Na Hamza Temba - WMU
SERIKALI imesema imedhamiria kufungua utalii wa Kanda ya Kusini
ili kupanua wigo wa vivutio vya utalii nchini na hatimaye kuongeza idadi ya
watalii na kipato kwa Serikali na jamii kwa ujumla.
Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii,
Japhet Hasunga katika kijiji cha Kapozwa Wilaya ya Kalambo Mkoani Rukwa wakati
wa ziara yake ya siku moja ya kutembelea Maporomoko ya Mto Kalambo ambayo ni ya
pili kwa kina kirefu barani Afrika baada ya Maporomoko ya Tugela yaiyopo nchini
Afrika ya Kusini.
Alisema kwa sasa vivutio vingi vinavyotumika kwa utalii nchini
ni vile vya ukanda wa Kaskazini hususan vya wanyamapori ambavyo vimeanza
kuelemewa kutokana na watalii wengi kutembelea ukanda huo zaidi kuliko Kanda ya
Kusini ambayo pia ina vivutio mbalimbali vya asili.
Alisema Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa
maendeleo ikiwemo benki ya Dunia kupitia mradi wa REGROW imepanga kuboresha
miundombinu ya vivutio vya utalii vya Kanda ya Kusini na kuvitangaza ili
kuimarisha sekta hiyo muhimu ambayo inachangia asilimia 25 ya mapato yote ya
kigeni na asilimia 17.5 ya pato la taifa.
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga (kushoto) akiteta
jambo na Katibu Tawala Wilaya ya Kalambo Frank Schalwe wakati akishuka kwenye
ngazi maalum zinazojengwa kwa ajili ya kuwawezesha watalii kushuka hadi kwenye
kina cha Maporomoko ya Mto Kalambo wakati wa ziara yake mkoani Rukwa. Maporomoko hayo ambayo ni ya pili kwa kina kirefu barani Afrika baada
ya TUGELA yaliyopo Afrika ya Kusini yana kina cha mita 235 na upana kati ya
mita 3.6 hadi 18.
Muonekano wa ngazi hizo kuelekea kwenye Maporomoko ya Mto Kalambo.
Sehemu ya juu ya Maporomoko ya Mto Kalambo.
Taswira ya maporomoko ya mto Kalambo kutokea angani (Picha hii ni kwa hisani ya Mtandao)
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...