Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, Bw. Ludovick Utouh akisaini  katika kitabu cha wageni, wakati alipoutembelea ubalozi wa Tanzania  katika Umoja wa Mataifa,  na kuzungumza na  maafisa wa Ubalozi
 Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, Bw. Ludovick Utouh, akifafanua jambo wakati wa mazungumzo yake na Naibu Katibu Mkuu, Asha- Rose Migiro. Bw. Utouh akiongoza ujumbe wa watu watatu kutoka  Ofisi yake alikuwa hapa Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa kwa Ziara ya Kikazi ikiwa ni sehemu ya Maandalizi ya  Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu kuingia kwenye Bodi ya  Wakaguzi ya Umoja wa mataifa kuchukua nafasi inayoachwa wazi na Afrika ya Kusini. Tanzania inaingia kwenye Bodi hiyo mwezi  Julai mwaka huu.
 Bw. Otouh akiwa na Naibu Katibu Mkuu mara baada ya mazungumzo yao alipomtembelea Naibu Katibu Mkuu ofisini kwake
 CAG akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya maafisa wa Ubalozi wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, kutoka kushoto ni Mkuu wa Utawala Bw. Modest  Mero,  Mkurugenzi wa  Ukaguzi wa Nje, Bw. Fransis Kitauli, CAG,  Kaimu Balozi, Bibi Maura Mwingira,  Bw. Salhina Makumba, Naibu Mkurugenzi ukaguzi wa nje , Bibi  Salome Mollel, Mkurugenzi wa Utawala Ofisi ya Mdhibiti na Bw. Justin Kisoka afisa ubalozi anayehusika na Kamati ya  Tano ya  Bajeti na Utawala  ya Umoja wa Mataifa

Naibu Katibu Mkuu na   CAG akiwa katika picha ya pamoja na  kutoka kushoto, Bw. Justin Kisoka afisa wa Ubalozi wa Tanzania Umoja wa Mataifa anayehusika na Kamati ya Tano ya Masuala ya  Bajeti  na Utawala, Bw.Fransis Kitauli, Mkurugenzi wa  Ukaguzi wa Nje,  kulina kwa Naibu Katibu Mkuu ni, Bw. Salhina Mkumba  Naibu Mkurugenzi ukaguzi wa nje na Balozi Tuvako Manongi msadizi wa Naibu Katibu Mkuu.

Na  Mwandishi Maalum
New York

 Ikiwa imebaki  takribani miezi miwili  kabla ya Tanzania  kupitia Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi  Mkuu wa Hesabu za Serikali ( NAOT) kuingia rasmi katika  Ujumbe wa Bodi ya Wakaguzi ya Umoja wa Mataifa ( UNBOA).  Mkuu wa  chombo hicho, Bw. Ludovick Utouh anasema yeye binafsi na ofisi yake amekwisha kujipanga vema  kulikabili jukumu hilo.
Bw, Utoh ameyaeleza hayo  siku ya alhamisi wiki hii wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ,   Asha- Rose Migiro alipomtembelea ofisi  kwake . Bw. Utouh yupo hapa Umoja wa Mataifa akifuatana na   wasaidizi wake  watatu   kwa  ziara ya kikazi ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya awali  kujiunga na Bodi hiyo.
Katika mazungumzo hayo,  Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za serikali,  amemhakikishia Naibu Katibu Mkuu kwamba yeye binafsi anatambua ukubwa wa  kazi inayomkabili mbele yake,  na dhamana  anayoibeba  kwa niaba ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na watanzania wote.
“ Tanzania tumeaminiwa, sifa zetu zinafahamika na ndiyo maana tukapendekezwa kuingia kwenye Bodi  hii . Tumejianda na kujipanga, tutatumia uwezo wetu na  maarifa yetu  kulikabili jukumu hili na heshima hii tuliyopewa” akasisizia Bw. Utouh.
Akaeleza zaidi kwa kusema kwamba,  yeye na wataalamu wake, na kwa kushirikiana na wajumbe wengine wa Bodi hiyo, watalitekeleza jukumu hilo kwa uwazi na siyo kuviziana.
“ Tumejipanga kuifanya  kazi hii kwa misingi  na taratibu zote zilizoweka , tutafanya ukaguzi kwa uwazi, tutajadiliana na wahusika,  na siyo kuviziana lengo ni kuboresha utendaji wa chombo hiki muhimu” akasisitiza
Na kuongeza.  “Jambo la msingi na muhimu ni  lazima  kuwepo mawasiliano mazuri pamoja na   kuheshimiana na siyo kuviziana au kuumbuana. hapana, siyo ajenda yetu. Tutaangalia wapi kuna matatizo na kutoa mapendekezo ya  nini kifanyike ili kurekebisha kasoro hizo”.
Akabainisha zaidi kwa kusema, ukaguzi wa kuviziana na kuumbuana umeshapitwa na wakati. “Ukaguzi wa  kuviziana ni wa kizamani hata nyumbani ( Tanzania)  hatufanyi  aina hiyo, tumeendelea, tunafanya ukaguzi wa viwango, tunajadiliana , kuelekezana na siyo kuviziana au kukomoana tunataka kujenga na si kubomoa” akasisitiza
Akifafanua zaidi kuhusu maandalizi ambayo ofisi yake imekwisha kufanya,   ili kuwajenga uwezo mpana wataalamu wake, ameyataja   maandalizi hayo ni pamoja na  kuwapatia mafunzo ya vitendo na mitihani  maafisa wake, kufanya ziara za kikazi, kuhudhuria mikutano ya kimataifa inayohusiana na masuala ya ukaguzi wa hesabu ikiwamo ziara  hii ya kikazi ambaye yeye na maafisa wake wameifanya hapa Umoja wa Mataifa.
Katika Mazungumzo hayo, Naibu Katibu Mkuu Asha- Rose Migiro alimpongeza  Bw. Utouh,  Ofisi yake na Serikali kwa ujumla kwa kupata fursa hiyo ya kuingia kwenye Bodi ya Ukaguzi ya Umoja wa Mataifa.
Akasema kuwa, Tanzania imekuwa mfano wa kuingwa katika  Bara la Afrika katika eneo hilo la Ukaguzi wa mahesabu kiasi cha kutambuliwa na Umoja wa Mataifa.
Migiro akaeleza kuwa  Umoja wa Mataifa utatoa ushirikiano wa karibu kwa wajumbe wa Bodi ya Wakaguzi  ya UM  katika utekelezaji wa majukumu  waliyopewa.
Akabainisha kwamba dunia hivi sasa inapita katika kipindi kigumu cha kuyumba kwa uchumi na kwamba kila senti inayopatikana  inatakiwa kutumiwa kwa uangalifu..
“  Tunapita katika kipindi kigumu, hali ya uchumi ni ngumu na imewakwaza hata wachangiaji wakubwa wa UM, lakini hali ni mbaya pia hata kwa wachangiaji wadogo, na ndio maana Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa amekuwa akisisitiza sana kuwa na matumizi  bora na sahihi kwa kila senti inayopatikana”.
Kwa sababu hiyo akasema, kwa Tanzania kujiunga katika Bodi hii, itasaidia sana katika  kutoa ushauri na mapendekezo  ya  namna bora ya kuboresha uwajibikaji na uwazi”. akasititiza Migiro.
Akiwa hapa  Umoja wa Mataifa, Bw. Utouh na ujumbe wake  pamoja na kukutana na kufanya mazungumzo na Naibu Katibu Mkuu pia amekutana na baadhi wa  wakuu wa mashirika ya  UM  wakiwamo watendaji wa UNDP, UN-Women,  Msimamizi Mkuu wa Ofisi ya Katibu Mkuu, wajumbe wa  Kamati ya Tano inayohusika na masuala ya bajeti na utawala na wataalamu mbalimbali.
Wakati wa mazungumzo na watendaji hao,  walielezea kufurahishwa kwao na hata kushangazwa na namna Bw. Utouh alivyoonyesha uelewa wa hali  ya juu kuhusu masuala ya fedha na uhasibu wa UM lakini kubwa zaidi namna walivyojipanga  kabla  hata ya muda wa kuchukua ujumbe huo haujafika jambo lililoonyesha wazi kwamba Tanzania imejipanga na inajua nini inachotarajiwa kukifanya.
Akitoa tadhimini  yake kuhusu ziara yake hiyo ya kikazi, Bw. Utouh anasema ingawa ratiba ilikuwa  imebanana sana lakini katika  muda mfupi amewezea kujifunza mambo mengi, na kupata picha ya hali halisi ya mambo  jambo ambalo anasema limemweka yeye na wataalamu wake katika nafasi nzuri zaidi ya kiutendaji.
Mwishoni mwa mwaka jana, Baraza Kuu la 66 la Umoja wa Mataifa lilipitisha uteuzi wa Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali  kuwa  mjumbe wa Bodi ya Wakaguzi ya Umoja wa Mataifa.
Tanzania inachukua nafasi inayoachwa wazi na Afrika ya Kusini   mwezi Julai  mwaka huu na itafanya kazi na wajumbe wengine wawili wa  Bodi hiyo  kutoka   Uingereza na China. Tanzania  itadumu kwenye  bodi hiyo kwa kipindi cha  miaka sita.   Aidha Tanzania inakuwa nchi ya  tatu  kutoka Afrika baada ya Ghana na  Afrika ya Kusini kuwa mjumbe wa Bodi ya Wahasibu ya Umoja wa Mataifa.
  Baadhi ya majukumu ya  Bodi ya Wahasibu ya Umoja wa Mataifa ni kukagua vitabu vya hesabu za Makao Makuu ya UM, Mashirika na Asasi zote zilizochini ya UM,  Misheni za Ulinzi wa  Amani za Umoja wa Mataifa na miradi  mbalimbali inayosimamiwa  na Umoja wa Mataifa
Bodi hiyo hukutana mara mbili kwa mwaka katika miezi ya Juni na Novemba ingawa wanaweza kukutana wakati wowote pale wanapohitajika. Aidha wajumbe hao watatu watasaidiwa na wakurugenzi watatu kutoka nchi hizo.  Makazi ya wakurugenzi hao  na ofisi zao zakudumu zitakuwa Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

Kuna Maoni 3 mpaka sasa

  1. MkiboshoMay 12, 2012

    Mh. umeweka sana sana heshima yako na taifa kwa ujumla hongera sana.
    Tatizo ni serikali sidhani kama watawachulia hatua mafisadi waliotafuna fedha zetu kama mchwa!

    ReplyDelete
  2. AnonymousMay 13, 2012

    Hivi UN hawakuona watanzania wengine wa kuwateua zaidi ya Migiro na Utuoh ambao ni Wakilimanjaro na Wakaskazini??

    ReplyDelete
  3. AnonymousMay 13, 2012

    Jamani tujifunze kufahamu mambo kabla ya kuchangia. Uteuzi wa CAG kukagua UN siyo 'as a person' ni institution yaani ni ofisi ya taifa ya ukaguzi Tanzania. So hata akistaafu atakayekuja ukaguzi utaendelea for 6 years.

    ReplyDelete

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...