Na Muhidin Amri,Mbinga

ZAIDI ya wakulima 4000 kutoka vijiji mbalimbali katika Halmashauri ya Mbinga mkoani Ruvuma, wamepatiwa msaada wa mbegu bora za mahindi zitakazowasaidia kuongeza uzalishaji na kukuza  vipato vyao.

Akizungumza wakati wa zoezi la ugawaji wa mbegu hizo Kaimu Afisa kilimo wa Halmashauri Deodatus Kisima alisema, mchakato wa mpango huo umetokana na maombi ya uhitaji  wa mbegu kutoka serikali kuu kupitia  serikali ya mkoa ambapo awali walikubaliwa kupata tani 4.

Kwa mujibu wa Kisima,kutokana na mahitaji makubwa ya wakulima  katika Halmashauri hiyo Serikali ikaona ni vyema kuwaongezea  hadi kufikia  tani 8,hata hivyo katika hatua ya mwisho ya Utekelezaji wa mpango huo Halmashauri ilifanikiwa kupata  tani 11 ambazo ni sawa na kilo 11,000 za mbegu ya  mahindi zenye thamani ya shilingi milioni 77.

Kisima alisema, katika mpango huo kila mkulima atapata kilo 2 hadi 4 ya  mbegu  aina ya ni DK 90-89 ambazo zinafaa kwa mazingira ya ukuaji wa zao  ma mahindi katika Halmashauri hiyo.

Alisema,uteuzi wa wakulima ulifanywa na maafisa watendaji wa maeneo yaliyolengwa kupata mbegu kwa ajili ya kilimo cha mahindi ambapo maeneo yaliyolengwa na kupatiwa mbegu hizi ni vijiji vya kata ya AmaniMakolo,Mkako,Namswea,Muungano,Matiri,Muhongozi,Kitumbalomo,Kigonsera,Kihangimahuka na Lukarasi.


Alisema, katika kuhakikisha kuwa zoezi linatekelezwa kwa ufanisi,Halmashauri imeorodhesha na kupata wakulima ambao wamenufaika na mpango huo  ambapo wataalam wa kilimo kutoka maeneo hayo wameelekezwa namna ya kusimamia zoezi hilo. Kisima, ameishukuru Serikali kwa kufanikisha upatikanaji wa mbegu  kwani zitasaidia sana kuongeza uzalishaji katika ngazi ya kaya, Halmashauri,mkoa na Taifa.

Akizindua mpango huo na kukabidhi mbegu kwa wakulima, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya Samwel Komba amewataka wakulima waliobahatika kupata mbegu hizo kuzitumia vizuri na kushirikiana na wataalam wa kilimo ili waweze kupat mavuno mengi.

“kimsingi sisi kama Halmashauri tunaishukuru sana Serikali kwa kuwezesha kupata mbegu hizo,tunaamini zitasaidia sana kuinua  uzalishaji na hali ya uchumi kwa wakulima na Halmashauri yetu na kuleta mabadiliko chanya”alisema Komba.


Amewataka maafisa kilimo na watendaji wa vijiji  kuhakikisha mbegu hizo zinawafikia walengwa katika maeneo husika na kuepuka kugawa kwa viongozi au kwa kujuana.

Alisema, mbegu hizo zimetolewa kwa wakulima  kama fidia na janga la korona na lina lengo la kuongeza uzalishaji kwa wakulima wa Halmashauri hiyo na kuishukuru serikali kwa msaada huo wa mbegu za mahindi.

Amewataka wasimamizi wa mpango huo kufikisha mbegu hizo kwa walengwa  na kuhakikisha wanazingatia maelekezo yaliyotolewa na serikali badala ya kupeleka mbegu hizo katika maeneo na kwa watu wasio stahili.

Alisema, serikali imetoa mbegu hizo ili kuwa  na matokeo chanja kwa kuongeza uzalishaji wa zao la mahindi katika Halmashauri hiyo na  kuongeza pato la kiuchumi kwa wakulima.

Komba alisema, lengo la  serikali kutoa mbegu hizo ni kuongeza uzalishaji wa mahindi sambamba na kutatua changamoto ya ajira kwa wananchi hasa vijana kupitia sekta ya kilimo ambayo kwa muda mrefu imeleta mafanikio makubwa kwa wakazi wa Mbinga na maeneo mengine ya mkoa wa Ruvuma.

Baadhi ya wakulima waliopata mbegu  hizo Jakson Lwena na Ester Mapunda wameishukuru Serikali kwa kuwapatia msaada huo wa mbegu ambao unakwenda kuongeza uzalishaji wa mahindi katika maeneo yao.

Hata hivyo,wameiomba serikali kuangalia uwezekano wa kutoa mbegu za mazao mengine kama maharage,mpunga na hata  kahawa  mazao  yanayostawi vizuri katika wilaya ya Mbinga ili waweze kupanua wigo wa kilimo na kujinasua na umaskini.

 

Kaimu Afisa kilimo wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma Deusdedit Kisima kushoto,akimuonesha Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo Samwel Komba sehemu ya shehena ya mbegu bora za mahindi zilitolewa kwa wakulima wa Halmashauri hiyo kwa ajili ya kuongeza uzalishaji mashambani.

 Picha 1 Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma Samwel Komba kushoto,akimpa mfuko wa mbegu ya mahindi mkulima wa kijiji cha Mkako Ester Mapunda zilizotolewa na serikali kwa ajili ya kuwasaidia wakulima kuongeza uzalishaji na kuleta tija.

Picha zote na Muhidin Amri.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...