Dar es salaam Disemba 30, 2011. Kampuni ya simu ya mawasiliano ya Vodacom imepokea kwa mshtuko na huzuni kubwa taarifa za vifo vya wanahabari nguli nchini Bi. Halima Mchuka na Bw. John Ngahyoma.
Kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana, wanahabari hao wamefariki kwa siku tofauti akianza Halima juzi na baadae Ngahyoma aliyefariki asubuhi ya leo wote jijini Dar es salaam.
“Tunatoa mkono wa pole kwa familia za marehemu, waajiri wao na kipekee familia ya wanahabari nchini kwa kuondokewa na wapendwa wetu ambao walikuwa sehemu muhimu ya ujenzi wa tasnia ya habari na utangazaji nchini.”Alisema Ofisa Mkuu wa Masoko na Mahusiano wa Vodacom Tanzania Bi. Mwamvita Makamba.
Marehemu Bi. Halima Mchuka alikuwa mtangazaji wa Shirika la Utangazaji Tanzania – TBC na Marehemu Bw. John Ngahyoma hadi umauti unamkuta alikuwa ni mwanahabari wa Shirika la Utangazaji la Uingereza – BBC Ofisi ya Tanzania.
Marehemu wote wawili watakumbukwa kwa jinsi ambavyo walikuwa mahiri katika tasnia ya habari na utangazaji kwamba mchango wao utaendelea kuwa chachu hasa kwa vizazi vijavyo vya wanahabari chipukizi nchini.
“Tutamkumbuka sana Marehemu Halima ambae rekodi zinaonyesha kuwa ni mtangazaji wa kwanza mwanamke kutangaza mpira. Marehemu Ngahyoma kwa upande wake ni sehemu ya watangazaji wa awali kabisa wa televisheni Tanzania Bara mwanzoni mwa miaka ya tisini”Alisema Mwamvita.
Mwamvita amesema kampuni ya Vodacom daima ina thamini na kuheshimu mchango wa wanahabari katika maendeleo ya taifa na ushamirishaji ustawi wa jamii.
Mungu azilaze roho za Marehemu Bi Halima Mchuka na Bw. John Ngahyoma mahali pema peponi - Amen
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...