Na Eleuteri Mangi-MAELEZO
Watoto wa kike 20,000 kutoka mkoa wa Mara watanufaika kwa fursa ya kupata elimu kupitia
Mfuko wa Graca Machel (Graca Machel Trust) ambao umejikita katika kusaidia wanawake na
watoto nchi kadhaa za Afrika.
Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
(TAMISEMI), Mhe. George Simbachawene mara baada ya mazungumzo na Mama Graca
Machel alipomtembelea ofisini kwake leo jijini Dar es salaam.
“Ni fursa nzuri ya kushirikiana na wadau wa ndani na nje ya nchi kuwasaidia watoto wetu wa
kike kielimu ambayo itawasaidia kutoka katika jamii ya umasikini na kuhakikisha wamepata
fursa ya kuvuka umri wa vishawishi na maamuzi yasiyo sahihi” alisema Waziri Simbachawene.
Watoto hao watakaonufaika na Mfuko huo mkoani Mara watatoka katika shule 104 ambapo
inatarajiwa kuwafikia watoto wa kike wengi zaidi mara baada kuanza kutoa huduma hiyo
mkoani humo.
Waziri Simbachawene amesema kuwa Mama Graca Machel amechagua kuja katika Tanzania
kutokana ushirikiano mzuri uliopo kati ya Tanzania na Msumbiji kwa kuzingatia mchango
mkubwa wa Tanzania kwa nchi hiyo.
Aidha, Waziri Simbachawene amemshukuru Mama Graca Machel kwa kujali na kuuchagua
mkoa wa Mara ambao ndio mkoa alipozaliwa Mwasisi wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage
Nyerere.
Kwa upande wake Mama Graca Machel amemshukuru Waziri Simbachawene kwa mapokezi na
ushirikiano alioupata katika Serikali ya Awamu Tano iliyopo madarakani na kuahidi kuendelea
kusirikiana nao ambapo anaamini mpango wa kuwasaidia watoto wa kike kupita taasisi yake
utapanuka na hatimaye kuweza kuwafikia watoto wa kike wengi zaidi kupitia mikoa yote nchini.
“Lengo ni kuwabakisha watoto wa kike shuleni ili wapate elimu, ni lazima tusaidiane wote, tuna
kila sababu ya kusaidiana” alisema Mama Graca Machel.
Uhusiano wa Tanzania na Msumbiji ni wa kihistoria kwani wananchi wa nchi hizo
walishirikiana katika shughuli mbalimbali chini ya mwavuli wa unasaba na ushirikiano katika
biashara na tamaduni kwenye miji ya Unguja, Kilwa, Lindi na Mtwara kwa upande wa Tanzania
na katika miji ya Chilimbo, Tete, Pemba na Sofala nchini Msumbiji.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe.
George Simbachawene (kulia) akiongea na Mama Graca Machel (kushoto) alipomtembelea
ofisini kwake leo jijini Dar es salaam.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe.
George Simbachawene akiongea na Mama Graca Machel (hayupo pichani) alipomtembelea
ofisini kwake leo jijini Dar es salaam.
Mama Graca Machel akiongea na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na
Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. George Simbachawene (hayupo pichani) alipomtembelea
ofisini kwake leo jijini Dar es salaam.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe.
George Simbachawene (kulia) akiteta jambo na Mama Graca Machel (kushoto) mara baada ya
mazungumzo ofisini kwake leo jijini Dar es salaam.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...