MAMLAKA ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) imewasili rasmi mkoani Morogoro Septemba 2, 2026 ikiwa na tuzo mbili za World Travel Awards 2026 zilizotwaliwa na Hifadhi zake za Selous na Mpanga-Kipengere, siku chache baada ya kutangazwa washindi katika hafla ya tuzo hizo iliyofanyika Agosti 28, 2026, Zanzibar. 


 Akizungumza katika hafla ya mapokezi ya tuzo hizo, iliyofanyika katika Ofisi za Makao Makuu ya taasisi hiyo Morogoro, Kaimu Kamishna wa Uhifadhi wa TAWA Mlage Y. Kabange amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa juhudi za kuitangaza Tanzania na vivutio vyake katika soko la kimataifa, akisema jitihada hizo zimechangia nchi kufahamika zaidi duniani. Ametaja filamu za Tanzania The Royal Tour na Amazing Tanzania kuwa miongoni mwa juhudi zilizoongeza mwonekano wa Tanzania, huku akiwapongeza pia watumishi wa TAWA, wananchi na wadau wa utalii ndani na nje ya nchi waliohamasisha na kupiga kura na kuziwezesha Hifadhi zake kushinda katika mashindano hayo.

Amesema mafanikio hayo yana uzito wa kipekee kwa kuwa yamepatikana katika mwaka wa kwanza kwa TAWA kushiriki mashindano hayo.

Kabange amesema ukubwa wa ushindi huo unaonekana zaidi kwa kuzingatia ushindani wa vivutio mbalimbali barani Afrika, akifananisha mafanikio hayo na timu inayotwaa ubingwa wa Afrika katika mchezo wa soka. “Tunaongelea mashindano ya Afrika. Kama kwenye mpira, haya ni mashindano ya CAF. Sisi tumekwenda kwenye fainali ya Afrika kwa mara ya kwanza na tumetoka na ushindi. Kwa hiyo siyo kitu kidogo,” amesema Kabange.

Amesema matokeo ya ushindi huo yameanza kujionesha baada ya wadau wa utalii kuanza kutafuta taarifa za namna ya kufika Mpanga-Kipengere mara tu baada ya tuzo kutangazwa Zanzibar. Kwa mujibu wa Kabange, kampuni moja ya ndege ya Zanzibar imeonesha utayari wa kuanzisha safari za moja kwa moja kwenda hifadhini humo mara miundombinu husika itakapokuwa tayari. Amesema kuwa mwitikio huo unaashiria fursa ya kuongeza watalii, mapato, uwekezaji na manufaa kwa jamii zinazozunguka maeneo hayo.

Kutokana na fursa hizo, Kabange amewakaribisha wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kuwekeza katika miundombinu, malazi na huduma nyingine za utalii katika maeneo ya TAWA. Amesema uzoefu wa mafanikio ya Selous na Mpanga-Kipengere umeipa Mamlaka ujasiri wa kuyapeleka maeneo mengine katika ushindani wa kimataifa, huku Makuyuni Wildlife Park na Hifadhi ya Pande yakiwa miongoni mwa yaliyotajwa. 

Kwa upande wake, Naibu Kamishna wa Uhifadhi Emmanuel B. Musamba, ndc amesema tuzo hizo zina maana kubwa kwa kuwa ni uthibitisho wa kimataifa wa ubora wa rasilimali za utalii za Tanzania na juhudi zinazofanywa katika kuzihifadhi. “Hii ni kura ya imani kwa Tanzania, ni kura ya imani ya kimataifa kwa utajiri wa rasilimali tulizonazo Tanzania, lakini pia kwa juhudi za uhifadhi na uwezo wa maeneo yetu ya wanyamapori kutoa uzoefu wa kipekee,” amesema Musamba.

Musamba amesema ushindi huo pia ni heshima kwa watumishi wa TAWA na wale waliotangulia katika jukumu la kulinda rasilimali za wanyamapori, wakiwemo waliopoteza maisha katika utekelezaji wa jukumu hilo. Amesema mafanikio hayo yanaongeza wajibu wa Mamlaka kuhakikisha usalama wa wanyamapori, ubora wa maeneo na uendelevu wake vinaimarishwa kadri Tanzania inavyopanua nafasi yake katika soko la utalii la kimataifa.

“Tuzo hizi mbili siyo mwisho, ni mwanzo wa safari,” amesema Musamba, akisisitiza kuwa heshima iliyopatikana lazima iambatane na wajibu wa kuhakikisha ukuaji wa utalii hauathiri rasilimali zinazoubeba, bali unaimarisha uhifadhi endelevu, uchumi wa jamii na mchango wa sekta hiyo kwa Taifa.

Tuzo hizo ziliwasili Morogoro zikisindikizwa na shamrashamra zilizorindima kuanzia Kituo cha Treni ya Mwendokasi (SGR) cha Jakaya Mrisho Kikwete hadi Makao Makuu ya TAWA ambako viongozi, maafisa, Askari wa TAWA , watumishi wa taasisi mbalimbali pamoja na baadhi ya wananchi walikusanyika kuzipokea. 

Selous imetwaa Africa’s Leading Tourist Attraction 2026, huku Mpanga-Kipengere ikitwaa Africa’s Leading Honeymoon Destination 2026 mafanikio yaliyoiwezesha TAWA kuibuka na tuzo mbili katika ushiriki wake wa kwanza.








 


Na Mwandishi Wetu
MAKAMU wa Rais, Deogratius Ndejembi, amelipongeza Shirikisho la Wenye Viwanda (CTI) kwa Tuzo za Rais kwa Mzalishaji Bora Viwandani (PMAYA), akisema zimekuwa chachu ya maendeleo ya sekta ya viwanda tangu kuanzishwa kwake miaka 19 iliyopita.

Alitoa pongezi hizo Septemba 2, 2026 jijini Dar es Salaam wakati wa hafla ya utoaji wa tuzo hizo, ambapo Kampuni ya SILAFRICA Tanzania Limited iliibuka mshindi wa kwanza wa jumla, huku Alliance One ikiwa mshindi wa pili na Tanzania Cigarette PLC ikishika nafasi ya tatu.

Kampuni ya vinywaji ya Bonite Bottlers Limited iliibuka mshindi kwa upande wa kampuni kubwa zinazotengeneza vinywaji visivyo na kilevi.

Makamu wa Rais alisema sekta ya viwanda imeendelea kukua kwa kasi na viashiria mbalimbali vya uchumi vinaonyesha mafanikio chanya ya sekta hiyo, akitolea mfano mwaka 2025 ambapo sekta ya viwanda ilikua kwa asilimia 5.2, ikilinganishwa na ukuaji wa asilimia 4.2 mwaka 2024.

Aidha, alisema mchango wa sekta ya uzalishaji katika Pato la Taifa mwaka 2025 ulifikia asilimia 5.9 na kwamba inakadiriwa kuwa asilimia 12 ya ajira rasmi na bidhaa zilizokuwa zinauzwa nje zilikuwa za viwandani.

“Haya ni mafanikio makubwa kwa takwimu, lakini lazima tujiulize viwanda vyetu vimekua kwa kiasi gani na je, ukuaji huu unaviwezesha kuwa na ushindani Afrika Mashariki na duniani na je, tunajipima kwa hayo au bado tunazalisha kwa kuangalia soko la ndani peke yake?” alihoji Makamu wa Rais.

Aidha, aliiitaka Wizara ya Viwanda na Biashara kukaa na wazalishaji wa saruji kuweka mipango ya kuhakikisha saruji inapatikana kwa wingi na inashuka bei na kurejea ilivyokuwa.

Alisema hivi sasa Watanzania wanalazimika kununua saruji kwa gharama kubwa kutokana na viongozi kushindwa kuratibu vyema uzalishaji wa bidhaa hiyo viwandani.

“Haya yanasababisha uhaba wa saruji na anayeumia hapa ni Mtanzania wa kawaida na Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Daktari Samia Suluhu Hassan, kwa maelekezo yake, anataka kuona Mtanzania anapata mfuko wa saruji kwa gharama nafuu,” alisema na kuongeza:

“Sasa nakuagiza Waziri wa Viwanda na Biashara, namwona hapa Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda, Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), kaeni pamoja mmalize hili suala ili Mtanzania apate saruji bei iliyokuwepo.”

“Nataka kuona maono ya Rais Samia kutaka Mtanzania wa kawaida anapata saruji kwa bei ya kawaida yanatekelezeka na ninataka kupata ripoti ya suala hilo baada ya kikao hiki. Kaeni mjadili suala hili na muandike ripoti tumkabidhi Rais,” alisema.

Mkurugenzi Mkuu wa Shirikisho la Wenye Viwanda (CTI), Leodegar Tenga, alisema PMAYA inalenga kutambua, kuthamini na kuenzi mchango wa sekta ya viwanda katika ukuaji wa uchumi wa Tanzania.

Alisema tuzo hizo pia ni jukwaa la wazalishaji na wadau wa viwanda kukutana, kujadiliana na kubadilishana uzoefu kuhusu namna ya kuendeleza sekta hiyo.

Tenga alisisitiza kuwa tuzo hizo zinapaswa kuwa kichocheo cha kuongeza tija, ubunifu na ushindani katika uzalishaji wa viwandani.

Aidha, Tenga alisisitiza umuhimu wa uzalishaji endelevu unaozingatia mazingira, Environmental, Social and Governance (ESG), akisema ESG inazidi kuwa muhimu katika upatikanaji wa fedha, uwekezaji, masoko na kuingia katika minyororo ya thamani ya kimataifa.

Alisema kwa PMAYA 19, CTI imeanzisha Mabalozi 10 wa ESG, ambao watafuatiliwa kwa mwaka mmoja ili kupima utekelezaji na matokeo ya kanuni hizo katika kampuni zao.

Alisema kampuni itakayofanya vizuri zaidi itatambuliwa kama ESG Champion katika PMAYA 20.









-Apanga kuitisha kikao cha wasafirishaji wa mizigo

-Aomba wakulima watumie mbolea zinazozalishwa nchini


WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema kuanza uzalishaji kwa kiwanda cha saruji cha Kigoma kutasaidia kuondoa tatizo la kupanda bei kwa bidhaa hiyo kwenye mikoa ya Magharibi mwa Tanzania.

Amesema Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amesisitiza katika dira yake ya uwekezaji kwamba kuwe na viwanda katika kanda mbalimbali za nchi ili kupunguza changamoto za gharama za usafirishaji. “Pale gharama za usafirishaji zinapopanda, bei ya bidhaa nayo hupanda,” amesema.

Ametoa kauli hiyo Bungeni jijini Dodoma, leo (Alhamisi, Septemba 03, 2026) wakati akijibu swali la Mbunge wa Kasulu Vijijini, Bw. Edibily Kazala Kinyoma, kwenye kipindi cha maswali ya papo kwa papo kwa Waziri Mkuu ambaye alitaka kujua kauli ya Serikali kuhusu kuanzisha tathmini ya gharama halisi za uzalishaji wa saruji nchini ili kuwe na bei elekezi itakayotoa unafuu kwa wananchi na kuchochea sekta ya ujenzi Tanzania.

Mbunge huyo amesema pamoja na uwekezaji uliofanyika kwenye sekta ya viwanda, bado kuna changamoto katika upande wa saruji kwani bei yake imekuwa ikipanda kwa kasi na baadhi ya maeneo imefikia zaidi ya sh. 25,000.

“Habari njema ni kwamba Mheshimiwa Rais tayari ameelekeza watu wanaotaka kuwekeza katika bidhaa hizi wapewe kipaumbele. Kwa taarifa nilizonazo, kule Kigoma kuna kiwanda kimojawapo cha saruji ambacho kiko katika hatua za utekelezaji. Lengo ni kuwa na viwanda vingine vinavyozalisha bidhaa hii katika maeneo ya magharibi mwa nchi ikiwemo Kigoma, Kagera na Katavi,” amesema.

Dkt. Mwigulu amesema kuwepo kwa viwanda kama hivyo kwenye mikoa na kanda tofauti kutasaidia kupunguza gharama za kusafirisha saruji kutoka Mtwara au Tanga kwenda upande mwingine wa nchi, jambo ambalo linaongeza gharama za usafirishaji na usambazaji.

Amesema amepanga kuitisha kikao kitakachowahusisha wasambazaji mbalimbali nchini ili kujadiliana nao namna ya kudhibiti ongezeko la bei na kuhakikisha wananchi hawaathiriki kwa kiwango kikubwa, jambo ambalo anaamini litasaidia kupunguza gharama za ujenzi na kuchochea maendeleo.

“Jambo hili la bei ya saruji linagusa maisha ya kila Mtanzania na kupanda kwa bei ya saruji hivi karibuni kumehusishwa pia na kupanda kwa bei za mafuta, jambo ambalo limeongeza gharama za usafirishaji. Serikali imeshakaa na wadau wa usafirishaji na kutafuta namna ya kupunguza gharama hizo. Nimekwishakutana na wasafirishaji wa abiria, na nimepanga pia kukutana na wasafirishaji wa mizigo ili kuangalia maeneo tunayoweza kuyarekebisha na kupunguza gharama za usafirishaji,” amesema.

Katika hatua nyingine, akijibu swali kuhusu upatikanaji wa mbolea, Waziri Mkuu amesema Serikali imechukua hatua za muda wa kati kwa kukaa na waagizaji wa mbolea na kuwaelekeza waangalie uwezekano wa kuagiza bidhaa hiyo kutoka nchi mbadala badala ya kutegemea nchi za Ulaya Mashariki.

“Tumefanya hivyo pia kwa bidhaa nyingine, ikiwemo sukari. Kwa upande wa mbolea, tumeagiza kutoka nchi za Afrika, ikiwemo Morocco, na pia kuwaelekeza waagizaji waangalie masoko ya China ili kuhakikisha bidhaa hizo zinakuwepo nchini,” amesema.

Alikuwa akijibu swali la Mbunge Momba, Bi. Condester Sichalwe aliyetaka kujua Serikali imejipangaje kuhakikisha mbolea za ruzuku na pembejeo nyingine zinazolenga kumfanya mkulima kuwa mwekezaji na kilimo kuwa biashara zinafika kwa wakati na kuleta tija.

Dkt. Mwigulu amesema ili kupunguza utegemezi wa bidhaa kutoka nje na kuepuka matatizo ya usafirishaji, kwa muda mrefu, Serikali imeendelea kuhamasisha uwekezaji katika viwanda vya kuzalisha mbolea hapa nchini.

“Kiwanda kilichopo Dodoma kimeanza kufanya kazi. Pia tunaendelea kuhamasisha wakulima kutumia mbolea zinazozalishwa nchini, ikiwemo mbolea ya Mijingu kutoka Arusha, ambayo inatumika kwa kiwango kikubwa katika nchi jirani kuliko hapa Tanzania. Tunaendelea pia kuhamasisha viwanda vingine, hasa vile vinavyozalisha aina muhimu za mbolea ambazo tumekuwa tukiziagiza kutoka nje.”

Amesema Serikali imeendelea kuwalipa waagizaji wa mbolea ili kuhakikisha wanakuwa na ukwasi wa kutosha wa kuagiza mbolea na pembejeo nyingine kwa wakati. Wakati huohuo, tunazihimiza taasisi zinazosimamia usambazaji wa mbolea na sekta hiyo kufanya kazi kwa wakati. “Misimu ya kilimo siyo ya dharura, inajulikana mkoa gani unaanza msimu wa kilimo lini. Kwa hiyo, tunapaswa kupanga mapema ili mbolea na pembejeo ziwepo kabla ya msimu kuanza,” amesisitiza.








Vodacom Tanzania Plc leo imezindua ripoti ya Mazingira, Jamii na Utawala (ESG) kwa mwaka uliomalizika Machi 31, 2026, ikionesha kupungua kwa asilimia 24 ya hewa chafu, sambamba na mpango mkubwa zaidi wa uboreshaji wa mtandao katika historia ya kampuni.

Kampuni pia imewekeza shilingi 3.5 bilioni katika ufanisi wa nishati kwa mwaka huu, na kufikisha uokoaji wa megawati 18,340, ikiwa zaidi ya mara sita ya megawati 2,861 zilizookolewa kwa mwaka wa 2025.

Uzalishaji wa hewa chafu ulishuka hadi tani 18,445.5, kutoka tani 24,285.6. Pia, matumizi ya mafuta dizeli yalipungua kwa asilimia 24, kutoka lita milioni 8.6 hadi lita milioni 6.6.

Upunguaji huo ulitokana na kubadilisha vifaa vya zamani vya mawasiliano ya redio katika maeneo 1,808 ndani ya miezi saba, pamoja na uimarishaji wa upatikanaji wa umeme wa gridi uliopunguza muda wa uendeshaji wa jenereta katika vituo vya data vya kampuni.

Mtandao wa Vodacom Tanzania unatumia takriban jigawati (GWh) 169.5 kwa mwaka katika zaidi ya maeneo 3,800, ambapo 2,190 kati yake yapo vijijini. Vituo vya msingi vinachukua asilimia 78.9 ya matumizi yote.

Mwaka huu, maeneo 169 yaliyokuwa nje ya gridi ya taifa yaliunganishwa kwenye gridi ya taifa. Katika kituo cha data cha Kwale, umeme wa gridi ya Taifa uliongezeka kutoka 11kVA hadi 33kVA na kupunguza matumizi ya jenereta kutoka saa 18 kwa siku hadi saa mbili, sawa na upunguzaji wa asilimia 88 wa matumizi ya dizeli katika kituo hicho.

Asilimia 57 ya nishati yote iliyotumiwa na Vodacom Tanzania ilitokana na vyanzo vya nishati jadidifu. Kampuni iliendelea kuhakikisha kuwa umeme wote wa gridi iliyonunua unaendana na nishati inayotokana na vyanzo jadidifu, hatua iliyosaidia kufikia uzalishaji sifuri wa hewa chafuzi. Aidha, Vodacom Tanzania ilihuisha tena cheti chake cha ISO 50001. Uzalishaji wa hewa chafuzi unaotokana na shughuli zake za biashara na mnyororo wake wa thamani pia ulipungua hadi tani 94,944 kutoka tani 100,455.

"Mafanikio haya ya kimazingira yametokana na kufanya uhandisi wa msingi kwa usahihi, siyo kutoka mradi tofauti wa uendelevu," alisema Mkurugenzi wa Miundombinu ya Mtandao Andrew Lupembe huku akiongeza, "kubadilisha vifaa vya zamani katika maeneo 1,808 kunampa mteja muunganisho wa haraka zaidi huku taifa likifaidika na upunguzaji wa athari za mazingira ambazo zingesababishwa na lita milioni mbili zilizopunguzwa kwenye matumizi.”

Wigo wa mtandao wa 4G ulifikia asilimia 76.3 ya wakazi, huku wateja milioni 27.7 wakiwa kwenye mtandao baada ya uzinduzi wa huduma ya kwanza ya 5G nchini Tanzania. Umiliki wa simujanja ulifikia asilimia 46.7, huku wateja 325,415 wakipata vifaa kupitia ubia wa mikopo ya rejareja.

Kwa wateja wasio na simujanja, huduma mpya ya kidijitali inayotumia akili unde inawezesha upatikanaji wa intaneti kupitia jumbefupi (SMS) na simu za sauti, ikisambaza msaada wa kidijitali hadi maeneo ya vijijini.

M-Pesa ilihudumia wateja milioni 14.1 wa ujumuishwaji wa kifedha huku M-Koba, jukwaa la kidijitali la vikundi vya akiba ambao wanachama wake wengi ni wanawake, lilifikia vikundi hai 299,420 huku akiba jumla ikiongezeka kwa asilimia 81.

Vodacom Tanzania Foundation ilifikia wanufaika milioni 2.9, kwa kushirikiana na Taasisi ya Elimu Tanzania, kampuni iliondoa gharama ya data kwenye jukwaa la kitaifa la maendeleo ya walimu, na kuwapa walimu 121,832 fursa ya kupata nyenzo za maendeleo ya kitaaluma bila gharama ya data. Miti 80,000 ya asili iliongezwa katika Msitu wa Kahe 2 katika Mlima Kilimanjaro.

Kampuni ilirekodi mwaka wa kumi na nne mfululizo bila kutokea kifo cha mfanyakazi mahali pa kazi. Mpango wa uboreshaji ulihusisha wafanyakazi 411 waliosafiri zaidi ya kilomita milioni 1.7, na awamu ya kwanza ilikamilika bila kutokea kifo au tukio kubwa. Vodacom Tanzania ina uthibitisho wa ISO 27001 kwa usalama wa data na haikurekodi faini yoyote ya ushindani usio halali au utakatishaji fedha.

"Nyuma ya kila muunganisho kuna maisha yanayobadilika, mwalimu anayefikia nyenzo za kujifunzia bila gharama ya data, kikundi cha akiba ambacho hakihifadhi tena fedha taslimu katika bati. Tutaendelea kuwajibika kwa wananchi wa Tanzania wanaotuamini kila siku,” aliongeza Philip Besiimire, Afisa Mtendaji mkuu wa kampuni hiyo.

Kwa taarifa zaidi bofya: https://vodacom.com/pdf/our-purpose/reporting-centre/20261/vodacom-tanzania-esg-snapshot-2026.pdf

Mkurugenzi wa Kitengo cha Mtandao wa Vodacom Tanzania Plc Andrew Lupembe (kushoto) na Mkurugenzi wa Uhusiano na Mawasiliano wa kampuni hiyo Zuweina Farah wakizungumza wakati wa uzinduzi wa Ripoti ya Mazingira, Jamii na Utawala (ESG) ya kampuni hiyo kwa mwaka wa fedha ulioishia Machi 2026, ambayo imeonesha kupungua kwa uzalishaji hewa chafu (carbon emissions) kwa asilimia 24 na uwekezaji mkubwa katika uboreshaji wa mtandao. Tukio hilo lilifanyika jijini Dar es Salaam tarehe 3 Septemba, 2026.
Mkurugenzi wa Miundombinu wa Vodacom Tanzania Plc Andrew Lupembe akizungumza na waandishi wa Habari wakati wa uzinduzi wa ripoti  ya ESG ya mwaka 2026.
Mmoja wa wasikilizaji wakati wa uzinduzi wa ripoti ya ESG akiuliza swali ili apate ufafanuzi zaidi ya namna gani matokeo ya ripoti hiyo yatakavyozidi kuwanufaisha wananchi wa Kawaida.
Baadhi ya wananchi waliohudhuria uzinduzi wa ripoti hiyo wakisikiliza ufafanuzi wa namna kampuni hiyo inavyochukulia  ESG kwa uzito unaotakiwa, wakati Vodacom ilipozindua ripoti ya ESG ya mwaka ulioishia Machi 31, 2026
Serikali imeendelea kuchukua hatua za kuimarisha sekta ya elimu kwa kuongeza miaka ya elimu ya lazima, kupanua fursa za elimu ya sekondari na kuimarisha mafunzo ya ufundi ili kuwapa vijana uwezo wa kushiriki kikamilifu katika soko la ajira.

Akizungumza Septemba 02, 2026 jijini Dodoma na Balozi wa Uingereza nchini Tanzania, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, amesema maandalizi ya utekelezaji wa miaka 10 ya elimu ya lazima kuanzia mwaka 2028 yanaendelea, hatua itakayohitaji miundombinu, walimu na nafasi za kutosha katika shule za sekondari.

Prof. Mkenda amebainisha kuwa mpango huo utasababisha ongezeko kubwa la wanafunzi watakaoingia sekondari, hivyo Serikali imeweka mkakati wa kuhakikisha wanafunzi wote wanaostahili wanapata nafasi ya kuendelea na masomo.

Aidha, ameongeza kuwa Serikali inaendelea kuimarisha mfumo wa elimu wenye mikondo ya elimu ya jumla na elimu ya amali, ili wanafunzi wapate maarifa na stadi zinazowawezesha kuajirika au kujiajiri.

Katika mazungumzo hayo, Prof. Mkenda ameeleza kuwa Serikali inajenga vyuo vya ufundi katika maeneo mbalimbali na kuimarisha mafunzo ya ufundi ili kukidhi mahitaji ya vijana na uchumi wa Taifa.

Prof. Mkenda ameongeza kuwa Serikali inawekeza katika masomo ya sayansi, teknolojia, uhandisi na hisabati pamoja na teknolojia mpya kama akili bandia (AI), ujifunzaji wa mashine na usalama wa mtandao, ili kuandaa wataalamu wa kisasa.

Amesisitiza umuhimu wa ushiriki wa sekta binafsi katika kupanua fursa za elimu, hususan katika ujenzi wa miundombinu na utoaji wa elimu ya amali.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Prof. Carolyne Nombo, amesema kuwa Serikali inatazama uwezekano wa kuboresha vivutio vya kisera vitakavyoongeza uwekezaji wa sekta binafsi katika elimu.

Naye Balozi wa Uingereza nchini Tanzania, Mhe. Marianne Young, amepongeza juhudi za Tanzania na kuahidi kuendeleza ushirikiano katika elimu na na mafunzo ya ufundi, ikiwemo kuunganisha taasisi za Tanzania na vyuo vikuu vya Uingereza katika maeneo ya teknolojia ya kisasa na mazingira.




Timu ya Ujenzi Sports Club imeendelea kuunga mkono juhudi za kuwawezesha wanafunzi wenye mahitaji maalum kwa kutoa msaada wa vifaa mbalimbali kwa wanafunzi wa Shule ya Msingi Mlezi jijini Dodoma.

Msaada huo umetolewa Jumatano, Septemba 2, 2026, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Ujenzi Sports Club kuunga mkono kazi inayofanywa na shule hiyo katika kuwawezesha wanafunzi wenye mahitaji maalum pamoja na wanafunzi wengine kupata mazingira bora ya kujifunzia.

Vifaa vilivyotolewa ni pamoja na madaftari, vyombo vya kulia chakula, vifaa vya usafi, sabuni, ndoo pamoja na fedha kwa ajili ya ununuzi wa mipira ya michezo.

Akikabidhi msaada huo, Mwenyekiti wa Ujenzi Sports Club, Arch. Ibrahim Chatila, amesema klabu hiyo inatambua na kuthamini kazi kubwa inayofanywa na walimu katika kuwawezesha wanafunzi wenye mahitaji maalum kutimiza ndoto zao kielimu na katika maisha kwa ujumla.

Amesema msaada huo ni sehemu ya jitihada za Ujenzi Sports Club kuunga mkono juhudi zinazofanywa na shule hiyo, huku akiahidi kuwa klabu itaendelea kushirikiana na kuwahamasisha wadau wengine, hususan katika sekta ya ujenzi, kujitokeza na kusaidia juhudi hizo.

“Tunatambua kazi kubwa inayofanywa na walimu katika kuwalea na kuwawezesha watoto hawa. Msaada huu ni sehemu ya mchango wetu katika kuunga mkono juhudi hizo, na tutaendelea kuwahamasisha wadau wengine kujitokeza na kusaidia,” amesema Arch. Chatila.

Akizungumza baada ya kupokea msaada huo, Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Mlezi, Bi. Magreth Kisanga, ameishukuru Ujenzi Sports Club kwa ukarimu na moyo wa kujitolea uliouonyesha kwa kuwasaidia wanafunzi hao.

Amesema msaada huo utasaidia kupunguza changamoto ya upungufu wa baadhi ya vitendea kazi vinavyohitajika katika kuwawezesha wanafunzi kupata mazingira bora ya kujifunzia na kuishi shuleni.

Kwa upande wake, mwalimu anayesimamia kitengo cha wanafunzi wenye mahitaji maalum, Mwl. Hashim Msemo, amesema wanafunzi hao wamekuwa wakifanya vizuri katika masomo yao na wameendelea kufanya vyema katika mitihani yao.

Ametoa wito kwa wadau mbalimbali kujitokeza na kuunga mkono juhudi za shule hiyo ili kuongeza fursa na mazingira bora kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum.

Shule ya Msingi Mlezi ni shule jumuishi inayotoa elimu kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum pamoja na wanafunzi wengine, kwa lengo la kuhakikisha kila mtoto anapata fursa sawa ya elimu na maendeleo
Serikali imepongeza jitihada za muwekezaji Kampuni ya Uhandisi na Uzalishaji wa vifaa vya uchimbaji madini ya Mining Engineering Services Tanzania Limited (MES), kwa uwekezaji wake wa TZS bilioni 35 katika ujenzi wa kiwanda kipya cha uzalishaji wa vifaa mbalimbali vya uchimbaji madini hatua inayotajwa kuwa itasaidia kupunguza kwa kiasi kikubwa utegemezi wa bidhaa za matumizi ya uchimbaji madini chini ya ardhi zinazoagizwa kutoka nje.

Kampuni hiyo ambayo ni mwanachama wa Kundi la Makampuni la VINMART inajenga kiwanda hicho Kigamboni, Dar es Salaam, na kitazalisha bidhaa ambazo hadi sasa zimekuwa zikipatikana kwa kiasi kikubwa kutoka kwa wasambazaji wa nje ya nchi. Uwekezaji huo unahusisha kiwanda, mitambo na miundombinu saidizi inayohitajika kuwezesha uzalishaji wa bidhaa hizo nchini.

Uwekezaji huo ulielezwa wakati wa ziara ya Kamishna wa Tume ya Madini ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini (Local Content), Dkt. Theresia Charles Numbi, aliyetembelea kiwanda hicho kutathmini maendeleo yake na mipango ya uzalishaji.

Dkt. Numbi alifanya ziara katika kiwanda hicho kipya kinachojengwa kutoka hatua za awali, kwa lengo la kutathmini maendeleo ya mradi huo pamoja na mipango ya shughuli za uzalishaji. Alisema Serikali itaendelea kuunga mkono uwekezaji unaochangia ukuaji wa sekta ya madini, kuimarisha uzalishaji wa viwandani nchini na kuchochea maendeleo ya kiuchumi ya Tanzania.

Pamoja na kupongeza uwekezaji huo, Dkt Numbi alitoa wito kwa kampuni hiyo kuhakikisha kuwa mradi huo pamoja na bidhaa zitakazozalishwa vinabuniwa kwa namna itakayowawezesha wachimbaji wadogo na wa kati katika maeneo mbalimbali nchini kunufaika na uwekezaji huo.

“Serikali itaendelea kuunga mkono uwekezaji kama huu wa MES unaolenga kuwezesha ukuaji wa sekta ya madini na kuchangia maendeleo ya kiuchumi ya nchi,” alisema Dkt. Numbi.

Kiwanda cha MES kinatarajiwa kupunguza kwa kiasi kikubwa utegemezi wa Tanzania kwa bidhaa za matumizi ya mara kwa mara katika shughuli za uchimbaji madini chini ya ardhi, ambazo kwa kiasi kikubwa zimekuwa zikiagizwa kutoka kwa wasambazaji wa nje ya nchi.

Uwekezaji huo wa TZS bilioni 35 unahusisha ujenzi wa kiwanda, mitambo pamoja na miundombinu saidizi inayohitajika kuwezesha uzalishaji wa bidhaa hizo nchini.

Kwa mujibu wa uongozi wa MES, uwekezaji huo unalenga kuchukua nafasi ya bidhaa za matumizi ya mara kwa mara katika uchimbaji wa madini chini ya ardhi, ambazo kwa sasa huagizwa kutoka nje, kwa kuzalisha bidhaa hizo hapa nchini.

Mkurugenzi Mtendaji wa MES, Bw Pulin Manek, alisema kampuni hiyo imewekeza katika uwezo mkubwa wa uzalishaji utakaokidhi mahitaji ya soko la ndani, huku ukiweka mazingira ya Tanzania kuhudumia masoko mengine ya madini katika ukanda huu.

“Sababu ya kuanzisha kiwanda hiki ni kuisaidia Tanzania kupunguza utegemezi wa bidhaa za matumizi ya mara kwa mara katika uchimbaji wa madini chini ya ardhi zinazoagizwa kutoka nje, ambazo zinaendelea kuigharimu nchi kiasi kikubwa cha fedha,” alisema Manek.

“Tumewekeza katika uwezo wa kutosha wa uzalishaji ili kukidhi mahitaji ya soko la ndani, huku tukiiweka Tanzania katika nafasi ya kuhudumia masoko mengine ya madini katika ukanda huu.” Aliongeza.

Kiwanda hicho kitakapoanza kufanya kazi kwa ukamilifu, kitakuwa na uwezo wa kuzalisha bidhaa za ‘split sets’ kwa kiwango kinachokadiriwa kuwa mara mbili na nusu ya mahitaji ya sasa ya Tanzania kwa mwezi.

“Uwezo huu unatosha kuchukua nafasi ya uagizaji wa ‘split sets’ kutoka nje, huku ukiwezesha Tanzania kuuza ziada ya bidhaa hizo katika masoko ya kikanda,” alisema Manek.

Uwezo wa kiwanda hicho wa kuzalisha ‘mine mesh’ utakuwa mkubwa zaidi, ambapo kimebuniwa kuzalisha kiasi kinachokadiriwa kuwa mara nane ya mahitaji ya sasa ya Tanzania kwa mwezi.

Manek alisema uwezo huo wa ziada umeandaliwa kwa makusudi ili kuhudumia migodi mipya ya chini ya ardhi, kusaidia migodi inayobadilisha mfumo wa uchimbaji kutoka wazi kwenda chini ya ardhi, pamoja na kukidhi mahitaji ya masoko ya nchi jirani.

“Tunazalisha zaidi ya mahitaji ya sasa ya nchi kwa sababu tunaangalia mahitaji ya baadaye ya Tanzania katika uchimbaji wa madini chini ya ardhi, pamoja na fursa zilizopo katika ukanda mpana zaidi,” alisema Manek. “Tunaamini kuwa nchi haipaswi kuendelea kuagiza bidhaa za matumizi ya mara kwa mara ambazo zinaweza kuzalishwa hapa nchini.”

Kiwanda hicho kitakuwa na njia kuu tatu za uzalishaji, ambazo ni mine mesh, friction-stabiliser split sets na dome plates. Uwekezaji wa kampuni hiyo unalenga kuhudumia sekta za nishati, usafirishaji na madini.

Kwa mujibu wa Bw Manek, MES pia ni kampuni ya kwanza nchini Tanzania kuwekeza katika mtambo wa hot-dip galvanising bath, uwekezaji unaotarajiwa kuongeza zaidi uwezo wa nchi wa kuzalisha bidhaa zinazohusiana na shughuli za madini hapa nchini.

“Mbali na kupunguza utegemezi wa bidhaa zinazoagizwa kutoka nje, mradi huu unatarajiwa kuunda fursa za ajira kwa Watanzania, hususan katika uzalishaji, uchomeleaji, galvanising na uhandisi, huku ukisaidia kuimarisha ujuzi wa kitaalamu ndani ya mnyororo wa ugavi wa sekta ya madini nchini,” aliongeza Manek.

Kampuni hiyo pia inalenga masoko ya kikanda, yakiwemo Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Zambia na Zimbabwe, ikiwa na mipango ya kutumia nafasi ya kimkakati ya Tanzania pamoja na fursa ya usafirishaji kupitia Bandari ya Dar es Salaam ili kuifanya nchi kuwa kitovu cha uzalishaji na usambazaji wa bidhaa katika ukanda huu.

Aidha, uwezo wa uzalishaji wa kiwanda hicho unatarajiwa kuiwezesha Tanzania kuhudumia soko la ndani na kuuza bidhaa zitakazozalishwa kwa ziada katika masoko ya madini ya kikanda.

Uzalishaji wa ndani unatarajiwa pia kupunguza kwa kiasi kikubwa muda wa kuwasilisha bidhaa kwa wateja. Bidhaa za matumizi ya mara kwa mara katika shughuli za uchimbaji madini zinazoagizwa kutoka nje zinaweza kuchukua kati ya wiki nane hadi 16 kufika nchini, huku MES ikitarajia bidhaa zinazozalishwa ndani ya nchi kufikishwa kwa wateja ndani ya siku chache.

Uwekezaji huo unatajwa kuendana na Sheria ya Madini ya Tanzania pamoja na Kanuni za Maudhui ya Ndani, zinazotoa kipaumbele kwa bidhaa zinazozalishwa nchini na huduma zinazotolewa na raia wa Tanzania pamoja na kampuni zilizosajiliwa nchini.

Ujenzi wa kiwanda cha MES unafanyika wakati Serikali ikiendelea na juhudi za kuongeza ushiriki wa wazawa katika mnyororo wa thamani wa madini, kuongeza uzalishaji wa viwandani nchini na kuhakikisha kuwa uwekezaji katika sekta hiyo unazalisha manufaa mapana zaidi ya kiuchumi kwa Watanzania.


Kamishna wa Tume ya Madini ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini (Local Content), Dkt. Theresia Charles Numbi (katikati-kushoto), akizungumza na Wakurugenzi wa Kampuni ya Mining Engineering Services Tanzania Limited (MES), kampuni mwanachama wa Kundi la Makampuni la VINMART, wakati wa ziara yake katika kiwanda cha kampuni hiyo jijini Dar es Salaam jana.

Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Mining Engineering Services Tanzania Limited (MES), Pulin Manek (katikati), akizungumza na waandishi wa habari wakati wa ziara ya Kamishna wa Tume ya Madini ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini (Local Content), Dkt. Theresia Charles Numbi katika kampuni hiyo jijini Dar es Salaam jana.


Ifakara, Morogoro. Kampuni ya mawasiliano ya Yas Tanzania imekabidhi vifaa tiba na vifaa vya kujifungulia katika Kituo cha Afya Kibaoni, Ifakara, ikiwa ni mwendelezo wa Kampeni ya Tumaini inayolenga kuunga mkono huduma za afya kwa mama mjamzito.

Kituo hicho kinakuwa cha pili kunufaika na kampeni hiyo iliyoanzishwa jijini Dar es Salaam wiki iliyopita kupitia mchango wa wafanyakazi wa Yas.

Vifaa vilivyokabidhiwa ni pamoja na vitanda vya kujifungulia, viti mwendo, mashuka, khanga, aproni pamoja na vifaa muhimu vinavyotumika wakati wa kujifungua (maternity kits).

Akizungumza baada ya kupokea msaada huo, Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Wakili Dustan Kyobya, amepongeza ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi katika kuboresha huduma za afya, akisema mchango wa wadau una nafasi muhimu katika kukabiliana na changamoto zinazowakabili wananchi, hususan katika huduma za mama na mtoto.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Yas Kanda ya Kusini, Joseph Mutalemwa, amesema Kampeni ya Tumaini ilitokana na uamuzi wa wafanyakazi wa kampuni hiyo kuunganisha nguvu na kutoa mchango unaogusa moja kwa moja mahitaji ya jamii.

“Tunatambua kuwa ujio wa mtoto duniani ni wakati wa furaha na matumaini kwa kila familia, lakini pia ni kipindi ambacho mama anahitaji huduma bora, uangalizi wa karibu na mazingira salama ya kujifungua. Msaada huu ni sehemu ya kuunga mkono huduma za uzazi zinazotolewa hapa Kibaoni,” amesema Mutalemwa.

Amesema pamoja na jukumu la Yas la kuwaunganisha Watanzania kupitia huduma za mawasiliano, kampuni hiyo inaona umuhimu wa kushiriki katika juhudi zinazolenga kuboresha ustawi wa jamii.

“Kama tunavyojivunia kuwa Mtandao wa Viwango, tunaamini viwango havipaswi kuishia kwenye huduma za mawasiliano pekee, bali vinapaswa kuonekana pia katika namna tunavyowajibika kwa jamii tunayoihudumia,” amesema.

Mutalemwa amesema Kampeni ya Tumaini ni endelevu na inatarajiwa kufika katika wilaya na mikoa mingine nchini baada ya kuanzia Dar es Salaam na sasa Ifakara.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Ifakara, Pili Kitwana, amesema msaada huo utasaidia kupunguza upungufu wa baadhi ya vifaa muhimu vinavyotumika kutoa huduma za uzazi katika kituo hicho.

Amesema Kituo cha Afya Kibaoni kinahudumia idadi kubwa ya wananchi, hali inayoongeza mahitaji ya vifaa na miundombinu ya kutolea huduma, hivyo vifaa vilivyotolewa vinatarajiwa kuongeza uwezo wa wahudumu wa afya kuwahudumia wajawazito na kina mama wanaofika kujifungua.

Baadhi ya wananchi waliohudhuria makabidhiano hayo, akiwemo Diwani wa Kata ya Kibaoni, Rashidi Namtuka, wameeleza kuwa msaada huo utasaidia kuboresha mazingira ya utoaji huduma kwa wajawazito na kina mama wanaojifungua katika kituo hicho.
Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Mhe. Dustan Kyobya (katikati), akiwaongoza wafanyakazi wa Yas Tanzania kukabidhi vifaa tiba na vifaa vya kujifungulia katika Kituo cha Afya Kibaoni, Ifakara mkoani Morogoro, hivi karibuni. Msaada huo ni sehemu ya Kampeni ya Tumaini inayoendeshwa na wafanyakazi wa Yas, yenye lengo la kuunga mkono huduma za afya ya mama kwa kutoa vifaa muhimu katika vituo vya afya nchini.

Mamia ya wananchi wamejitokeza kupata huduma katika Kambi Maalum ya Matibabu ya Macho inayoendeshwa na madaktari bingwa kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH)kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Qatar Charity ampo leo Septemba 01, 2026 huduma hizo zimeanza kutolewa rasmi katika Kituo cha Afya Sebuleni, Mkoa wa Mjini Magharibi.

Akizindua huduma hizo, Mkuu wa Wilaya ya Mjini Mh.  Hassan Khamis Hafidh, amepongeza ushirikiano kati ya Muhimbili, Qatar Charity na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, akisema umewezesha wananchi kusogezewa huduma za kibingwa za macho na kuongeza fursa ya kupata matibabu ya kisasa karibu na maeneo yao.

"Ushirikiano kati ya Hospitali ya Taifa Muhimbili, Qatar Charity na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar umeleta huduma za kibingwa karibu na wananchi wetu. Hii ni hatua muhimu ya kuboresha upatikanaji wa huduma za afya na kuwafikia wananchi wanaohitaji matibabu ya macho kwa wakati, nawaombeni wananchi wote wa Zanzibar tuitumie fursa hii” amesema Mhe. Hafidh.

Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Magonjwa ya Macho kutoka Muhimbili, Dkt. Joachim Kilemile, amesema hospitali imejipanga kuhakikisha kila mwananchi anayefika kambini anapata huduma, na kuwataka wananchi kutokata tamaa licha ya idadi kubwa ya watu waliojitokeza kwani wote watahudumiwa.

“Tunawaomba wananchi wasikate tamaa kutokana na idadi kubwa ya waliojitokeza. Muhimbili imejipanga kwa wataalamu na vifaa vya kutosha kuhakikisha kila mgonjwa anayefika kambini anapata huduma stahiki, ikiwemo upasuaji wa mtoto wa jicho kwa njia ya tundu dogo.” ameeleza Dkt. Kilemile.

Kambi hiyo imeanza Agosti 29 na itahitimishwa Septemba 4, 2026, ikitoa huduma za uchunguzi wa macho, dawa, miwani kwa wenye uhitaji pamoja na upasuaji wa mtoto wa jicho kwa njia ya tundu dogo, upasuaji unaofanyika kwa kutumia gari maalum la upasuaji, ikiwa ni mara ya kwanza nchini Tanzania kutekelezwa kwa mfumo huo wa kisasa.

Kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi 2022, kiwango cha ulemavu kwa watu wenye umri wa miaka 7 na kuendelea Zanzibar kimeongezeka kutoka 7.5% mwaka 2012 hadi 11.4% mwaka 2022, sawa na ongezeko la asilimia 3.9 ambapo katika makundi hayo, ulemavu wa kuona ni miongoni mwa aina zilizoongoza, ikiashiria ongezeko la mahitaji ya huduma za afya ya macho Zanzibar.MAMIA WAFURIKA KATIKA KAMBI YA MATIBABU YA MACHO INAYOENDESHWA NA MUHIMBILI ZANZIBAR

Mamia ya wananchi wamejitokeza kupata huduma katika Kambi Maalum ya Matibabu ya Macho inayoendeshwa na madaktari bingwa kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH)kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Qatar Charity ampo leo Septemba 01, 2026 huduma hizo zimeanza kutolewa rasmi katika Kituo cha Afya Sebuleni, Mkoa wa Mjini Magharibi.

Akizindua huduma hizo, Mkuu wa Wilaya ya Mjini Mh.  Hassan Khamis Hafidh, amepongeza ushirikiano kati ya Muhimbili, Qatar Charity na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, akisema umewezesha wananchi kusogezewa huduma za kibingwa za macho na kuongeza fursa ya kupata matibabu ya kisasa karibu na maeneo yao.

"Ushirikiano kati ya Hospitali ya Taifa Muhimbili, Qatar Charity na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar umeleta huduma za kibingwa karibu na wananchi wetu. Hii ni hatua muhimu ya kuboresha upatikanaji wa huduma za afya na kuwafikia wananchi wanaohitaji matibabu ya macho kwa wakati, nawaombeni wananchi wote wa Zanzibar tuitumie fursa hii” amesema Mhe. Hafidh.

Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Magonjwa ya Macho kutoka Muhimbili, Dkt. Joachim Kilemile, amesema hospitali imejipanga kuhakikisha kila mwananchi anayefika kambini anapata huduma, na kuwataka wananchi kutokata tamaa licha ya idadi kubwa ya watu waliojitokeza kwani wote watahudumiwa.

“Tunawaomba wananchi wasikate tamaa kutokana na idadi kubwa ya waliojitokeza. Muhimbili imejipanga kwa wataalamu na vifaa vya kutosha kuhakikisha kila mgonjwa anayefika kambini anapata huduma stahiki, ikiwemo upasuaji wa mtoto wa jicho kwa njia ya tundu dogo.” ameeleza Dkt. Kilemile.

Kambi hiyo imeanza Agosti 29 na itahitimishwa Septemba 4, 2026, ikitoa huduma za uchunguzi wa macho, dawa, miwani kwa wenye uhitaji pamoja na upasuaji wa mtoto wa jicho kwa njia ya tundu dogo, upasuaji unaofanyika kwa kutumia gari maalum la upasuaji, ikiwa ni mara ya kwanza nchini Tanzania kutekelezwa kwa mfumo huo wa kisasa.

Kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi 2022, kiwango cha ulemavu kwa watu wenye umri wa miaka 7 na kuendelea Zanzibar kimeongezeka kutoka 7.5% mwaka 2012 hadi 11.4% mwaka 2022, sawa na ongezeko la asilimia 3.9 ambapo katika makundi hayo, ulemavu wa kuona ni miongoni mwa aina zilizoongoza, ikiashiria ongezeko la mahitaji ya huduma za afya ya macho Zanzibar.




 

NNa Mwandishi Wetu - Dodoma


SERIKALI imetoa maelekezo 13 kwa umma, kamati za usimamizi wa maafa, Wizara, Taasisi, Mikoa, Halmashauri na sekta mbalimbali nchini, kwa ajili ya kujiandaa na kukabiliana na madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na mvua za El-Nino.

Imeelekeza maeneo yote hatarishi yatambuliwe mapema, tathmini za vihatarishi zifanyike na hatua stahiki zichukuliwe, ikiwemo kuwahamasisha wananchi kuondoka katika maeneo hatarishi na kwenda maeneo salama.

Maelekezo hayo yametolewa hii leo (02 Septemba,2026) na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Profesa Palamagamba Kabudi, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Dharura wa Kukabiliana na Madhara ya El-Nino.

Profesa Kabudi amesema Serikali imeelekeza kuhakikisha mvua hizo zinatumika kikamilifu kwa shughuli za uzalishaji, ikiwemo kilimo, ufugaji, uvunaji wa maji na uvuvi.

Aidha, amesisitiza wananchi wanapaswa kuelimishwa na kuhimizwa kuchukua hatua za kupunguza madhara yanayoweza kusababishwa na mvua hizo, ikiwemo kufanya shughuli za kiuchumi na kijamii katika maeneo salama, kuweka akiba ya chakula, kutumia mbinu bora za kilimo na kuchagua mazao pamoja na mbegu bora kwa msimu wa Vuli.

“Kuandaa rasilimali kwa ajili ya kuzuia au kupunguza madhara, kujiandaa na kukabiliana na maafa yatakayotokea na kushirikisha wadau wote wa maafa, wakiwemo wananchi, taasisi na sekta binafsi katika maeneo yao,” amesema.

Ameongeza kuwa: “Serikali imeagiza kuandaliwa na kutekelezwa kwa mipango ya kuzuia milipuko ya magonjwa kwa binadamu, wanyama na mimea.”

Profesa Kabudi amesema Wizara, Taasisi, Mikoa na wadau wengine wanaohusika na miundombinu wanapaswa kufanya ukaguzi wa miundombinu muhimu na kuhakikisha inaimarishwa na kusafishwa, ikiwemo madaraja, makaravati na mitaro.

Amesema hatua hiyo itasaidia kuhakikisha upatikanaji wa huduma muhimu kabla, wakati na baada ya maafa kutokea, zikiwemo huduma za usafirishaji, maji na umeme.

Serikali pia imeagiza kuimarishwa kwa usimamizi wa mazingira, ikiwemo udhibiti wa taka ngumu, usafishaji na uimarishaji wa njia za maji, kingo za mito na mabwawa.

Aidha, imeelekeza kuhakikisha vifaa vya uokoaji, huduma za dharura na mifumo ya mawasiliano vinapatikana na kuwa katika hali ya utayari wakati wote.

Katika hatua nyingine, Serikali imeagiza kubainisha na kutenga maeneo salama yatakayotumika kwa ajili ya makazi ya dharura pindi maafa yatakapotokea.

Kwa upande wa sekta ya utalii, Serikali imeagiza kufanyika kwa ukaguzi na ukarabati wa miundombinu iliyopo katika maeneo ya Hifadhi za Taifa na Hifadhi za Jamii ili kuhakikisha shughuli za utalii zinaendelea wakati wote.

“Wizara, Taasisi, Mikoa na Halmashauri zote zimeagizwa kufuatilia na kuzingatia maelekezo ya kitaalamu pamoja na taarifa za utabiri wa hali ya hewa zinazotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), ili hatua stahiki za kujiandaa na kukabiliana na madhara ya El-Nino zichukuliwe kwa wakati.”


KUHUSU BILIONI 730


Akizungumzia taarifa iliyosambaa katika mitandao ya kijamii kuhusu makadirio ya matumizi ya Sh. bilioni 730 katika kujiandaa na kukabiliana na El-Niño, Profesa Kabudi amesema taarifa hiyo haikutoa ufafanuzi wa kina kuhusu shughuli zilizoainishwa katika mpango huo.

Amesema Sh. bilioni 730 ni makadirio ya fedha zinazohitajika kutekeleza Mpango wa Taifa wa Dharura wa Kukabiliana na Madhara ya El-Niño kabla, wakati na baada ya El-Nino kutokea.

“Kwa mujibu wa Mpango, makadirio ya fedha zinazohitajika kutumika katika kutekeleza Mpango huo ni Sh. bilioni 730,” amesema.

Hata hivyo, amesema fedha zilizotengwa katika bajeti ya Serikali ya mwaka wa fedha 2026/2027 kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli hizo katika sekta zote ni Sh. bilioni 10.