Na Grace Michael, Morogoro

 KATIKA kuhakikisha Watanzania wanakuwa na uhakika wa kupata huduma za matibabu kupitia Mfumo wa Bima ya Afya, Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya umekutana na waratibu wake kutoka halmashauri zote nchini kwa lengo la kujipanga kuwafikia wananchi wengi zaidi pamoja na uboreshaji wa huduma kwa wanachama. 

Akifungua kikao kazi hicho cha siku mbili, Mkurugenzi Mkuu wa NHIF, Bernard Konga alisema kuwa ili kutimiza azma ya Serikali ya Awamu ya Tano ya Serikali ya Viwanda ni lazima Mfuko kwa kushirikiana na wadau wake kuhakikisha wananchi wengi zaidi wanafikiwa kwa kujiunga na Mfuko ili kuwa na uhakika wa huduma za matibabu. 

“Ili kufikia lengo la Nchi ya Viwanda ambalo Rais wetu amelianzisha, ni lazima tuhakikishe wananchi wote wanakuwa na uhakika wa kupata huduma za matibabu wakati wanapopatwa na magonjwa na ndio maana tumeamua kabisa tukutane kwa pamoja ili tukubaliane namna bora ya kuwafikia lakini pia kuboresha na kuimarisha huduma za matibabu katika vituo vya kutolea huduma,” alisema Bw. Konga. 

Kikao hicho pia kina lengo la kupata mrejesho wa pande zote mbili kuhusu maboresho mbalimbali yaliyofanyika ndani ya Mfuko na kujadili kwa pamoja mambo yanayohitaji kuboreshwa kwa lengo la kuongeza wigo na kutoa huduma bora. Mkurugenzi Mkuu pia alisisitiza juu ya kukabiliana na tatizo la udanganyifu ambalo limekuwa likifanywa na baadhi ya watoa huduma wasiokuwa waaminifu hali inayorudisha nyuma jitihada kubwa za Mfuko za kuimarisha Mfuko. 

Alisema kuwa kwa upande wa Mfuko, umeanzisha mifumo mbalimbali ya TEHAMA ambayo inatumika katika kubana mianya ya udanganyifu kwenye utumiaji wa huduma na uwasilishaji wa madai ya watoa huduma hivyo akawaomba waratibu hao kutoa ushirikiano mkubwa katika suala hili kwa lengo la kulinda uhai wa Mfuko. 

Kwa upande wa waratibu wamesema kuwa mkutano huo ni fursa kubwa kwao kupata taarifa mbalimbali za maboresho yaliyofanywa na kujengeana uwezo wa ushawishi kwa wananchi kujiunga na huduma za Mfuko.
 Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), Bw. Bernad Konga akifungua kikao kazi kilichohusisha Waratibu wa Mfuko kutoka Halmashauri zote nchini mjini Morogoro.
  Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko Bw. Bernard Konga akifuatilia mada zilizokuwa zinawasilishwa katikati ni Meneja wa NHIF, Mkoa wa Morogoro Bi. Agnes Chaki na Kushoto ni Mkurugenzi wa 
Utawala na Rasilimali Watu Bw. Charles Lengeju.
 Waratibu wa Mfuko wakifuatilia mada mbalimbali kutoka kwa wawezeshaji

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...