Serikali imepongeza taasisi isiyo ya Kiserikali ya Makumbusho Urithi
Tanga kwa jitihada nzuri walizofanya za kuandaa makumbusho itakayo
hifadhi utamaduni wa wakazi wa Mkoa wa Tanga.
Pongezi hizo zimetolewa leo jijini Tanga na Naibu Waziri wa
Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo alipotembelea Makumbusho hayo ya
Urithi Tanga alipokuwa katika ziara yake ya kikazi mkoani hapo iliyolenga
kujua uendeshwaji wa shughuli za kisekta.
“Kazi hii ya ukusanyaji wa taarifa mbalimbali za wakazi wa Tanga kuanzia
ngazi ya Makabila yote saba ya Mkoa wa Tanga,Mila na Desturi zao,
pamoja na kuhimiza ukarabati majengo ya kale kweli mnahitaji pongezi
kwa uzalendo huo”,
Naibu Waziri wa Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo Mhe. Anastazia Wambura akitazama baadhi ya picha zenye historia zilizohifadhiwa katika Makumbusho ya Urithi wa Tanga (kushoto) ni Mkurugenzi wa Makumbusho hayo Mhandisi Raymond Mhando akitoa maelezo ya picha hizo.
“Serikali ya China iliahidi kusaidia kujenga Majumba ya Makumbusho kwa
nchi za Afrika hivyo andikeni barua ya Wizarani kuwa ajili ya kuendeleza
makumbusho haya halafu tutaiwasilisha Ubalozi wa China”.alisema Naibu
Waziri Wambura,
Kwa upande Mkurugenzi wa Makumbusho ya Urithi Tanga Mhandisi
Godwin Mhando alisema lengo la kuanzisha makumbusho hayo ilikuwa ni
kutaka kutunza historia ya Mkoa wa Tanga pamoja na kulinda kuhifadhi
Mila na Desturi za watu wa Tanga kwa ajili ya vizazi vijavyo kwani Mkoa
huo unahistoria kubwa katika nchi.
“Makumbusho haya ya Urithi Tanga siyo kwa maslahi binafsi bali kwa
wanatanga wote na tumeamua kufanya uhifadhi huu kwa kuwa tumeona
ipo haja ya kuhifadhi historia Mkoa wetu.”alisema Mhandisi Mhando.
Jengo la Makumbusho ya Urithi wa Tanga linalohifadhi Utamaduni wa wakazi wa Tanga pamoja na historia jiji la Tanga Mkoani hapo.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Tanga Thobias Mwilapwa alisema ofisi yake
itajitahidi kushirikiana na viongozi wa makumbusho hayo kwa kuhakikisha
inafikia malengo iliyojiwekea kwa maslahi ya wakazi wa Tanga pamoja na
Watanzania wote kwa ujumla.
Aidha Mkurugenzi huyo wa makumbusho aliendelea kusema kupitia ofisi
hiyo wamekuwa wakipanga siku ambayo hufanya maonesho ya shughuli za
kiutamaduni kama matibabu ya kiasili,kuwepo kwa vyakula vya asili hii
ikiwa ni siku ya maadhimisho ya kuenzi utamaduni wa wakazi wa Tanga.
Hata hivyo kila Mtanzania ametakiwa kujali asili yake pamoja utamaduni
wake na pia kuenzi kwani ni urithi mkubwa kwa vizazi vijavyo.imeandikwa na Anitha Jonas – MAELEZO


Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...