JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA MALIASILI NA UTALII

TAARIFA KWA UMMA

SHERIA HAIRUHUSU VIBALI KUUZWA KWENYE SHAMBA LA SAO HILL

Wizara ya Maliasili na Utalii inafafanua kuwa uvunaji wa Miti katika Shamba la Sao Hill unafuata utaratibu uliowekwa kisheria.

Sheria ya Misitu haimzuii mwananchi yeyote kuvuna mazao ya misitu kutoka kwenye misitu ya asili au ya kupandwa mradi awe amefuata sheria na taratibu zilizopo katika nyaraka husika, na hakuna nyaraka yoyote inayoagiza kwamba vibali vya uvunaji vigawiwe kwa viongozi ama watumishi wa serikali ili waviuze.

Ufafanuzi huu unatolewa kufuatia habari zilizoandikwa na gazeti moja kuwa vigogo wa Maliasili ndiyo wanaochukua vibali na kuviuza kwa wateja. Habari hiyo haina msingi maana utaratibu unaotumika unatekelezwa kwa uwazi na unajulikana kwa wateja wa mazao ya misitu.

Shughuli za uvunaji wa mazao ya misitu hufanywa kwa kufuata ‘Mwongozo wa Uvunaji Endelevu na Biashara ya Mazao ya Misitu’ wa mwaka 2007, ambao unaonyesha taratibu muhimu za kufuatwa katika shughuli za uvunaji na biashara ya mazao ya misitu.

Mwongozo huo unatokana na Sera ya Taifa ya Misitu ya mwaka 1998 na Sheria ya Misitu Namba 14 ya mwaka 2002, pamoja na Matangazo ya Serikali (Government Notices) Namba 69 na 70 ya mwaka 2006.

Shughuli za ugawaji wa mazao ya kuvuna katika kila shamba la Serikali hufanywa na Kamati ya Ugawaji Mazao ya Misitu ya sehemu husika.

Utaratibu uliopo ni kuwa mwananchi anayehitaji mazao kutoka katika misitu ya mbao laini, kama ile ya Sao Hill, hupeleka maombi yake kwa Meneja wa shamba linalohusika, kuanzia Januari 1 hadi tarehe 30 Aprili kila mwaka. Maombi hayo yanatakiwa yapokelewe mapema maana Kamati ya Ugawaji hufanya kikao chake mwezi Juni kila mwaka.

Aidha mwongozo wa uvunaji unaotumika hivi sasa unatanabaisha kuwa kipaumbele kitatolewa kwa mwombaji mwenye kiwanda lakini sio lazima awe na kiwanda.

Hata hivyo, taratibu hizo za uvunaji zimefanyiwa marekebisho yatakayoanza kutumika mwaka ujao wa fedha ambapo mwombaji sasa atalazimika kuwa na kiwanda ili aweze kupata kibali. Utaratibu huu ulitangazwa kwenye vyombo vya habari na tovuti ya Wizara www.mnrt.go.tz.

Katika utaratibu huo mpya Wizara itandaa utaratibu maalumu wa kuhakikisha wanavijiji wanaopakana na misitu ya serikali inayovunwa wananufaika na misitu hiyo kwa kuwa wanachangia kuilinda.

George Matiko
MSEMAJI WA WIZARA
Tarehe 24 Mei 2012

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

Kuna Maoni 1 mpaka sasa

  1. AnonymousMay 24, 2012

    Tatizo la Afisa Wanyamapori wanakula na Wakurugenzi wa wilaya plus Wakuu wa Wilaya. Safi sana Mh Kikwete kuwabadilisha wakuu wa Wilaya. Ila Magraduate Vijana walikufunzu Mali Asili wapewe vitengo wazee wanamaliza Wanyamapori wetu kwa kushirikiana na Vigogo na Wanasiasa

    ReplyDelete

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...