Kamati za Kudumu za Bunge zitaanza kukutana Mjini Dodoma kutekeleza
majukumu yake kuanzia Tarehe 20 Machi, 2017 hadi Tarehe 2 Aprili, 2017 kabla ya
kuanza kwa Mkutano wa Saba wa Bunge uliopangwa kuanza Tarehe 4 Aprili 2017.
Kufuatia shughuli hizi za Kamati, Waheshimiwa Wabunge wanatarajiwa kufika Mjini
Dodoma Jumapili tarehe 19 Machi, 2017.
Pamoja na Shughuli nyingine zitakazotekelezwa na Kamati katika Kipindi hiki,
kuanzia Tarehe 20 hadi 27 Machi 2017, Kamati zitatembelea maeneo mbalimbali
nchini kukagua miradi ya maendeleo iliyotengewa fedha kwa Mwaka wa Fedha
2016/2017 inayotekelezwa na Wizara/Idara zinazosimamiwa na Kamati husika.
Baada ya ziara hizo kukamilika, Kamati zitachambua Taarifa za utekelezaji wa
Bajeti za Wizara inazozisimamia kwa Mwaka wa Fedha unaoisha kwa ajili ya
kufanya ulinganisho kuhusu makadirio ya matumizi ya Serikali kwa mwaka wa
fedha unaofuata.
Aidha, kulingana na matakwa ya kikanuni, Tarehe 28 Machi, 2017 kutakuwa na
Mkutano wa Wabunge wote kwa ajili ya kupokea Mapendekezo ya Serikali kuhusu
Mpango na Kiwango cha Ukomo wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha
2017/2018.
Ratiba zote za Shughuli za Kamati za Bunge ikiwa ni pamoja na maeneo ambayo
kamati hizo zitafanya ziara, vinapatikana katika Tovuti ya Bunge ambayo ni
www.parliament.go.tz.
Imetolewa na:
Kitengo cha Habari, Elimu na Mawasiliano
Ofisi ya Bunge
DODOMA
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...