Charles James, Michuzi TV
WAZIRI wa Katiba na Sheria, Prof Palamagamba Kabudi amesema Kiswahili ni lugha ya 10 duniani kwa kuwa na wazungumzaji wengi kwahiyo sasa Kiswahili ni lugha ya kimataifa .
Pia amesema Sheria 449 itaanza kuwekwa katika mfumo wa kutumia lugha ya Kiswahili kuanzia mahakama za mwanzo hadi mahakama kuu.
Kabudi ameyasema hayo leo jijini Dodoma wakati akifungua baraza la wakurugenzi wa sheria kutoka taasisi za serikali.
Waziri Kabudi amesema Kiswahili ni lugha ya Taifa lakini sasa inazungumzwa na nchi nyingi na kutumika miongoni mwa vyombo vya habari vya kitaifa na kimataifa.
“Maafisa wanaotoka Nchi ya Ufaransa na wanataka kuja kufanya kazi katika nchi za afrika lazima wasome na wafaulu somo la Kiswahili bila hivyo hawapati nafasi,” Amesema Prof Kabudi.
Amesema maamuzi yaliyofanywa na serikali ya awamu ya tano na kuendelezwa na serikali ya awamu ya sita kutumia lugha ya Kiswahili katika sheria sio kwa sababu watanzania hawajui kiingereza bali ni kwa sababu ndio lugha yao ya Taifa na lugha ya ukombozi ambayo sasa ina hadhi na heshima ya lugha ya kimataifa.
Kwa mujibu wa Waziri Kabudi amesema Jitihada hizo za kukifanya Kiswahili kutumika katika sheria zilianza tangu 1958 na Hayati Mwalimu Julius Nyerere.
“Namshukuru sana Mwalimu Nyerere kwa kusimamia zoezi hilo kwa ufasaha na serikali ya awamu ya sita ambayo nayo imesaidia leo tunaongelea utekelezaji wa sheria ya bunge ya matumizi ya lugha ya Kiswahili katika sekta ya sheria,” Amesema.
Amewataka wadau wote kuunga mkono juhudi za serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan katika zoezi la kusimamia matumizi ya lugha ya Kiswahili katika tasnia ya sheria na utoaji wa haki nchini.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...