) akisalimiana na baadhi wa Wafanyakazi wa Ranchi ya Kongwa muda mfupi baada ya kufika katika Rachi hiyo kukagua hali ya mifugo kufuatia mlipuko wa ugonjwa wa Homa ya Mapafu iliyowapata baadhi ya ng'ombe katika Ranchi hiyo Iliyopo jijini Dodoma Disemba 11, 2020. Wa pili kushoto ni Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel.
Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki (Wa kwanza kushoto) akiongea na baadhi ya Wafanyakazi wa Ranchi ya Kongwa alipofanya ziara ya kukagua hali ya mifugo kufuatia mlipuko wa Homa ya mapafu iliyowapata baadhi ya ng'ombe katika Ranchi hiyo iliyopo jijini Dodoma Disemba 11, 2020. Katikati ni Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel.
Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki (kulia) akimsikiliza Daktari wa Mifugo wa Ranchi ya Kongwa, Dkt. Nickson Mbise (kushoto) alipofanya ziara ya kukagua hali ya mifugo kufuatia mlipuko wa homa ya mapafu iliyowapata baadhi ya ng'ombe katika Ranchi hiyo iliyopo jijini Dodoma Disemba 11, 2020. Katikati ni Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel.

 Daktari wa Mifugo wa Ranchi ya Kongwa, Dkt. Nickson Mbise (katikati) akitoa maelezo kwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki (kushoto) kuhusu hali ya ng'ombe  baada ya mlipuko wa homa ya mapafu ulioikumba Ranchi hiyo iliyopo jijini Dodoma Disemba 11, 2020. Kulia ni Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...