Na Karama Kenyunko, Glogu ya Jamii.
MWANAJESHI MT Private Ramadhan Mlaku (28) amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akiwa juu ya kitanda cha wagonjwa kujibu tuhuma za mauaji ya askari mwenzake MT 79512 SGT Saimon Munyama.
Mshtakiwa huyo amefikishwa mahakamani hapo leo, saa tano asubuhi akiwa na katika gari la kubebea wagonjwa ambapo alikaa kwenye gari hilo kwa takribani saa moja hadi pale ilipotimu saa sita mchana akashushwa akiwa ndani ya gari akiwa amebebwa kwenye kitanda cha wagonjwa na kupelekwa katika chumba cha Mawakili wa Serikali ambapo alisomewa shtaka lake la mauaji linalomkabili.
Akisomewa shtaka na Wakili wa Serikali, Mosii Kaima mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu,Thomas Simba imedaiwa Oktoba 30, mwaka jana mshtakiwa Mlaku ambaye ni Mwanajeshi wa Kambi ya Jeshi la Makongo, akiwa Makao Mkuu ya JWTZ Upanga Ilala Dar es Salaam alimuua askari mwenzie MT 79512 SGT Munyama.
Hata hivyo, mshtakiwa hakuruhusiwa kujibu kitu chochote mahakamani hapo kwa sababu Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu haina mamlaka ya kuisikiliza kesi za mauaji ambazo kwa kawaida zinasikilizwa Mahakama kuu.
Aidha mshtakiwa amerudishwa rumande kwa kuwa kosa la mauaji linalomkabili halina dhamana kwa mujibu wa sheria.Kwa mujibu wa upande wa mashtaka upelelezi katika kesi hiyo bado haujakamilika huku Hakimu Simba akiutaka upande wa mashtaka kujitahidi kukamilisha upelelezi wa kesi hiyo mapema.
Kesi imeahirishwa hadi Machi 28, mwaka huu kwa ajili ya kutajwa.
Baada ya kusomewa shtaka lake, mshtakiwa huyo alipandishwa tena katika gari la Jeshi la wagonjwa ambalo lilimleta mahakamani hapo kwa ajili ya kupelekwa mahabusu.


Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...