Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO.
Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika Maadhimisho ya Siku ya Nile “Nile Day” yatakayofanyika wiki ijayo  (Februari, 22), jijini Dar es Salaam.

Maadhimisho hayo yameandaliwa na Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa kushirikiana na taasisi inayosimamia shughuli za wanachama wa Bonde la Mto Nile-Nile Basin Initiative (NBI).

Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Mha. Gerson Lwenge ameyasema hayo hivi karibuni alipokuwa akiongea na mwandishi wa habari hii kuhusu maadhimisho hayo.

Mha. Lwenge amesema kuwa maadhimisho hayo hufanyika kila mwaka miongoni mwa nchi wanachama 10 zilizo katika bonde la mto huo; ambazo ni Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, Ethiopia, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Sudan, Sudan ya Kusini na Misri, ambapo kwa mwaka huu siku hiyo inasherekewa nchini Tanzania.

“Lengo la Siku ya Nile ni kukuza uelewa kwa watu wote kuhusu umuhimu wa ushirikiano baina ya nchi zote wanachama, masuala yanayotekelezwa na faida inayopatikana kutokana na matumizi bora ya rasilimali za Bonde la Mto Nile,” alisema Mha. Lwenge.

Amefafanua kuwa maadhimisho hayo yatasaidia kufahamu zaidi kuhusu umuhimu wa mto huo katika kutupatia chakula cha uhakika, maji, nishati ya umeme na faida nyingi kiuchumi pamoja na kubadilishana mawazo ya jinsi ya kulinda na kutumia rasilimali za mto huo kwa pamoja na kwa usawa na uendelevu kwa ajili ya kizazi cha leo na vizazi vijavyo.

Mha. Lwenge ameongeza kuwa maadhimisho hayo yataambatana na maandamano kutoka viwanja vya Mnazi Mmoja mpaka Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere, upandaji wa miti, maonesho ya vitu mbalimbali vinavyohusu Sekta za Maji na Umwagiliaji, burudani za kiutamaduni, pamoja na za watoto wa shule za msingi na sekondari.

Aidha, Waziri Lwenge amewataja washiriki wa maadhimisho hayo kuwa ni mawaziri wanaohusika na maji kutoka nchi wanachama, mabalozi, wawakilishi kutoka NBI, wabunge, washirika wa maendeleo, wataalamu, wanafunzi wa vyuo, sekondari na shule za msingi, taasisi binafsi, vyombo vya habari pamoja na umma kwa ujumla.

NBI ilianzishwa rasmi mwaka 1999, jijini Dar es Salaam, ambapo nchi wanachama waliungana na kukubaliana kuanzisha umoja wa ushirikiano katika kusimamia na kuendeleza rasilimali za Bonde la Mto Nile.


Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...