Baraza la Uuguzi na Ukunga Tanzania (TNMC) limewakuta na hatia na kuwapa karipio kali la maandishi Wauguzi Wakunga sita katika Hospitali ya Mkoa wa Morogoro kwa kushindwa kutimiza majukumu yao ya kitaaluma wakati wakitoa huduma kwa mgonjwa.
Katika kikao chake cha 193 kilichofanyika tarehe 28 Juni, 2018 katika Ofisi za Baraza hilo zilizopo Kibaha, Mkoani Pwani, chini ya Mwenyekiti wa Baraza la Uuguzi na Ukunga Tanzania, Bw. Abner Mathube, lilisikiliza shauri la ukwiukwaji wa maadili ya kazi lililotokea katika Hospitali ya Mkoa wa Morogoro ambapo mama mjamzito alilalamika kutokupatiwa huduma stahiki alipowasili hospitalini hapo hali iliyosababisha mama kukosa mtoto.
Pamoja na karipio hilo, Wauguzi Wakunga wameonywa kuwa endapo watarudia kosa hilo, Baraza la Wauguzi na Ukunga Tanzania, halitasita kuwachukulia hatua kali zaidi za ikiwemo kuwafutia usajili.
Akizungumza na wanahabari, Msajili wa TNMC Bi. Agnes Mtawa amesema katika kikao hicho, Baraza limejadili suala la baadhi ya watu wanaogushi vyeti na leseni za taaluma ya uuguzi na ukunga ambapo limebaini kuwa katika robo mwaka Aprili-Juni, 2018 watu watano walitambuliwa kugushi vyeti na leseni hivyo wamepelekwa kwenye vyombo vya dola ili hatua stahiki za kisheria ziweze kuchukuliwa dhidi yao.
Aidha, Baraza limewabaini watu 15 wanaojitambulisha kuwa ni wauguzi lakini kanzi data ya Baraza hilo imeonesha kuwa vyeti hivyo siyo halali na leseni wanazotumia ni za kugushi. Kwakuwa watu hawa wapo mikoa mbalimbali hapa nchini Baraza linawataka kujisalimisha mara moja kabla halijawafuata huko waliko.
Baraza linatoa onyo kali na kuwataka watu wanao ghushi vyeti na leseni za kitaaluma ya Uuguzi na Ukunga kuacha kuacha tabia hiyo mara moja kwani hatua kazi zitachukuliwa dhidi yao ikiwemo kufikishwa kwenye vyombo vya dola.
Katikati ni Mwenyekiti wa Baraza la Uuguzi na Ukunga Tanzania (TNMC) Bw. Abner Mathube akiongoza kikao cha baraza hilo, Kibaha Mkoani Pwani. Kushoto kwake ni Msajili wa Bazara Bi. Agnes Mtawa
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...