MAPOKEZI makubwa ya wanariadha wanaokimbiza bendera ya Taifa kwenda kilele cha Mlima Kilimanjaro, yamemzindua Mkuu wa Wilaya ya Same, Ibrahim Marwa na sasa ameahidi kuelekeza nguvu zake katika kukuza mchezo huo wilayani mwake.
Marwa aliyasema hayo jana mjini hapa alipokuwa anakabidhi bendera ya Taifa kwa mwanariadha nyota Francis Naali, aliyeanzisha ngwe ya mwisho ya mbio hizo zinazodhaminiwa na Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) kupitia Bia yake ya Kilimanjaro.
Naali alikuwa anaanzisha mbio kumalizia kilomita 104 kati ya 567 walizokimbia wanariadha zaidi ya 70 tangu kuanza kwa mbio hizo Jumapili iliyopita jijini Dar es Salaam na kuendelea kwa siku nne mfululizo, zikipita katika mikoa ya Pwani, Tanga na hatimaye Kilimanjaro.
“Jamani, nimehamasika sana na ninawashukuru Bia ya Kilimanjaro kwa kuipa Same heshima ya kuwa na kituo cha mbio hizi. Binafsi nimehamasika na ninatangaza rasmi kwamba, kuanzia sasa nitaweka mkazo katika riadha wilayani kwangu.
“Ndiyo, nani asiyejua michezo inatoa ajira kubwa? Hawa wanariadha tunaowaona leo wameajiriwa au wanaendesha maisha yao kupitia riadha, nasi Same tuna vijana wengi ambao mkama wakiandaliwa vyema, watakuja kuwa nyota wa kweli wa nchi hii,” alisema Marwa ambaye mara kadhaa hotuba yake fupi ilikatishwa kwa makofi, vigelegele na mayowe kutoka kwa wakazi wa Same waliofurika Kituo Kikuu cha Mabasi mjini hapa kushuhudia wanariadha wakiianza ngwe ya mwisho ya mbio hizo.
Naye Meneja Masoko wa TBL, David Minja akiwa mwenye tabasamu, alisema: “Tunajivunia kampeni hii ya kupandisha bendera katika Mlima Kilimanjaro, na kikubwa tunashukuru kwa jinsi Watanzania walivyopokea kampeni hii ya “Fikisha Tanzania Katika Hatua za Juu”. Tunajivunia mlima mrefu kuliko yote Afrika na tunajivunia bia yetu ya Kilimanjaro…”
Kauli ya shukrani kwa wakazi wa mikoa waliyopitia wanariadha hao ilitolewa pia na Meneja wa Bia ya Kilimanjaro, George Kavishe.
Alisema; “Leo ni siku ya nne ya mbio hizi za aina yake na tunashukuru kwa mwamko ambao Watanzania wameuonyesha kote tulikopita.
Sisi wa Bia ya Kilimanjaro tuko kamili na tunajipanga kuhakikisha mbio hizi zinapata mafanikio zaidi na zaidi, lengo likiwa kwenda sambamba na umaarufu wa mlima wa Kilimanjaro.”
Mbali ya kuanzisha kwa mbio za kukimbiza bendera ya taifa kuelekea kilele cha Mlima Kilimanjaro, Bia ya Kilimanjaro imekuwa mstari wa mbele katika kudhamini michezo mingine nchini.
Bia hiyo, ndiyo inayozidhamini klabu kongwe na maarufu zaidi katika soka nchini, Simba na Yanga, pia ni mdhamini wa muda mrefu wa mbio za kimataifa za Marathoni za Kilimanjaro na zile zinazoshirikisha wanariadha kutoka zaidi ya nchi 25 duniani.
Pia ni wadhamini wa Tuzo za Muziki za Kilimanjaro. Imekuwa pia ikidhamini michuano ya mpira wa kikapu ya mkoani Dar es Salaam `RBA Kili’.
Mbio hizo zilitarajiwa kuingia Marangu jana jioni, tayari kwa kuipandisha kileleni mwa Mlima Kilimanjaro, leo.
Nawapongeza Kilimanjaro Premium Lager kwa kampeni hii.. kwa kuboresha, napendekeza pia Kili lager waangalie uwezekano wa kubadili kile kibao cha pale kileleni, Gilmans point. nilikiona ktk picha za Gerald Hando na hali ya kile kibao sio ya kuridhisha
ReplyDeleteWewe apo juu sidhani kama kile kibao kinahitaji nguvu ya kiwanda kukitengeneza. Hata wewe tu mwenyewe unaweza kujitolea na kufanya wonders.
ReplyDeleteVitu vingi Tanzania havihitaji hata hela ni kuwa tu creative na kuacha uvivu wa kusubiri kufanyiwa kama umeona kitu kinahitaji marekebisho do it....