Na. Calvin Katera - Arusha.

Taarifa ya awali ya utafiti wa muundo wa utalii endelevu (Tourism Sustainable Model) Hifadhi ya Taifa Serengeti imewasilishwa na kujadiliwa leo Mei 25, 2026 kwa wadau zaidi ya 81 wa utalii, wawekezaji na Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) katika semina iliyofanyika ndani ya hoteli ya Mount Meru, jijini Arusha.

Tafiti hiyo iliyofanywa na wataalamu mbalimbali katika nyanja za utalii, uhifadhi na usimamizi wa fedha kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Chuo cha usimamizi wa wanyamapori (MWEKA) ililenga kuibua namna bora ya utalii wenye faida za kiuchumi bila kuathiri mazingira na ikolojia ya wanyamapori.

Akifungua Semina hiyo kwa niaba ya Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini TANAPA, Dkt. Robert Fyumagwa alieleza kuwa Dira ya Taifa ya 2050 imelenga kuhakikisha uhifadhi na matumizi endelevu ya rasilimali za asili ni kwaajili ya manufaa ya watu wote hapa nchini huku akibainisha kuwa semina hii isiishie kuthibitisha matokeo ya tafiti badala yake itoe suluhisho la vitendo.

“Tanzania imejidhatiti kupitia Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 kuhakikisha uhifadhi na matumizi endelevu ya rasilimali za asili zinawanufaisha kizazi cha sasa na vijavyo. Kazi tunayoijadili leo inaendana na azma hiyo ya Taifa.” alisema Fyumagwa.

Akiwasilisha ripoti hiyo mmoja wa timu ya washauri wataalamu Dkt. James Wakibara alieleza kuwa tafiti inaonyesha kuwa Hifadhi ya Taifa Serengeti inapokea zaidi ya watalii laki tatu kwa mwaka na bado wanaongezeka. Na moja ya sababu zinazoibua changamoto ni pamoja na baadhi ya wadau kutosimamia taratibu zilizowekwa na hifadhi (GMP - General Management Plan) katika kuwakarimu wageni pale wanapowapokea.

Naye, Mtaalamu Mshauri wa Mazingira Dkt. Flora Tibarazwa alieleza kuwa kutokana na ripoti iliyowasilishwa, TANAPA inauwezo wa kuandaa mikakati itakayowaongoza wawekezaji na wadau wa utalii kwa kuwapatia mikataba yenye miongozo itakayosimamia taratibu na sheria za uendeshaji wa biashara zao ili kuepuka uharibifu wa mazingira.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha watoa huduma za utalii nchini (TATO) na Mmiliki wa Kampuni ya Tanganyika Wilderness Camps (TWC) Willy Chambilo alieleza kuwa msongamano wa wageni hifadhini unaweza kuthibitiwa ikiwa siku za kuwakarimu wageni zitarejewa na kufanyiwa maboresho kulingana na mapendekezo ya wadau hao.

Akimwakilisha Kamishna wa Uhifadhi TANAPA, Naibu Kamishna wa Uhifadhi na Maendeleo ya Biashara Masana Mwishawa alieleza kuwa ushirikiano uliooneshwa na watafiti, wadau, wawekezaji na taasisi za uhifadhi nje na ndani ya nchi kupitia ripoti iliyowasilishwa itachangia maboresho ya mapendekezo yaliyoainishwa kwakuzingatia sheria na taratibu zinazosimamia uhifadhi na utalii ili kuendeleza uhifadhi endelevu katika sekta ya utalii.

Tafiti hii ilianza kufanyika Oktoba 2024 ikidhaminiwa na Serikali ya Ujerumani kupitia Benki ya Maendeleo ya KFW na Frankfurt Zoological Society na imekuwa kielelezo kikubwa cha tumaini kwa wadau na wawekezaji ndani ya Hifadhi ya Taifa Serengeti wakitegemea maboresho juu ya mapendekezo yaliyotewa na wadau hao.














Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...