Na: Calvin Gwabara – Dodoma.
Mamlaka
ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA) imeeleza kuwa imefanikiwa kuokoa
zaidi ya tani milioni 2.1 za chakula msimu uliopita na ekari zaidi ya 700,000 baada
ya kudhibiti milipuko ya visumbufu vya mazao, ikiwemo ndege aina ya Kwelea
kwelea, Panya na Viwavi Jeshi.
| Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. James Kinyasi Millya (Kulia) akimsikiliza Mkurugenzi Mkuu wa TPHPA Prof. Joseph Ndunguru |
Akizungumza
jijini Dodoma kwenye maonesho ya wakulim Nanenane kitaifa, Mkurugenzi Mkuu wa
TPHPA, Prof. Joseph Ndunguru, amesema mamlaka hiyo ina mchango mkubwa katika
kuhakikisha Tanzania inafikia utoshelevu wa chakula unaofikia asilimia 130,
kupitia udhibiti wa wadudu, magonjwa ya mimea na visumbufu mbalimbali
vinavyohatarisha uzalishaji wa mazao.
Amesema
katika msimu uliopita, TPHPA ilidhibiti uvamizi wa ndege aina ya kwelea kwelea
wapatao milioni 231 waliovamia skimu kubwa za mpunga, hususan maeneo ya Mbarali
Mkoani Mbeya, Bariadi Mkoani Simiyu na Kilosa Mkoani Morogoro, hatua
iliyosaidia kuokoa zaidi ya tani milioni 1.6 za chakula.
“Kwa
mfano, tunadhibiti visumbufu milipuko kama vile ndege aina ya Quelea quelea,
ambao wanaharibu nafaka kwa kula mpunga, mtama na uwele. Msimu uliopita
tulikuwa na uvamizi wa ndege hao wapatao milioni 231 katika skimu kubwa za
mpunga. Tulienda kuwazuia kwa kutumia ndege maalum na tuliweza kuokoa zaidi ya
tani milioni 1.6 za chakula,” amesema Prof. Ndunguru.
Aidha,
amesema mamlaka hiyo ilidhibiti uvamizi wa panya katika mikoa 19 na wilaya 54,
ambapo hatua zilizochukuliwa ziliwezesha kuokoa takribani ekari 408,000 za
mazao huku kwa upande wa viwavi jeshi vamizi waliokoa zaidi ya ekari 219,000,
ambapo udhibiti wake uliwezesha kuokoa tani 519,000 za mahindi.
Amesema
jitihada hizo zimechangia kuongeza uzalishaji wa mahindi nchini na kuipandisha
Tanzania kutoka nafasi ya tatu hadi ya pili kwa uzalishaji wa mahindi barani
Afrika, ikitanguliwa na Afrika Kusini.
Kwa
upande wake, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Mhe. James Kinyasi Millya, ameipongeza TPHPA kwa juhudi zake za kuhakikisha
wakulima wanapata masoko ya uhakika kwa mazao yao kwani uzalishaji mkubwa bila
soko kunaweza kuwakatisha tamaa wakulima.
Amesema
Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki iko
tayari kushirikiana na TPHPA katika kutafuta masoko ya mazao ya Tanzania
kupitia balozi za nchi hiyo zilizopo katika mataifa mbalimbali duniani.
“Jambo
kubwa ambalo nimelifurahia ni jinsi mnavyopambana kutafuta masoko ya wakulima
wetu. Tunahimiza kuzalisha sana, lakini mwisho wakikosa masoko na kupata hasara
wanaweza kukata tamaa. Hivyo, nyinyi mnatusaidia sana kwa upande wa Serikali
kuondoa changamoto hiyo,” amesema Mhe. Millya.
Amesema
ushirikiano huo ni sehemu ya maagizo maalumu ya Rais kwa mabalozi wa Tanzania
kushirikiana na taasisi zinazohusika na uzalishaji na biashara ya mazao ili
kuwezesha bidhaa za wakulima wa Tanzania kupata masoko katika nchi
wanazowakilisha.
Mhe.
Millya ameitaka TPHPA kutumia fursa zilizopo katika masoko ya kimataifa,
akitolea mfano zao la ndizi zinazozalishwa Bukoba na kupelekwa katika baadhi ya
masoko ya nje, ikiwemo Marekani na Canada.
“Naomba
TPHPA iangalie fursa ya zao la ndizi za Bukoba zinazokwenda Marekani, Canada na
nchi nyingine, shirikianeni na balozi zetu kuona namna gani tunaweza kupeleka
ndizi zetu katika nchi hizo na kuongeza masoko kwa wakulima wetu,” amesema Mhe.
Millya.
Amesema
ushirikiano kati ya TPHPA na Wizara ya Mambo ya Nje ni muhimu katika
kuhakikisha mazao ya Tanzania yanapata masoko ya uhakika nje ya nchi, huku
akisisitiza kuwa Serikali itaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wakulima na
wadau wa sekta ya kilimo kuongeza uzalishaji na tija.
MATUKIO KATIKA PICHA KWENYE BANDA LA TPHPA


Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...