Watanzania wametakiwa kumuunga mkono Rais John Magufuli kwenye vita ya
kulinda rasilimali za nchi aliyoianzisha kwani kwa muda mrefu watu
wachache walishiriki kufuja mali za nchi ambazo zingetumika kwa
manufaa ya watu wengi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu Mkoani Manyara,
Hudson Starnley Kamoga aliyasema hayo kwenye maadhimisho ya siku ya
albino duniani, ambayo kimkoa ilifanyika kituo cha 4 Angle mji mdogo
wa Haydom, alipokuwa mgeni rasmi kwa niaba ya Mkuu wa mkoa huo Dr Joel
Nkaya Bendera.
Alisema vita ya kulinda rasilimali ya nchi inapaswa kuungwa mkono
kwani utajiri wa nchi ya Tanzania haulingani na hali halisi iliyopo
kutokana na watu wachache kupora utajiri kupitia madini mbalimbali.
Alisema ana imani Rais Magufuli na watanzania kwa ujumla watashinda
vita ya kulinda rasilimali kwani kupitia ripoti ya pili ya makania
imeonyesha namna wananchi wanyonge wanavyoibiwa.
“Pamoja na kuathimisha siku ya albino duniani tunapaswa kumuunga mkono
Rais Magufuli katika vita hii ya kusimamia na kulinda rasilimali za
nchi kupitia madini yetu kwani nia ya dhati ameionyesha,” alisema
Kamoga.
Alisema aliwaagiza watumishi wa halmashauri hiyo waangalie kwenye
runinga na yeye mwenyewe aliiangalia ripoti hiyo kwa lengo la kumuunga
mkono Rais Magufuli katika kusimamia rasilimali zilizopo kwenye eneo
hilo.
"Ukiisikiliza kwa makini hiyo taarifa ya pili ya makinikia na sisi
ambao tunafanya kazi ya kumsaidia Rais kutimiza ndoto yake ya
kuhakikisha kuwa wananchi wanyonge wanafaidika na rasilimali
waliyonayo unaweza ukalia kwa sababu hali iliyopo ni tofauti na
uhalisia," alisema Kamoga.
Alisema wananchi na viongozi wanapaswa kuunga mkono jitihada za Rais
Magufuli na endapo dhamira ya dhati itakuwepo kwa wote rasilimali za
nchi zitawanufaisha wananchi wote.
Naye, Mwenyekiti wa chama cha maalbino mkoani Manyara, Joseph Masasi
alisema wanakabiliwa na changamoto ya kutobaini idadi kamili ya watu
wenye ualbino mkoani humo hivyo kukosa takwimu sahihi.
Masasi alisema tatizo hilo linasababisha hata kukitokea tatizo lolote
linalohitaji msaada kwao inakuwa vigumu kwani wengine wanakosa
kutokana na kutobainishwa kwa idadi yao katika wilaya za mkoa huo.
Alisema pia wanakabiliwa na tatizo la ukosefu wa mafuta maalum ya
kujipaka kwa watu wenye ualbino yanayowasaidia kila siku ili
wasiathiriwe na mionzi ya jua na kusababisha baadhi yao kuathirika.
“Pamoja na hayo tunashukuru kwenye mkoa wa Manyara hakuna matukio ya
watu wenye ualbino kuuawa au kukatwa viungo na watu makatili ila kuna
badhi ya matishio madogo madogo,” alisema Masasi.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya hiyo Joseph
Mandoo alisema halmashauri yao itaendelea kushirikiana na uongozi wa
ualbino kwa ajili ya kuhakikisha wanatoa msaada unaohitajika kwa watu
hao.
Mandoo alitoa wito kwa wazazi na walezi wenye watoto wenye ualbino
kutowafisha ndani na badala yake wawafikishe kwenye sehemu husika ili
pindi misaada itakapotolewa waweze kupatiwa.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu Mkoani Manyara, Hudson Starnley Kamoga, akiwa na viongozi mbalimbali kwenye picha ya pamoja na watu wenye ulemavu wa ngozi (albino) katika maadhimisho ya siku ya albino duniani ambayo kimkoa ilifanyika Mji mdogo wa Haydom wilayani Mbulu.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...