Toka tarehe  17 hadi 20 Oktoba, Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Marekani la Maendeleo ya Kimataifa (USAID) Andy Karas alifanya ziara mkoani Morogoro ili kujionea matokeo ya programu mbalimbali zinazoendeshwa na USAID mkoani humo pamoja na kufanya mazungumzo na wabia na walengwa wa programu hizo. 
Ziara hii inaakisi wigo mpana wa miradi inayofadhiliwa na Marekani nchini Tanzania, ikijumuisha sekta za kilimo, lishe, elimu, afya, wanawake na vijana na utawala bora. 
Kwa muda mrefu, mkoa wa Morogoro umekuwa mlengwa wa msaada wa maendeleo wa Serikali ya Marekani kutokana na fursa yake kubwa ya kilimo, taasisi za kielimu na kuwa katika eneo zuri la kimkakati lililo karibu na miundombinu ya usafirishaji. 
Mkoani humo ndipo ilipo mojawapo ya programu za kwanza kabisa kufadhiliwa na USAID nchini Tanzania – ambayo ni uanzishwaji wa Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine.  
Akiwa chuoni hapo, Mkurugenzi Mkazi Karas alitembelea maabara mpya ya TEHAMA iliyofadhiliwa na USAID  na kukutana na wanafunzi wa Shahada ya Uzamili walionufaika kutokana na mradi wa utafiti wa kilimo ujulikanao kama Innovative Agricultural Research Initiative -iAGRI, uliokuwa ukifadhiliwa na USAID. 
Ziara hiyo iliangazia msaada unaotolewa na USAID kwa shule, vituo vya afya, mradi wa kilimo cha umwagiliaji wa Dakawa na ushirika wa wakulima 950 wanaonufaika nao. Hali kadhalika, ziara ilihusisha miradi ya kijamii ya lishe na ile ya kuboresha utoaji huduma katika sekta ya umma na mamlaka za serikali za mitaa.  
Aidha, Mkurugenzi Mkazi Karas alikutana na viongozi wa serikali mkoani humo pamoja na washiriki wa programu nyingine zinazofadhiliwa na Serikali ya Marekani ikiwa ni pamoja na Wafanyakazi wa Kujitolea wa Peace Corps na wahitimu wa mpango wa kuwaendeleza vijana wa Kiafrika katika uongozi uitwao Young African Leaders Initiative (YALI).
Mkurugenzi Mkazi Andy Karas alijiunga na USAID/Tanzania mwezi Agosti 2017. Amewahi kufanyakazi na USAID katika nchi za Rwanda, Afghanistan, Djibouti, Ghana na Ofisi ya Kanda ya Afrika Mashariki jijini Nairobi.
Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Marekani la Maendeleo ya Kimataifa (USAID) Andy Karas akiwa na wanafunzi wa Shule ya Msingi Dumila wakati alipofanya ziara mkoani Morogoro ili kujionea matokeo ya programu mbalimbali zinazoendeshwa na USAID mkoani humo hivi karibuni.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...