Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto leo imezindua sehemu ya kuchezea watoto wanaolazwa na wale wanaofika katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) kwa ajili ya kupatiwa matibabu mbalimbali. 
 Sehemu ya kuchezea watoto imezinduliwa leo na Kaimu Mkurugenzi wa Huduma za Upasuaji wa hospitali hiyo, Dk Julieth Magandi kwa niaba ya Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Dk Mpoki Ulisubisya. 
 Akizindua sehemu ya kuchezea watoto, Dk Magandi amesema kuwapo kwa sehemu ya kuchezea kutaongeza chachu ya watoto kuacha kuogopa hospitali kwani watavutiwa na kutambua kwamba wapo katika mazingira salama na rafiki wakati wakipatiwa huduma za matibabu. 
 “Nawapongeza Hospitali ya Taifa Muhimbili licha ya kufungua sehemu hii ya michezo leo bado ndani ya jengo mmeweka vivutio vingi kwenye kuta zote za jengo la watoto ili kuhakikisha watoto wanafurahi,” amesema Dk Magandi. 
 Dk Magandi amesema kuwa sehemu hiyo ya michezo ambako pamefungwa vifaa vya kisasa vya kuchezea itawasaidia watoto wanaokaa muda mrefu hospitalini kuanzia mwezi mmoja hadi mwaka mmoja kupata faraja. 
 “Nina imani kuwa sehemu hii itawapa uhuru wa kucheza kwa nafasi na usalama zaidi ukilinganisha na hali ilivyokuwa awali. Ni kweli ndani ya jengo kuna michoro ya wanyama mbalimbali na katuni zinazotoa taswira rafiki kwa watoto na kuondoa mawazo ya kwamba hospitali ni sehemu ya maumivu muda wote, lakini kuongezeka kwa sehemu hii ya michezo itachochea zaidi hali ya watoto kupenda kutibiwa na kujisikia huru zaidi,” amesema. 
 Pia, Dk Magandi amewashukuru Human Welfare Trust Fund kwa kujenga sehemu ya kuchezea watoto kwani wameonyesha wanawajali watoto wetu. 
 Naye Mkurugenzi wa Tiba katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH), Dk Hedwiga Swai akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa hospitali hiyo, Profesa Lawrence Museru amesema kwamba watoto wanaolazwa katika Jengo la Watoto ni wale wanaohitaji tiba za upasuaji, wenye majeraha ya moto, utapiamlo, matatizo ya moyo, wenye matatizo ya mishipa ya fahamu, figo, magonjwa ya tezi na kisukari, magonjwa ya mfumo wa damu, macho na watoto wanaohitaji ushauri wa lishe bora.
 “Sehemu hii ya michezo itatumika kwa watoto wanaokuja kliniki kwa ajili ya uchunguzi wa magonjwa mbalimbali, wale wanaofatiliwa maendeleo yao baada ya kupata nafuu na wale wanaopata ruhusa ya kurudi nyumbani na watoto waliolazwa wodini,” amesema Dk Swai.
Baadhi ya wageni waliofika Muhimbili kushuhudia uzinduzi huo wakimsikiliza mgeni rasmi Dk Magandi.


Kaimu Mkurugenzi wa Huduma za Upasuaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Dk Julieth Magandi akikata utepe kuzindua sehemu ya kuchezea watoto wanaotibiwa Muhimbili. Dk Magandi amezindua sehemu ya kuchezea watoto kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk Mpoki Ulisubisya. Kutoka kushoto ni Mkurugenzi wa Tiba Muhimbili, Dk Hedwiga Swai na mwakilishi wa Human Welfare Trust, Bi. Veena Jog.
Kaimu Mkurugenzi wa Huduma za Upasuaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Dk Julieth Magandi na wageni baada ya kuzindua sehemu ya kuchezea watoto wanaotibiwa Muhimbili. Dk Magandi amezindua sehemu ya kuchezea watoto,
Sehemu ya kuchezea watoto wanaotibiwa Muhimbili.
Kaimu Mkurugenzi wa Huduma za Upasuaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Dk Julieth Magandi  akimshukuru mwakilishi wa Human Welfare Trust, Bi. Veena Jog.  baada ya  kuzindua sehemu ya kuchezea watoto wanaotibiwa Muhimbili. 

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...