Na Bashir Yakub.
Mgawanyo wa mali za marehemu hutegemea mambo makubwa mawili. Kwanza ni ikiwa marehemu ameacha wosia na pili ni ikiwa hakuacha wosia. Ikiwa ameacha wosia basi huwa ni rahisi sana kwani mali zake zitagawanywa kwa kufuata wosia. Ikiwa hakuacha wosia hapa huwa si kwepesi sana kwani mali zake hulazimika kugawanywa kwa mujibu wa sheria zilizopo wakati sheria zenyewe ziko tatu tofauti. Wakati mwingine ni kazi kidogo kuamua sheria ipi itumike katika kugawa mali za marehemu.
1.SHERIA IPI ITUMIKE KATIKA KUGAWA MALI ZA MAREHEMU.
Ikiwa hakuna wosia swali la sheria ipi itumike katika kugawa mali za marehemu lazima liibuke. Kwa ujumla kuna sheria tatu zinazotumika katika kugawa mirathi.
( a ) Sheria ya kwanza ni sheria ya urithi ya India 1865 . Hapa kwetu sheria hii hujulikana kwa wengi kama sheria ya mirathi ya serikali.
Sheria hii hutumika kwa marehemu ambaye hakuishi maisha ya kiislam na hakuishi maisha ya kimila. Zaidi tunaweza kusema kuwa sheria hii hutumika kwa wakristo na madhehebu mengine ambayo sio ya kiislam.Hata hivyo hata muislam ambaye itathibitika kuwa hakuishi maisha ya kiislam wala ya kimila sheria hii itatumika kugawa mali zake.
( b ) Pili ni sheria ya kiislam. Sheria hii hutumiwa na waumini wa dini ya kiislamu. Lakini haitoshi kusema inatumiki kwa waislam isipokuwa inatosha kusema itatumika kwa waliokuwa wakiishi maisha ya kiislam. Sheria hii hufuata misingi ya Quran tukufu na Sunnah.
( c ) Tatu ni sheria za kimila. Sheria hizi hutumika iwapo marehemu aliishi maisha ya kimila. Mfano wake ni kama tunavyoona kwa wamasai, wahadzabe, na makabila mengine hasa vijijini ambao huishi maisha yao yote pasi na kufuata dini yoyote isipokuwa mila tu. Sheria hii imo katika kanuni za urithi, tangazo la serikali namba 436 la mwaka 1963.
Kwa ujumla swali la sheria ipi itumike kugawa mali za marehemu pale ambapo hakuacha wosia, hujibiwa kwa kuangalia aina ya maisha aliyoishi marehemu.



Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...