Kamati ya Utendaji ya Chama cha Soka mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) iliketi Machi 25, 2018 katika kikao cha kawaida kinachofanyika kila baada ya miezi mitatu kujadili masuala mbalimbali ya kiutendaji.

Miongoni mwa masuala yaliyojadiliwa katika kikao hicho ni kama yafuatayo:

1. KUZINDULIWA KWA MPANGO MKAKATI (Stategic Plan) WA MIAKA MINNE

Mara baada ya Uongozi huu wa DRFA kuingia madarakani uliazimia kuandaa mpango mkakati wa miaka minne ambao ulibuniwa ili kuepuka kuendesha chama bila mipango iliyoainishwa kabla. Mpango huo utakaozinduliwa siku moja kabla ya mkutano mkuu wa DRFA.

2. MAANDALIZI YA MKUTANO MKUU

Mkutano mkuu wa DRFA umepangwa kufanyika kabla ya mwezi wa sita huku jukumu la kupanga mahali na tarehe maalum likiachwa kwa Sekretarieti ambayo itatangaza hivi karibuni. Mkutano huu ni wakikatiba na wajumbe wake wametajwa kwenye katiba, kwa maana viongozi wa wilaya na vingozi wa vyama shiriki.

3. MAANDALIZI YA MAFUNZO YA UTAWALA NA USIMAMIZI WA SOKA

Baada ya kufanikiwa katika kozi ya kwanza ya makocha wa soka la vijana iliyomalizika mwanzoni mwa mwezi huu, DRFA inaandaa kozi nyingine awamu hii ikigeukia upande wa uongozi wa klabu na vyama vya soka. Lengo la kozi hii ni kuwaongezea uwezo na utaalam viongozi wa soka mkoani Dar es Salaam ili kuhakikisha klabu na vyama vya soka vinaongozwa na watu wenye weledi kwa manufaa ya soka la mkoa huu na taifa kwa ujumla. Hii itafanyika Aprili katika tarehe itakayotangazwa na sekretarieti hivi karibuni. Kozi hiyo itafuatiwa na nyingine ya waamuzi ambayo ina lengo la kuongeza idadi ya waamuzi wenye uwezo mkubwa mkoani Dar es Salaam.

4. MWENENDO WA LIGI YA MKOA

Ligi ya mkoa inaendelea vizuri katika hali ya utulivu bila kuwa na malalamiko mengi toka kwa klabu. Hii imetokana na usimamizi kabambe uliowekwa na DRFA katika vituo vyote ili kuhakikisha sheria 17 za soka zinafuatwa wakati wote. Ni imani ya DRFA kwamba usimamizi huo utapelekea kupatikana kwa wawakilishi watatu watakaokwenda kuonyesha ushindani wa kweli kwenye ligi daraja la pili ngazi ya Taifa. Ligi hiyo yenye makundi matatu inatarajiwa kumalizika Machi 30 huku mechi zake zikichezwa kila siku katika viwanja vitano tofauti.

5. UGENI TOKA ZANZIBAR

Kuna uhusiano mkubwa uliodumu kwa miaka mingi kati ya DRFA na chama cha soka mkoa wa Mjini Magharibi ambapo kila mwezi wa nne vyama hivi hutembeleana kwa zamu kwa ajili ya kujadili na kupeana ushauri wa masuala mbalimbali yahusuyo maendeleo ya soka. Mwaka huu DRFA itatembelewa na ndugu zetu wa Zanzibar hivyo kamati hiyo imeandaa utaratibu wa mapokezi ya maafisa wa chama hicho watakaokuja ikiwa ni pamoja na mchakato mzima wa uwepo wao hapa jijini Dar es Salaam.

6. MAANDALIZI YA LIGI YA MKOA YA VIJANA (U15) IJULIKANAYO KAMA NDONDO ACADEMY

Baada kuzalisha makocha 25 wa soka la vijana katika kozi iliyomalizika Machi 10, DRFA iliwaagiza kwenda kuitumia elimu waliyoipata kwa kufundisha vijana kwenye vituo mbalimbali kukuza soka la vijana (Academy). Michuano ya Ndondo Academy si tu imeandaliwa kwa ajili ya kuibua vipaji vipya, bali pia ni katika kupata mwendelezo bora wa progaramu ya maendeleo ya soka la vijana iliyoanza kwa mafunzo ya ukocha. Ligi hii itasimamiwa kwa pamoja na Kamati ya Soka la Vijana na Kamati ya Mashindano ya DRFA.

7. MAANDALIZI YA LIGI YA MKOA YA WANAWAKE CHINI YA MIAKA 15 (U15) 

Kamati ya Utendaji ya DRFA imegundua kwamba idadi ya wasichana walio na utayari wa kuchezo soka imepungua na kwamba hakuna chanzo maalum cha kuzalisha wachezaji wapya. Kwa kuliona hilo DRFA imeamua kufungua 'kiwanda' cha nyota wapya wa soka la wanawake kwa kuanzisha ligi ya vijana, ligi itakayosimamiwa na Chama cha Soka la Wanawake, Kamati ya Soka la Vijana na Kamati ya Mashindano ya DRFA.

Ahsante
Karim Boimanda
Afisa Habari na Mawasiliano
DRFA

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...