Na Mwandishi
Wetu
SERIKALI
imesema iko tayari kushirikiana na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) katika uhamasishaji wa
wananchi kujiunga na Mfuko wa Afya ya
Jamii (CHF) ili wawe na uhakika wa kupata matibabu wakati wowote.
Akizungumzia
umuhimu wa kujiuga na utaratibu wa bima za afya, Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya
Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Kassim Majaliwa alipotembea
ofisi za NHIF, Dar es
Salaam jana, alisema akiwa kama mwakilishi wa wananchi wa Jimbo la Ruangwa
atahakikisha anakutana na makundi mbalimbali na kuyaeleza umuhimu wa kuwa ndani
ya utaratibu wa CHF.
"Kwa kweli
kazi mnayofanya ni kubwa katika kuboresha huduma za afya kwa wanachama wenu na
kwa wananchi wa kawaida, nimefurahishwa sana na utaratibu wa kutambua kundi la waendesha
piki piki na makundi mengine, hawa mtaji wao ni afya yao hivyo wakiwa na
uhakika wa matibabu watafanya kazi zao za kujiingia vipato kila kukicha,"
alisema Majaliwa.
Akizungumzia
hospitali ya Wilaya ya Ruangwa, alisema kuwa bado inakabiliwa na changamoto
mbalimbali zikiwemo za ukosefu wa vifaa tiba kama x-ray na vingine hali
inayosababisha usumbufu kwa
wagonjwa kwa kulazimika kwenda umbali mrefu kutafuta huduma hiyo.Kutokana na
hali hiyo, aliuomba Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya kuiangalia hospitali hiyo
kwa jicho la pekee na kuipa kipaumbele katika fursa ya Mikopo ya Vifaa tiba na
Ukarabati wa majengo ili
iweze kuwa bora na kutoa huduma stahili kwa wananchi wa jimbo hilo.
Kwa upande wake
Naibu Mkurugenzi wa NHIF, Hamis Mdee, alisema kuwa, Mfuko umekuwa ukifanya
mambo mbalimbali yanayolenga moja kwa moja kuboresha huduma za matibabu vituoni hivyo
suala la fursa ya mikopo hiyo litafanyiwa kazi baada ya kupokea maombi kutoka
Hopsitali hiyo.
"Sisi
lengo letu ni kuona wanachama wetu wa NHIF, CHF na wananchi kwa ujumla popote
walipo wanapata huduma bora hivyo nasi tutahakikisha tunalifanyia kazi baada ya
kupokea maombi na uzuri
wa mikopo hii inalipwa kwa makato ya madai ambayo wanachama wetu
wametibiwa," alisema Mdee.
Wakati huo huo, sekondari za bweni mkoani pwani zimetakiwa kuwaandikisha
wanafunzi wao katika mfuko wa afya ya jamii ili waweze kunufaika na huduma zinazotolewa
na mfuko huo.
Afisa anayeshughulikia huduma za mfuko kutoka Mfuko wa Taifa wa Bima ya
Afya NHIF Rehani Athumani ametoa wito huo alipokutana na
wadau wa wadau wa sekta ya elimu waliokutana
mjini Kibaha kutathimini matokeo ya mtihani wa kidato cha nne kwa mwaka 2011.
Rehani amesema, utaratibu wa kuwajumuisha wanafunzi umefanywa kuwa rahisi
kwa sababu wanafunzi hao wanatakiwa kuchangia kati ya shilingi 1,000 mpaka
2,000 kwa mwaka hiyo kwa kuwawezesha kupata matibabu mwaka mzima.
Amesema utaratibu wa sasa wa kutoa fedha za tahadhari umekuwa na changamoto
kadhaa ikiwemo kukosekana kwa uhakika wa huduma za matibabu kwa wanafunzi
husika.
Naye mkuu wa mkoa huo Mwantum Mahiza amezitaka mamlaka za Halmashauri
kutumia fursa ya fedha ya tele kuboresha huduma ikiwemo kuwasilisha madai ya
kuomba fedha hizo NHIF mapema.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...