WAZIRI Tizeba amemwagiza Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo kuwasimamisha kazi Wakuu wa Taasisi, Idara na kuwaamisha Wakuu wa Vituo ya Utafiti kuanzia leo.
Waziri wa Kilimo Mifugo na Uvuvi, Mhe. Dkt. Charles Tizeba amemwagiza Katibu Mkuu, Wizara ya Kilimo Mifugo na Uvuvi(Idara Kuu- Kilimo) Dkt. Dkt. Florens Turuka kuwasimamisha kazi na kuwabadirisha Vituo vya kazi, Wakuu wa Taasisi na Idara zilizo chini ya Wizara.
Waliosimamishwa kazi ni pamoja na Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Taifa ya Hifadhi ya Chakula, (NFRA) Bwana Charles Walwa, Mkurugenzi wa Mipango na Uendeshaji, Bibi. Anna Ng’oo, Mkurugenzi wa Masoko, Bwana Mikalu Mapunda na Meneja wa Kanda ya Songea Bwana Jeremia Mtafya.
Waziri wa Kilimo Mifugo na Uvuvi, Dkt. Tizeba alisema kuwa sababu ya kusimamishwa kwao inatokana na tuhuma ya kuchelesha kwa mchakato wa uuzaji wa mahindi kwa wanunuzi ambao walikuwa wameomba kununua mahindi hayo ambayo yamekuwa kwenye akiba kwa kipindi kirefu.
Waziri Tizeba aliongeza kuwa Meneja wa Kanda Dodoma Bwana Deusdedit Mpazi atakaimu nafasi ya Mtendaji Mkuu Wakala wa Taifa Hifadhi ya Chakula mpaka hapo itakapoamuliwa vingine.
“Ndugu zangu naomba ielewe kuwa, hatujakurupuka kuwasimamisha kazi Watendaji hawa, tumejiridhisha kuwa walizembea katika kutoa maamuzi na kuisababishia Serikali hasara kubwa kwani, kiasi cha mahindi kilichokuwa kiuzwe kilikuwa kikubwa” Alisisitiza Waziri Tizeba.
Aidha, Waziri Tizeba amemwagiza Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo, Dkt. Turuka kumuondoa kwenye nafasi yake kazi, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Usalama wa Chakula, Bwana Ombaeli Lemweli kwa kosa la kutoa vibali vya kusafirisha mahindi kwenda nje ya nchi bila ya kuzingatia taratibu za utoaji wa vibali hivyo.
Dkt. Tizeba amesema kuwa kwa sasa nafasi ya Bwana Ombaeli Lemwli, itaongozwa na aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko, Bwana Eliyampa Kiranga.
Wengine walioamishwa kutoka katika Vituo vyao ni pamoja na aliyekuwa Mkuu wa Kituo cha Utafiti – Uyole (Mbeya) Dkt. Zakaria Malley ambaye anahamishiwa Kituo cha Utafiti, Selian (Arusha).
Mkuu wa Kituo cha Utafiti Selian (Arusha) Dkt. Totole Lugendo Bucheyeki ambaye anakwenda Kituo cha Utafiti Ilonga (Morogoro) na Dkt. Arnold Msongi anatoka Ilonga (Morogoro) na kwenda Uyole (Mbeya).
Wakati huohuo Bwana John Maige kutoka Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko atakaimu nafasi ya Mkurugenzi wa Bodi hiyo mpaka hapo itakapoamuliwa vingine.



Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...