Na Said Mwishehe, Michuzi TV
Fuatilia historia ya kijana Ahmed Khatibu maarufu Ahmed Zolla ambaye kwa sasa anaishi mkoani Morogoro ni miongoni mwa Watanzania walioamua kwa hiyari yao kuachana na matumizi ya dawa za kulevya.

Khatibu alizaliwa mwaka 1982 visiwani Zanzibar alianza kujihusisha na utumiaji wa dawa za kuelevya akiwa na umri wa miaka 14, alianza kujihusisha na dawa za kulevya kwa lugha rahisi akiwa mtoto. Kwa Tanzania mtoto ni yule aliyekuwa na umri chini ya miaka 18, Inasikitisha.

Tunafahamu changamoto wanazopitia watumiaji wa dawa za kulevya, wanapitia magumu mno, wanaishi maisha ya kutoaminika kutokana na aina ya tabia ambazo watumiaji wengi wa dawa za kulevya wanazo.
Anayetumia dawa za kulevya kuiba, kupora, kukaba na kufanya kila aina ya matendo ya hovyo ni jambo la kawaida.

Ndio nawazungumzia watumiaji wa dawa za kulevya ambao wengine tunapishana nao barabarani, wachafuuu. Unajua kwanini wanakuwa wachafu? Jibu ni kwamba wakioga wanaondoa Stimu, hivyo hawako tayari kuiondoa yaaani atumie fedha kuipata halafu kirahisi tu aiondoe kwa kuoga, kwake hapana, hayuko tayari.

Kijana Khatibu amepitia maisha yote wanayoishi Waraibu, anaeleza hatua kwa hatua jinsi ambavyo aliishi wakati anatumia dawa za kulevya.
Aliishi maisha ya hovyo sana, alipora,aliiba na wakati mwingine alilazimika kudanganya.

Aina ya maisha aliyopitia , ndiyo yaliyomfanya kwa hiyari yake kuamua kuachana na utumiaji wa  dawa za kulevya, ameamua kuwa shuhuda wa kueleza magumu na machungu aliyopitia , hataki kurudi nyuma na moyo wake umebaki na machungu kutokana na jinsi ambavyo ameishi maisha ya hovyo, anaumia kwa muda alioupoteza.

Kupitia makala haya maalum ,Khatibu anafafanua hatua kwa hatua alivyoingia kutumia dawa za kulevya na hadi alipoamua kuacha kutumia dawa hizo."Niliingia katika utumiaji wa dawa za kulevya kutokana na kukaa vijiweni na maskani.

"Kwa sasa nimeacha , nimekuwa nikihamasisha vijana wengine kuacha, nimeamua kuanzisha Sober House mkoani Morogoro, inaitwa Free at Last Sober House na huu ni mwaka wa nane nipo Morogoro naendelea na kazi hii.

Kuhusu athari za dawa za kulevya Khatibu anaeeleza zipo nyingi, ukiondoa watumiaji wengi wa dawa za kulevya kuwa na HIV na TB, pia kuna madhara mengine mengi ya kiafya, mtumiaji wa  dawa za kulevya ni rahisi kupata magonjwa yasiyoambukiza .

"Nimepata strock ( kupooza ) mkono kwasababu ya kutumia dawa za kulevya,wakati natumia nilikuwa najidunga sindano, hivyo imekwenda kuua mishipa ya mkono na kunifanya nipooze, kuna wengine wameathirika HIV kwasababu ya kuchoma sindano. Wapo ambao wamepata TB,"anaeleza.

Katika kuhakikisha anajiondoa kwenye utumiaji wa dawa za kulevya ametumia njia mbalimbali ,alikwenda hospitali lakini hakuweza kuacha kwasababu hakupata elimu kuhusu madhara ya dawa za kulevya."Niliacha baada ya kwenda Sober House, nilipata elimu ya kutosha, nashukuru Mungu nimeacha na sasa nahamasisha wengine kuacha.

"Lakini katika kuacha huko pia nilifuata hatua 12 ambazo ni kanuni rahisi ya kumsaidia anayetumia dawa za kulevya, hatua ya kwanza ni kufungua akili kwamba nataka kuacha , pili nia ya kweli. Ninachoweza kueleza kabla ya kuingia katika hizo hatua unachotakiwa kukifanya ni  kuwa muwazi na uwe na  hamu ya kile unachotaka kufanya,"anasema Khatibu.

Akifafanua zaidi anasema pamoja na kuacha kutumia dawa za kulevya,changamoto kubwa ni kuaminika katika jamii, ni ngumu jamii kuamini kama umeacha."Nimetumia dawa kwa miaka 12 , sasa kumtengenezea mtu imani ni changamoto, hivyo nia inabaki kwao mwenyewe, ukiaminiwa au usipoaminiwa unakuwa mwenyewe."

Pamoja na hayo anaeleza katika Sober House nyingi kinacholiwa ni mboga za majani, ugali na maharage na hivyo ndivyo vyakula ambavyo vinamuwezesha aliyekuwa anatumia dawa za kulevya kupata afya na nguvu."Tunakula hivyo vyakula tu lakini ladha haipo mdomoni."

Aidha Khatibu anasema kuwa changamoto nyingine anayokutana nayo mtumiaji wa  dawa za kulevya anapoamua kuacha kutumia ni maradhi."Unapoacha kutumia dawa za kulevya kuna maradhi mengi yanaibuka mwilini,lakini nashauri vijana na Watanzania kuachana na kutumia dawa za kulevya."

BAADA YA KUACHA 

Khatibu anasema hivi " Baada ya kuacha dawa za kulevya imenichukua miaka mitano nikaingia hatua ya pili kuoa, na ndugu zangu niliwaambia nataka kuwa mtu mzima na moja kwa moja wakaamini nimebadilika, nimetumia dawa za kulevya kwa miaka 12, nilianza nikiwa na miaka 14 tangu unga ukiwa bure.

"Nakumbuka kuna mabraza walikuwa wanatoka Ulaya wanakuja maskani kule Zanzibar na mimi nikawa napenda kuwa nao na walikuwa wanakuja na zawadi, hivyo nikajiukuta naingia kwenye kutumia na nakumbuka kete moja nilikuwa nanunua sh.200, sasa hivi inauzwa shilingi 5000 hadi sh.6000, nilianza kutumia mwaka 1994.

"Kwa hiyo kuingia ilikuwa rahisi lakini kutoka ikawa shida, nakumbuka nilikuwa nacheza sana mpira hivyo nilikuwa na mashibiki wengi,  leo najutia nimepoteza kipaji changu cha mpira.Wito wangu kwa vijana wengine kuishi bila kutumia dawa za kulevya inawezekana kwani hata mie imewezekana.

"Jambo la pili vijana wasijaribu kuiga, hata mimi huko awali nilikuwa na fedha nyingi, nilikuwa namiliki gari yangu aina ya Toyota, nilikuwa na kiwanja ambacho nilinunuliwa kutokana na uwezo wangu wa kucheza mpira, nilikuwa napata hela kupitia mpira.

"Cha ajabu kadri siku zilivyokuwa zinaenda nikawa ninajiibia mwenyewe, ukiwa mteja unajiibia mwenyewe, unakuwa na kiatu kizuri unauza, unakuwa na simu unaona haina maana unauza, hivyo nilikuwa naidanganya nafsi yangu mwenyewe, hadi mwisho nikaanza kuuza viti vya nyuma vya gari yangu.

"Alikuja jamaa yangu akaniambia gari yake viti vya nyuma watu wanalalamika wanaumia,hivyo akaniambia nimuuzie vyangu , kweli nikauza , nilianza tu kwa taratibu lakini mwisho nikauza na gari yangu kwa Sh.650,000 tu wakati gari niliinua Sh.milioni 3.5.Hakuna mteja anayeanza kumuibia mtu, mteja cha kwanza ataanza kujiibia mwenyewe, nimeuza nguo, nimeuza kila kitu na kibaya zaidi nimeuza nafsi yangu,"amesema Khatibu.

Anaongeza kwa sasa  moyo wake unaumia sana, hasa akikumbuka aliyopitia huko awali wakati anatumia dawa za kulevya, na kibaya zaidi akikumbuka aliyopitia na sasa moyo wake umekuwa na wivu, anatamani awe na maisha mazuri kushinda mwanzo.

"Lakini changamoto iliyopo ni kwamba walioacha kutumia dawa za kulevya hawaamini, kwangu nashukuru nimesimama imara, nahamasisha wengine waache, hivyo kila nikipata nafasi ya kuzungumza na Watanzania nawahamasisha kuacha kutumia dawa za kulevya," anasema Khatibu , kijana mpole,mcheshi, mtaratibu ambaye kwa sasa anaishi maisha huru baada kuachana na kutumia dawa za kulevya.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...