Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein akizungumza Mtawala wa Ras-Al-Khaimah Mtukufu Sheikh Saud Bin Saqr Al Qasimi na kufanya nae mazungumzo yaliolenga kuendeleza uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo baina ya pande mbili hizo.
Mazungumzo hayo yaliofanyika katika makaazi ya Sheikh Saud Bin Saqr Al Qasimi mjini Ras-Al-Khaimah, ambapo viongozi hao kwa pamoja walieleza haja ya kuendeleza uhusiano na kuimarisha mashirikiano katika kuinua sekta za maendeleo ikiwemo sekta ya mafuta na gesi asilia.
Aidha, viongozi hao walizungumza juu ya hatua zinazoendelea katika suala zima la utafiti wa mafuta na gesi asilia ambapo katika mazungumzo hayo walieleza haja ya kuimarisha zaidi ushirikiano wa pamoja ili kufikia lengo la kuipaisha Zanzibar kiuchumi na kimaendeleo.
Katika maelezo yake, Dk. Shein alitoa shukrani kwa kiongozi huyo kutokana na juhudi zake za kuendelea kuiunga mkono Zanzibar na kumpongeza kiongozi huyo kwa mafanikio yaliopatikana nchini humo katika kipindi kifupi.
Rais Dk. Shein alimueleza kiongozi huyo kuwa Zanzibar ina mengi ya kujifunza kutoka kwa ndugu zao wa Ras Al Khaimah na iko tayari kupanua wigo wa maendeleo kutoka nchini humo kwani inatambua mafanikio yaliopatikana kutokana na mikakati iliyowekwa.
Pamoja na hayo, viongozi hao kwa pamoja walizungumzia hatua zaidi zinazohitajika katika kuimarisha ushirikiano kati ya Zanzibar na Ras Al Khaimah katika sekta za maendeleo ikiwa ni pamoja na kupanga mipango madhubuti katika malengo yaliokusudiwa ya hapo baadae.
Nae Kiongozi huyo alieleza kuwa Ras Al Khaimah itaendeleza uhusiano na ushirikiano wake na Zanzibar hasa katika sekta hizo za maendeleo na kusisitiza kuwa uhusiano na ushirikiano huo utaletea maendeleo makubwa Zanzibar hasa kwa kutambua kuwa jambo hilo limo kwenye dhati ya moyo wake.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...