Na Greyson Mwase, Dar es Salaam
Wawekezaji kutoka katika makampuni yanayojihusisha na uzalishaji wa nishati ya umeme kutoka nchini China, wameeleza nia ya kuwekeza kwenye sekta ya nishati nchini ili iweze kuwa na mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi.
Waliyasema hayo katika kikao na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini anayeshughulikia masuala ya nishati Dk. Mhandisi Juliana Pallangyo pamoja na wataalam kutoka Wizara ya Nishati na Madini pamoja na taasisi mbalimbali ikiwa ni pamoja na Shirika la Umeme Nchini (TANESCO), Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) na Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA)
Akizungumza katika kikao hicho Mwakilishi kutoka Umoja wa Wafanyabiashara katika Jamhuri ya Watu wa China nchini Tanzania Lin Zhiyong, alisema kuwa nia ya makampuni yanayojishughulisha na uzalishaji wa nishati ya umeme ni kubaini fursa zilizopo katika sekta ya nishati nchini kabla ya kuja kuwekeza rasmi
Aliongeza kuwa ujumbe maalum wa wawekezaji kutoka nchini China unatarajiwa kuwasili nchini mapema wiki ijayo kwa ajili ya kupata taarifa mbalimbali zenye kubainisha fursa za uwekezaji nchini ikiwa ni pamoja na mpango kabambe (master plan), sera, na mpango mkakati katika sekta ya nishati, kabla ya kusaini makubaliano ya awali kwa ajili ya uzalishaji wa nishati ya umeme.
Zhiyong alisisitiza kuwa wawekezaji kutoka China wako tayari kushirikiana na wawekezaji wa ndani ya nchi kwenye uzalishaji wa nishati ya umeme ili taifa liweze kupata nishati ya uhakika kwa ukuaji wa uchumi wa nchi.
Wakati huo huo, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini anayeshughulikia nishati Dk. Mhandisi Juliana Pallangyo alishukuru ujumbe huo na kueleza kuwa fursa za uwekezaji kwenye sekta ya nishati ni nyingi na kuwataka kuchangamkia fursa hizo.
“Wananchi wanahitaji nishati ya uhakika ambayo ni kichocheo cha ukuaji wa uchumi wa nchi, hivyo tunawakaribisha kuwekeza katika uzalishaji wa nishati ya umeme kwa kuwa tuna vyanzo vingi kama vile gesi, jotoardhi, makaa ya mawe, jua, upepo n.k,” alisisitiza Dk. Palangyo.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini anayeshughulikia nishati Dk. Mhandisi Juliana Pallangyo (kulia) akisalimiana na mmoja wa wajumbe kutoka kampuni uzalishaji wa makaa ya mawe ya Shenhua
Ningxia Group Co. Limited kutoka China. (kushoto). Katikati ni
Mwakilishi kutoka Umoja wa Wafanyabiashara katika Jamhuri ya Watu wa
China nchini Tanzania, Lin Zhiyong.
Naibu
Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini anayeshughulikia nishati,
Dk. Mhandisi Juliana Pallangyo (kulia) akielezea fursa za uwekezaji
katika sekta ya nishati nchini. Kushoto ni Mwakilishi kutoka Umoja wa Wafanyabiashara katika Jamhuri ya Watu wa China nchini Tanzania Lin Zhiyong.
Sehemu ya ujumbe kutoka nchini China ukifuatilia majadiliano mbalimbali yaliyokuwa yanaendelea katika kikao hicho.


Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...