Na Khadija Kalili, Kibaha
Viongozi wa dini Mkoani wa Pwani wamekemea vikali migogoro ya ardhi na vitendo vya ukatili vinavyofanyika Mkoani hapa na kuiomba serikali iwashirikishe katika kutafuta Suluhu ya kulimaliza kabisa changamoto hizo.
Hayo yalisema leo na Mwenyekiti Mwenza wa Kamati ya Amani ya Mkoa wa Pwani Padri Beno Kikudo Paroko wa Parokia ya Tumbi iliyopo Kibaha alipokuwa akiongoza Ibada katika kongamano la viongozi wa dini na Mkoa katika maombi ya kumuombea Rais wa awamu ya sita Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ambaye anatimiza mwaka mmoja tangu aingie madarakani mwezi Machi mwaka jana.
Padri Kikudo alisema umefika wakati Sasa kwa viongozi wa dini kuwahubiria waumini kuachana na migogoro ya ardhi na vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia na mauaji ambayo yamekuwa yakifanyika ndani ya jamii pia wakulima na wafugaji huku wote wakiwa ni waumini wa makanisa wapo wanapokwenda kusali misikitini hivyo kwa sauti moja viongozi hao wamesema wanaomba baraka za Serikali Ili waweze kupaza sauti zao kukemea mambo maovu ikiwemo ukiukwaji wa haki za binadamu unaofanywa na jamii.
"Sisi kama viongozi wa dini tunao wajibu wa kukemea na kuishauri Serikali nini kifanyike ili kukomesha vitendo hivyo viovu ambavyo havikubaliki na Imani ya dini yeyote na Serikali pia tunaomba Kamati zetu za amani ziwajibike ili tufute kabisa haya mawazo maovu kwa jamii yetu ya Pwani" alisema Padri Kikudo.
Mwenyekiti Mwenza wa Kamati hiyo ambaye pia ni Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Pwani Hamisi Mtupa alisema kuwa mbali ya maombi na Dua maalumu walizoomba viongozi hao wa dini kufuatana na Imani zao kwa Rais Samia Suluhu ameisisitiza suala la waumini wote kutilia maanani suala zima la Sensa ya Watu na makazi itakayofanyika ifikapo mwezi Agosti mwaka huu.
Mbali yakumuombea maisha marefu Mheshimiwa Rais Samia pia Viongozi hao wameomba kwa Mungu Ili aiepushe nchi na majanga mbalimbali ikiwemo ugonjwa wa Covid 19 ambao umetikisa ulimwengu mzima huku akiwataka waumini wote kujitokeza kwa wingi kupata chanjo Ili kujikinga na ugonjwa huo.
"Viongozi wa dini tunao wajibu wa kuomba dua kupongeza mambo yote mazuri aliyoyafanya Rais wetu Mama Samia, viongozi wa dini tunatakiwa kuzisemea changamoto zilizopo pia kuinua mikono kumuombea Rais wetu huu ni muda sahihi kwetu tumuombe Mungu atuondoshee majanga mbalimbali yanatokea katika nchi za wenzetu Ukraine na Urusi na kuifanya Tanzania iwe kisiwa cha amani duniani"
Mkuu wa Mkoa wa Pwani Alhaji Abubakari Kunenge aliyekuwa mgeni rasmi katika kongamano hilo alisema kuwa kwa niaba ya wasaidizi wake akiwemo Mhandisi Hajat Mwanasha Tumbo,Mkuu wa Wilaya Kibaha Sara Msafiri pamoja na Kamati ya Ulinzi na Usalama Mkoa wa Pwani wamewashukuru viongozi hao wa dini na wote walijitokeza kufanikisha huku akisisitiza kwa kusema kuwa yeye anazungumza kama mwakilishi wa Rais Samia na kwamba wote tunafahamu kuwa nchi yetu haina dini na hatuna kifungu chochote katika Katiba yetu kinachohusu kufungamana na dini.
"Niendelee kumshukuru Rais wetu Samia Suluhu Hassan kwa kutoa heshima na kuendelea kushirikiana na viongozi wa dini nchini hivyo na sisi Pwani tumeungana pamoja katika kumuombea Rais wetu , nchi yetu na Dunia nzima kwa ujumla wake"alisema RC Kunenge.
"Serikali ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu imedhamiria kwa dhati kuifungua nchi yetu hivyo basi sisi viongozi wa Pwani ambao ni Katibu Tawala Mhandisi Mwanasha Tumbo,Mkuu wa Wilaya ya Kibaha Sara Msafiri na Wakuu wengine wa Wilaya tumedhamiria kubadilisha Mkoa wa Pwani hivyo tunaomba msaada wenu viongozi wa dini"alisema RC Kunenge.
Akizungumzia kuhusu migogoro ya ardhi ndani ya Mkoa wa Pwani alisema kuwa changamoto nyingi zinatokana na watu kutofuata sheria ,hawana heshima,walarushwa na wavamizi wengi huvamia maeneo ya watu ambayo tayari yamepimwa,hivyo hakuna sababu ya kuwa na migogoro ya wakulima na wafugaji wakati taratibu zipo tutajitahidi kwa kiwango tutakacho jaaliwa.
Kongamano hilo limewakutanisha Viongozi mbalimbali wa kidini wakiwemo mapadri wachungaji kutoka madhehebu mbalimbali yaliyomo Pwani pamoja na Maimamu na Masheikh na Jumuiya za akina mama wa Kiislamu na Kikristo.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...