Baadhi ya watoto walioshiriki katika tamasha maalumu la siku moja la mpira wa watoto maarufu kama ‘All Stars Day’ lililoandaliwa na Magnet Youth Academy wakionesha medali walizoshinda wakati wa tamasha hilo. SGA Security ilikuwa mmoja wa wadhamini wa tamasha hilo.
Mkurugenzi Mtendaji wa SGA Tanzania, Eric Sambu akitoa medali kwa baadhi ya watoto walioshiriki katika tamasha hilo.
Na Mwandishi Wetu
KAMPUNI ya SGA Security imetangaza kuwa itaendelea kukuza vipaji vya vijana wenye umri mdogo kupitia academy za mpira nchini.
Hayo yalisemwa na Mkurugenzi Mtendaji wa SGA Tanzania, Bw. Eric Sambu wakati wa tamasha la mpira la siku moja maarufu kama ‘All Stars Day’ lililoandaliwa na Magnet Youth Academy ya Jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki.
Tamasha hilo la kila mwaka, liliwakusanya zaidi ya watoto 300 kutoka academy zote za Magnet ambapo SGA Security ilikuwa moja ya wadhamini. SGA pia inadhamini timu za mpira za chini ya umri wa miaka 17 na 19 ambazo zinashiriki kwenye Ligi ya Taifa ya vijana (National Youth League).
Bw. Sambu aliipongeza academy hiyo kwa kukuza vipaji ambapo vijana wengi wamechaguliwa kwenda kwa majaribio katika academy kubwa barani Ulaya.
Timu ya wauguzi wa SGA wakiwa na magari ya huduma ya kwanza walishiriki vilivyo katika tamasha hilo kuhakikisha washiriki hawaondoki na majeraha.
“Dira yetu kama SGA ni kutoa huduma za ulinzi lakini pia tunalipa kipaumbele suala la afya ndio maana tuna magari ya huduma ya kwanza kila kona ya jiji ili kusaidia pale ambapo kuna uhitaji. Matamasha kama haya ya michezo ni kichocheo kikubwa cha afya njema katika Nyanja mbalimbali ikiwemo mchezo wa soka,” alisema Bw. Sambu.
Mwenyekiti wa Magnet Sports Academy Bw. Tuntufye Mwambusi, aliipongeza SGA na makampuni mengine kwa kuendelea kuchangia tamasha hilo la kila mwaka huku akibainisha kuwa SGA imekuwa mdhamini kwa miaka mitatu sasa.
Alisema academy yake imezalisha wachezaji katika ngazi mbalimbali za kitaifa. “Wachezaji wetu wana upeo mkubwa kwani wameshiriki katika matamasha makubwa ya mpira nchini Sweden, Norway, Ujerumani na nchi za Kiarabu (UAE). Tumepata pia fursa ya kufundishwa na makocha wakzoefu kutoka Uispania na wengi wa wachezaji wetu wameshaenda kwa majaribio barani Ulaya,” alisema.
SGA Security pia imedhamini matukio mengine ya kimichezo kama marathon za NMB, CRDB na NBC kama sehemu ya kuchangia katika jamii huku kampuni hiyo ikiadhimisha miaka 50 tangu kuanzishwa kwake.
SGA Security ndio kampuni kongwe ya ulinzi nchini na imeajiri zaidi ya watanzania 6000. Kampuni hiyo inafahamika kwa usafirishaji wa fedha kote nchini, huduma za ulinzi katika sekta zote, huduma za vifurushi, huduma za alarm, tracking na huduma za ulinzi zinazotumia umeme.
“SGA ndio kampuni pekee ya ulinzi yenye cheti cha ISO 18788 ambacho huthibitishwa nchini mahususi kwa viwango fulani vya huduma za ulinzi. Hii inathibitisha namna tunavyowajali wateja na ubora wa huduma zetu,,” alisema Bw. Sambu.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...