Na Mwandishi Wetu
MBUNGE wa Jimbo la Lindi Mjini, Salum Baruany amewashauri watu waliowahi kusoma katika mikoa ya Kusini mwa Tanzania kushirikiana katika kufanikisha tamasha la kuchangia maendeleo ya elimu kwa ajili ya mikoa hiyo.
Baruany aliyasema hayo juzi katika kikao cha maandalizi ya tamasha la kuchangia maendeleo ya elimu kwa mikoa ya Lindi, Mtwara na Ruvuma kilichofanyika Ukumbi wa Imasco, Temeke jijini Dar es Salaam.
Akiwa mmoja wa waalikwa wa vikao hivyo vya kila wiki, Baruany alielezea kukunwa kwake na ubunifu wa baadhi ya wanafunzi walioamua kuwahamasisha wenzao kukumbuka walikotoka kielimu, kwa lengo la kuwainua wengine.
“Nawapongeza sana. Ni wachache wanaoweza kukumbuka walikotoka, hasa kielimu. Hapa mmelenga, mikoa ya kusini iko nyuma kielimu, naamini wa kusaidia kupandisha hadhi ni ninyi wenyewe mliosoma kule na wadau wengine wanaoguswa na suala hili.
“Msikate tamaa, mtafanikiwa. Cha msingi ni kuwashirikisha na kuwashawishi wengine waliosoma ana kuwa karibu na mazingira ya kielimu ya mikoa hii. Nchi hujengwa na wananchi wenye moyo, nanyi kwa kuguswa kwenu, naamini elimu ya kusini itainuka kwa sababu ni vigumu mtu mmoja mmoja kuchangia na bado maendeleo ya kweli yakaonekana, bali kupitia mshikamano kama wenu,” alisema mbunge huyo.
Naye Mratibu wa tamasha hilo, Asanterabbi Mtaki, licha ya kumshukuru mbunge huyo kwa nasaha zake, aliwataka wadau wa elimu nchini kuungana na waliosoma mikoa ya kusini ili kufanikisha azma ya kuiinua kusini kielimu.
“Tangu awali tumeelezea hali ya elimu ya mikoa ya Kusini, kwa kweli si nzuri na inahitajika nguvu ya ziada, ndiyo maana tumeungana kuhakikisha tunafanikisha kitu kwa ajili ya shule za kusini na wanafunzi wake, hasa yatima, walemavu na wasiojiweza ili wapate haki ya kupata elimu bora,” alisema Mtaki.
Alisisitiza kuwa, kasi ya maandalizi ya tamasha hilo inaridhisha na kuongeza kuwa, nafasi ya waliosoma kusini kuchangia mawazo bado ipo, hasa kupitia vikao vya kila mwisho wa wiki vinavyofanyika ukumbi wa Imasco.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...