JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
KURUGENZI YA MAWASILIANO YA RAIS IKULU
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Makamu wa Pili wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Mheshimiwa Balozi Seif Ali Idd amemhakikishia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli kuwa hali ya Zanzibar ni shwari na Wazanzibar wanasubiri kutangaziwa tarehe ya kufanyika kwa uchaguzi.
Balozi Seif Ali Idd ameyasema hayo Ikulu jijini Dar es salaam leo tarehe 20 Januari, 2016 mara baada ya kukutana na kufanya mazungumzo na Rais Magufuli.
"Mimi nimekuja kumpa taarifa juu ya hali yetu Zanzibar inavyokwenda, nimemueleza kwamba Zanzibar ipo salama, Zanzibar ina utulivu na ina amani, nimeona nije nimueleze kwa kuwa yeye ni kiongozi wetu" alisisitiza Balozi Seif Ali Idd.
Makamu huyo wa pili wa Zanzibar ameongeza kuwa kutokana na uwepo wa amani na utulivu, wananchi wa Zanzibar wanaendelea na shughuli zao kama kawaida tofauti na inavyoripotiwa na baadhi ya vyombo vya habari.
"Hayo yanayoandikwa kwenye magazeti kuwa Zanzibar kuna fujo, Zanzibar kutatokea machafuko sio kweli, na kama unavyojua uchaguzi ulifutwa na tume ya uchaguzi na tunasubiri tarehe mpya ya uchaguzi itangazwe na tume ili tufanye uchaguzi" amebainisha Balozi Seif Ali Idd.
Gerson Msigwa.
Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano, IKULU.
Dar es salaam.
20 Januari, 2016.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...