Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, Uratibu na Bunge) Mhe. William Lukuvi (Mb), akisalimiana na Mwenyekiti Mtendaji wa Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania (TACAIDS) Bibi Fatma Mrisho wakati wa mapokezi ya Waziri huyo katika viwanja ya Ofisi ya Waziri Mkuu alipowasili kuanza kazi yake rasmi tarehe 29 Novemba 2010. Nyuma ya Waziri ni Kaimu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu Bw. Fanuel Mbonde.
Kaimu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu Bw. Fanuel Mbonde akiwatambulisha Mawaziri wa Nchi katika Ofisi ya Waziri Mkuu, Mhe. Mary Nagu (Mb) anayeshughulikia (Uwekezaji na Uwezeshaji) na Mhe. William Lukuvi (Mb) anayeshughulikia (Sera Uratibu na Bunge) kwa Wakuu wa Idara, Vitengo na Taasisi zilizoko chini ya Ofisi hiyo (hawako pichani), tarehe 29 Novemba, 2010 wakati Mawaziri hao waliporipoti Ofisi ya Waziri Mkuu kuanza kazi rasmi baada ya kuapishwa.


Mawaziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Mhe. Mary Nagu (Mb) anayeshughulikia (Uwekezaji na Uwezeshaji) na Mhe. William Lukuvi (Mb) anayeshughulikia (Sera, Uratibu na Bunge) baada ya kuapishwa rasmi na Rais wa Jamhuri ya Muungao wa Tanzania Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete, tarehe 29 Novemba, 2010 waliripotii rasmi katika Ofisi ya Waziri Mkuu na kuzungumza na Wakuu wa Idara, Vitengo na Taasisi chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu.

Wakizungumza na Viongozi wa Idara, Vitengo na Taasisi zilizoko chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Mawaziri hao waliwataka watendaji hao kufanya kazi kwa ubunifu, ushirikiano, upendo, uwazi na bidii zaidi ili kukidhi matarajio ya wananchi.

“Kinachotakiwa ni ushirikiano, upendo na uwazi baina ya watendaji na wafanyakazi wote ili kufikia malengo ya Ofisi” alisisitiza Mhe. Mary Nagu.

Mhe. Nagu alisisitiza umuhimu wa Ofisi ya Waziri Mkuu kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji pasipokuwa na ngoja ngoja ambayo ni chanzo cha kuwakatisha tamaa wawekezaji. Alisema hakuna uchumi wowote duniani uliofanya vizuri bila uwekezaji, iwe wa kutoka nje ya nchi hiyo au ndani ya nchi husika. Alibainisha kuwa Watanzania ndiyo wanaotakiwa kushika hatamu ya uchumi wao.

Kwa upande wake, Mhe. Lukuvi alisisitiza watendaji kuwa wabunifu na kufanya kazi kwa kasi zaidi ili kuongeza ufanisi na hatimaye kufikia malengo ya Ofisi ya Waziri Mkuu na Taifa kwa ujumla.

“Tujipange vizuri kufanya kazi kwa ubunifu na kasi zaidi ili kumsaidia Waziri Mkuu kutekeleza majukumu yake na hatimaye Serikali nzima ifanye vizuri kama inavyotarajiwa na wananchi,” alisisitiza Mhe. Lukuvi.

Mapema akiwakaribisha Mawaziri hao, Kaimu Katibu Mkuu katika Ofisi ya Waziri Mkuu Bw. Fanuel Mbonde aliwapongeza kwa uteuzi wao na kuwaahidi ushirikiano mkubwa. “Tuna imani kubwa nanyi na tunawaahidi ushirikiano na hatutawaangusha,” alibainisha Bw. Mbonde.

Aidha, Bw. Mbonde aliwaeleza Mawaziri hao majukumu makuu ya Ofisi ya Waziri Mkuu kuwa ni pamoja na uratibu wa shughuli za Serikali katika Sekta zote na ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano, uratibu wa maafa, uwekezaji na uwezeshaji na masuala ya UKIMWI. Masuala mengine aliyataja kuwa ni ya uchaguzi na ya vyama vya siasa.

Ofisi ya Waziri Mkuu hivi sasa inaundwa na Idara saba (7), Vitengo saba (7) na Taasisi nane (8).

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...