Profesa Kennedy Gastorn, Katibu Mkuu mpya AALCO
Mkurugenzi wa masuala ya Kimataifa katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Kennedy Gastorn amechaguliwa kuwa Katibu Mkuu mpya wa Jumuiya ya Mashauriano ya Masuala ya Kisheria katika nchi za Asia na Afrika-‘Asian-African Legal Consultative Organisation-AALCO’.
Profesa Gastorn alichaguliwa kwa kauli moja wakati wa Mkutano wa 55 wa Jumuiya hiyo yenye jumla ya nchi wanachama 47 uliofanyika Mjini New Delhi, India tarehe 17 Mei, 2016 na kuhudhuriwa pia na Mkurugenzi wa Sheria katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Baraka Luvanda.
Aidha, Profesa Gastorn ambaye alikuwa ni mgombea pekee wa nafasi hiyo baada ya kupendekezwa na Tanzania na kupitishwa na Umoja wa Afrika, anachukua nafasi ya Katibu Mkuu anayemaliza muda wake Profesa Rahmat Mohamad wa Malaysia ambaye muda wake unamalizika rasmi ifikapo mwezi Agosti, 2016 na Profesa Gastorn anatarajia kukabidhiwa madaraka hayo mwanzoni mwa mwezi Agosti, 2016.
Mkutano wa Jumuiya ya AALCO ulifanyika kuanzia tarehe 16 Mei na kumalizika tarehe 20 Mei, 2016.
Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dar es Salaam, 20 Mei, 2016.



Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...