Wanawake kutoka maeneo mbalimbali waliohudhuria
tukio hilo la utoaji tuzo zilizotolewa na TWCC kwa mwaka 2021 wakiburudika kwa
kucheza muziki uliokuwa ukipigwa wakati wa shughuli ikiendelea.
Mwenyekiti TWCC akizungumza kabla ya kumkaribisha
mgeni rasmi ambaye ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais-Muungano na
Mazingra Ummy Mwalimu.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais-Muungano na Mazingra Ummy Mwalimu ajadiliana jambo na viongozi wa TWCC.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais-Muungano
na Mazingira Ummy Mwalimu akiangalia moja ya jarida wakati wa hafla hiyo
ikiendelea.
Picha mbalimbali za matukio katika hafla ya utoaji wa tuzo katika maadhimisho ya wiki ya viwanda ya wanawake Tanzania kwa mwaka 2021.
Na Said Mwishehe, Michuzi TV
WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano
na Mazingira Ummy Mwalimu amesema atahakikisha anaanzisha dirisha la wanawake
katika Wizara hiyo ili kuwezesha
upatikanaji wa haraka wa vibali vya kimazingira kwa wanawake watakaokuwa
wanahitaji kuanzisha viwanda na biashara mbalimbali vinavyohitaji vibali vya
ofisi yake.
Aidha amesema umefika wakati kutambua adui ya
mwanamke si mwanamke bali adui ya mwanamke ni umasikini, hivyo wanawake wote
wana kila sababu ya kushikana mkono na kunyanyuana katika kuchangamkia fursa
zilizopo nchini.
Waziri Ummy Mwalim ambaye aliyekuwa mgeni rasmi amesema hayo wakati akitoa hotuba yake kwenye hafla ya utoaji tuzo katika maadhimisho ya Wiki ya Viwanda ya Wanawake Tanzania kwa mwaka 2021 yaliyokwenda sambamba na utoaji tuzo za wanawake katika viwanda 2021.Tuzo hizo zimetolewa na Chemba ya Wanawake Wafanyabiashara Tanzania(TWCC).
Amefafanua katika kuhakikisha wanawake wanaendelea
kupata fursa kuna mambo mengi Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais Dk.John
Magufuli yakiwmo ya kuweka mazingira mazuri ya kufanya shughuli ambazo
zitachangia kuleta uchumi nchini.
"Kuna hatua mbalimbali ambazo zimeendelea
kuchukuliwa na Serikali ya Awamu ya Tano katika kuweka mazingira mazuri ya
wanawake kushiriki katika shughuli za maendeleo, nakumbuka nikiwa Wizara ya
Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia ,Wazee na Watoto nilikuwa mkereketwa wa haki
sawa kati ya wanawake na wanaume, na hii nimekuwa nikiifanya kwa muda mrefu
sana.
"Naomba kutumia fursa hii kuwahakikisha
wanawake wote nchini katika Wizara ambayo niko sasa hivi, tutaanzisha dirisha
ambalo lenyewe litakuwa mahususi kabisa kusaidia wanawake hasa katika kupata
vibali vya kimazingira pindi wanapotaka kuanzisha viwanda au wanapohitaji aina
yoyote ya kibali kutoka Wizara yetu.Tunataka wanawake wanapokuja kwetu wawe
wanapewa kipaumbele kupita dirisha hilo,"amesema Waziri Ummy Mwalimu.
Aidha amewapongeza TWCC kwa kuandaa tuzo hizo kwa
ajili ya kutambua mchango wa wanawake katika sekta ya viwanda na tuzo ambazo
zimetolewa kwa taasisi za Serikali na binafsi zinakwenda kuchochea ukuaji wa
maendeleo ya nchi yetu."Nchi yetu iko kwneye uchumi wa kati, na wanawake
nao ni sehemu ya hatua hiyo ambayo nchi yetu imefikia."
Hata hivyo amesema umefika wakati wa kuhakikisha
TWCC wanapewa jukumu la kuhakikisha wanawake ambao wanahitaji kuendelezwa
kibiashara wanapita kwenye chemba hiyo ambayo ina uzoefu mkubwa katika eneo
hilo badala ya kufikiria kaunzisha mashirikisho mengine mengi kwa ajili ya
kusaidia wanawake.
Awali akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu Wizara ya Afya,Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto (Idara Kuu Maedeleo ya Jamii) Mkurugenzi wa Idara ya Mtoto katika Wizara hiyo Mwajuma Magwiza amesema Serikali imeendelea kutenga fedha na kuwapatia wanawake fursa katika kushiriki shughul za kiuchumi na kupambana na umasikini ili kujiletea maendeleo .
Aidha Serikali imeweka mazingira rafiki kwa
wanawake wajasiriamali kupata mikopo yenye masharti nafuu na kuondoa riba
kwenye mikopo inayotokana na fedha hizo, hiyo ni pamoja na uanzishwaji mifuko
46 ya uwezeshaji kiuchumi ambayo yote inawezesha wanawake kiuchumi.
"Kupitia mfuko wa maendeleo ya wanawake kwa
fedha zinazotengwa kupitia vyanzo vya ndani vya mamlaka za Serikali za Mitaa
kiasi cha Sh. 63,489,080.00 zimetolewa kama mikopo na kunufaisha vikundi 938,802
kwa kipindi cha miaka mitano 2015 hadi 2020,"amesema.
Pia amesema katika kipindi cha kuanzia Julai hadi
Desemba 2020jumla ya Sh.bilioni nne
zilitolewa kwa vikundi vya kiuchumi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.Serikali
imefanya marekebisho ya sheria ya fedha za Mamlaka za Serikali za Mitaa ya
mwaka 2018 ,kifungu cha 37 A, ambacho kinaelekeza mamlaka hizo kutenga asilimia
10 ya mapato ya ndani.
"Dirisha la Wanawake la Benki ya Posta
Tanzania linaendeleza huduma zilizokuwa zikitolewa na iliyokuwa Benki ya
Wanawake Tanzania kupitia dirisha hilo , kuanzia Julai 2020 hadi Desemba 2020,
mikopo yenye thamani ya Sh.9,994,830,000 imetolewa kwa wajasiriamali 5,234
kutoka katika mikoa 26 ya Tanzania Bara,"amesema.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...