Frederick Siwale
Na Francis Godwin Blog,Iringa

MWANDISHI wa habari wa Radio Free Afrika na Star Tv mkoa wa Iringa Frederick Siwale(49) (pichani) amenusurika kuuwawa na viongozi wa serikali ya kijiji cha Maleusi wilaya ya Makete mkoani Iringa baada ya kuwekewa magogo njiani kwa lengo la kumteka na kumfanyia unyama huo alipokuwa akifuatilia sakata ya mgogoro wa ardhi kijijini hapo.

Tayari jeshi la polisi mkoani Iringa linawashikilia viongozi wawili wa serikali ya kijiji cha Maleusi katika Wilaya ya Makete mkoani Iringa kwa tuhuma za kutaka kumfanyia unyama huo mwanahabari huyo .

Siwale alikutwa na mkasa huo majira ya saa tano asubuhi baada ya kufika kijijni hapo kwa ajili ya kufuatilia na kuripoti sakata ya mgogoro wa ardhi uliozuka kati ya pande mbili kati ya kijiji na familia .

Kiini cha tukio hilo kimefahamika kuwa ni viongozi hao kuhusishwa katika tuhuma za ubadhilifu wa ardhi iliyotumika kwa maziko ya wananchi kuibinafsisha kwa mwekezaji.

Eneo lilitumika kwa maziko ambalo limefahamika kuwa nila ukoo wa Mbilinyi ambao kwa mujibu wa wasemaji wa ukoo huo Nazarena Mbilinyi na Paulo Mbilinyi eneo hilo lilianza kutumika kwa maziko tangu mwaka 1945.

Akizungumzia tukio hilo Siwale alisema baada ya kupata taarifa ya kuuzwa kwa eneo la makaburi kama ilivyo ada ya kazi yake alifunga safari kwenda Makete ili kupata undani wa tukio hilo.

“Nilifika Makete na siku iliyofuata nilianza safari ya kwenda kijijini huko Maleusi kwa ajili ya kukamilisha kazi yangu ya kihabari, nilipata ushirikiano mzuri kutoka kwa wananchi ikiwa pamoja na wahusika wa ukoo wa Mbilinyi waliokuwa wakiwalalamikia viongozi hao, lakini nilipotaka kukamilisha habari yangu kwa walalamikiwa mwenyekiti wa serikali ya kijiji aliwaita wajumbe na kuamuru ngoma ya lamgambo na mtendaji alipiga simu ambayo alisikika akisema njiani yawekwe magogo ili kunizuia kupita, na niliposikia hivyo nilikimbia kwa kubadili njia ndiyo ilikuwa salama yangu,” Alisema Siwale.

Kamanda wa jeshi la Polisi mkoani Iringa Evarist Mangala alikiri kukamatwa kwa viongozi hao ambao aliwataja majina watuhumiwa wa tukio hilo kuwa ni Rubern Mbilinyi mwenyekiti wa serikali ya kijiji cha Maleusi na Michael Sanga ambaye ni afisa mtendaji wa kijiji cha maleusi na kuwa watafikishwa mahakani baada ya uchunguzi kukamilika.

Klabu ya waandishi wa habari mkoa wa Iringa (IPC) imeeleza kusikitishwa na hatua ya viongozi hao wa vijiji kutaka kwenda kinyume na katiba ya nchi ambayo inatoa nafasi kwa kila mtanzani kupata habari na ile ya uhuru wa vyombo vya habari inayowataka wanahabari kufanya kazi yao bila kunyanyaswa.

Katibu mtendaji wa IPC Frank Leonrad alisema kuwa mbali ya kulipongeza jeshi la polisi mkoa wa Iringa kupitia kamanda wake Mangalla kwa kuwakamata wahusika hao bado alitaka viongozi wa serikali kutowaona wanahabari wanaofika katika maeneo yao kuwa ni maadui .

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

Kuna Maoni 4 mpaka sasa

  1. Kwanza, pole sana kwa msukosuko na hatari iliyokuwa inakukabili. Pili, baada ya kuisoma hii taarifa, sijauona uhusiano kati ya kuwekwa magogo ili kukuzuia kupita na njama za kukuua. Je, hayo magogo yaliashiria njama ya kukuzuia kupita, kukukamata, kukuadhibu au kukuua? Ukweli wake unajulikana au unahisiwa?

    ReplyDelete
  2. Njama pia ni kosa hata kama hukutenda hilo kosa. "Conspiracy to commit a crime is a crime"

    ReplyDelete
  3. Naungana na mdau wa juu kabisa. Nimeisoma hii habari nami imenichanganya kidogo. Ni vema kuripoti bila ya kushikilia upande. Sema tu waliagiza magogo yawekwe barabarani kunizuia kupita (kama ambavyo ulimsikia aliyekuwa akitoa maagizo kwa simu). Usiende mbali sana na kuhitimisha malengo yao maana tutakuhoji umbali huo umeufikiaje.

    Yote na yote, pole sana maana lako lilikuwa la nia njema kwako, kwao na kwetu sote. Usikate tamaa, jitahidi uipate hiyo habari maana inaonesha kuna shida kubwa huko. Mamlaka husika nazo ziingilie kati kutafiti kinachoendelea huko.

    ReplyDelete
  4. Asante kwa kuleta habari hii. Kwanza mimi ningependa sana kujua ukweli wa habari yenyewe,

    Wadau, kijiji kinaitwa Maleutsi sio Maleusi.

    Pili sielewi kinachoendelea hapo kijijini ni nini kwani habari hii hapo juu ina utata kidogo sijui aliyeandika alikuwa anaharaka au la.

    Inadai kuwa mwandishi wa habari alipokelewa vizuri na ukoo wa mbilinyi, sasa magogo aliyokuwa anadai kuwa mwenyekiti wa serikali ya kijiji alikuwa anapiga simu yawekwe wapi kama mtu ameshapokewa?

    Michuzi nakuomba kutumia mitandao yako mbalimbali naomba uifuatilie hii habari vizuri kwani nitawasiliana nawe kukuulizia.

    asante Mdau UK.

    ReplyDelete

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...