WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika kongamano la kibiashara kati ya Tanzania na India linalotarajiwa kufanyika julai 10 mwaka huu.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo, Meneja mahusiano wa Kituo cha Uwekezaji (TIC) Daud Riganda amesema kuwa lengo la kongamano hilo ni kuwaleta pamoja wafanyabiashara wa nchi hizo mbili kwa ajili ya kujadiliana na kubadilishana uzoefu katika masuala ya biashara na uwekezaji.
Amesema Tanzania na India ni nchi zenye ushirikiano wa muda mrefu katika masuala ya kisiasa, kijamii na kibiashara hivyo ujumbe wa wafanyabiashara kutoka India utajumuisha sekta za kilimo, viwanda, miundombinu, elimu, afya, nishati na maji.
Riganda amesema kati ya mwaka 1990 na Juni 2016 TIC imeweza kusajili jumla ya miradi 442 ya uwekezaji kutoka India yenye thamani ya Dola za Marekani bilioni 2.12.
Alisema miradi hiyo inayoongoza katika kusajiliwa ni ile iliyopo katika sekta ya viwanda na usindikaji ambapo takribani asilimia 53 ni miradi ya kutoka sekta hiyo.
Pia alisema kongamano hilo limeandaliwa na TIC kwa kushirikiana na Taasisi ya sekta binafsi nchini(TPSF), Jukwaa la Biashara la India(IBF) na Shrikisho la Biashara na Viwanda la India(FICCI).
Alisema makampuni kutoka India ni miongoni mwa mataifa yanayoshika nafasi ya tano za juu kiuwekezaji hapa nchini kwa kuzingatia thamani katika uwekezaji.
Hata hivyo aliwataka wafanyabiashara kushiriki kikamilifu katika kongamano hilo ili kujijengea uwezo na kuweza kufikia malengo ya sekta ya uwekezaji kupitia viwanda.
Meneja mahusiano Kituo cha Uwekezaji (TIC) Daud Riganda akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) kuhusu kongamano la kibiashara kati ya Tanzania na India linalotarajiwa kufanyika julai 10 mwaka huu, ambalo Waziri Mkuu Kassim Majaliwa anatarajiwa kuwa mgeni rasmi. Leo jijini Dar es Salaam. Kulia ni Meneja Uhamasishaji Uwekezaji wa Nje Zacharia Kingu.
Waandi wa habari wakimsikiliza Meneja mahusiano Kituo cha Uwekezaji (TIC) Daud Riganda, leo jijini Dar es Salaam.


Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...