Na Saidina Msangi na Joseph Mahumi, WF, Dodoma
Waziri
wa Fedha Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), amesema kuwa Tanzania
ni nchi ya mfano Afrika kwa kutimiza viashiria vya Malengo ya Milenia
ambapo imefanya vizuri katika sekta za Afya, Elimu, Maji.
Dkt.
Nchemba alitoa ufafanuzi huo wa ukomo wa Bajeti kwa mwaka 2024/25,
wakati alipokuwa akiweka jiwe la msingi katika jengo la Taaluma la Chuo
cha Uhasibu Arusha (IAA), jijini Dodoma.
Alisema
kuwa katika makadirio yaliyowasilishwa bungeni Serikali inatarajia
kutumia kiasi cha shilingi trilioni 49.34 ambapo fedha za maendeleo
zilizotengwa ni kiasi cha shilingi trilioni 16.
‘‘Fedha
za maendeleo ni trilioni 16, fedha hizi zinatarajiwa kutumika katika
Miradi ya Kilimo cha Umwagiliaji, Elimu ya Msingi na Elimu ya Juu,
Ujenzi wa Barabara, Maji, Umeme Miradi ya Afya pamoja na ukamilishaji wa
Bwawa la umeme la Mwalimu Nyerere’’, alifafanua Dkt. Nchemba.
Alisema
kiasi cha fedha kinachotarajiwa kutumika katika uchaguzi ni shilingi
bilioni 600 kwa mwaka unaofuata na kwa mwaka huu ni Shilingi bilioni 300
inayoenda kwenye uchaguzi.
‘‘Uchaguzi
ni matakwa la kikatiba sio maamuzi ya Serikali bali ni kuhakikisha kuwa
matakwa ya kikatiba yanatimizwa hivyo katika bajeti ya Sh. trilioni 49
kiasi kitakachoitumika katika kuendesha uchaguzi kwa mwaka ujao ni
shilingi bilioni 300, alifafanua Dkt. Nchemba.
Akifafanua
kuhusu fedha zinazotarajiwa kutumika katika maandalizi ya Kombe la
Mataifa ya Afrika (AFCON) 2027 linalotarajiwa kufanyika Tanzania Dkt.
Nchemba alisema kuwa Tanzania kuwa mwenyeji wa AFCON ni suala la
kujivunia kwani ni heshima kwa Taifa ambapo kiasi kilichotengwa ni Sh.
bilioni 200 tu katika bajeti ya shilingi. trilioni 49.
Akizungumza
kuhusu ugharamiaji wa Deni la Taifa Dkt. Nchemba alisema kuwa katika
sh. trilioni 49, deni halisi ni shilingi trilioni tano (5) pamoja na
riba ambayo haitazidi kiasi cha shilingi trilioni 10.
‘'Deni
lenyewe ni miradi ya maendeleo inayoonekana kama ni ujenzi wa reli ya
kisasa, kivuko cha Kigongo Busisi Mwanza, ujenzi wa mabweni ya shule,
tumejenga mabweni ya vyuo vikuu karibu kila chuo kimepata kwa mradi
mkubwa wa fedha za Benki ya Dunia ili kuwawezesha wanafunzi wakae katika
mazingira salama’’,
alifafanua Dkt. Nchemba.
Aliongeza
kuwa jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita zinaonekana kwani fedha za
maendeleo yanayotekelezwa yanajitambulisha kwani zimegusa mpaka kwenye
maeneo ambayo hayajawahi kupata maendeleo.
‘‘Vijiji
ambavyo havijawahi kupata barabara sasa vina madaraja na barabara
kuunganisha vijiji na sasa zinaenda kujengwa barabara za kudumu, vituo
vya afya vimejengwa kwenye kila makao makuu ya tarafa pamoja na kuweka
vitendea kazi ambapo ndani ya miaka mitatu mikoa yote ina CT SCAN ambapo
awali zilikuwepo 6 nchi nzima’’, alifafanua Dkt. Nchemba.
Waziri
wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu (Mb), akizungumza
wakati wa hafla ya Uwekaji Jiwe la Msingi la Ujenzi wa Jengo la Taaluma
la Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA) Kampasi ya Dodoma, katika eneo la
Njedengwa, jijini Dodoma, ambapo alitumia jukwaa hilo kufafanua ukomo wa Bajeti kwa mwaka 2024/25.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...