Na Veronica Simba – Dodoma
Mtaalam Mwelekezi aliyeingia Mkataba na Serikali kupitia Shirika la
Umeme Tanzania (TANESCO), kufanya Tathmini ya Mazingira (EIA) katika
Mradi wa kuzalisha umeme kwa kutumia nguvu ya maji ya Mto Rufiji
Profesa Raphael Mwalyosi, amesema kuwa athari za kimazingira
zilizobainika kuweza kutokea, zinaweza kuzuilika.
Ameyasema hayo leo, Juni 11, 2018 wakati akiwasilisha Tathmini hiyo ya
Mazingira kwa Makatibu Wakuu wa Wizara mbalimbali zenye majukumu ya
kutekeleza miundombinu wezeshi ya Mradi husika.
“Tathmini yetu imebainisha kuwa Mradi husika unaweza kutekelezwa
pasipo shaka yoyote kwani athari zake kimazingira zinaweza kuzuilika.
Muhimu ni kuweka mikakati ya kuzizuia,” alifafanua.
Uwasilishwaji wa Tathmini ya Mazingira kwa Kamati hiyo Tendaji,
umefanyika Makao Makuu ya Wizara ya Nishati jijini Dodoma, ambapo ni
moja ya hatua muhimu zinazoendelea kufanyika kabla ya kuanza rasmi
utekelezaji wa Mradi huo.
Wajumbe walioshiriki katika zoezi la uwasilishwaji wa Tathmini husika ni
Makatibu Wakuu kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya
Makazi; Maliasili na Utalii; Mambo ya Ndani ya Nchi, Mambo ya Nje na
Ushirikiano wa Afrika Mashariki; Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo;
Kilimo; Mifugo na Uvuvi pamoja na Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.
Nyingine ni Wizara ya Fedha na Mipango; Ofisi ya Makamu wa Rais –
Mazingira; Ofisi ya Waziri Mkuu; Wizara ya Madini pamoja na Wizara ya
Nishati, ambayo ndiyo yenye dhamana.
Aidha, wadau wengine walioshiriki ni Msemaji Mkuu wa Serikali ambaye
pia ni Mkurugenzi wa Idara ya Habari (MAELEZO), Wakuu wa Taasisi za
Mamlaka ya Wanyamapori Tanzania (TAWA), Wakala wa Barabara
Tanzania (Tanroads) na TANESCO.
Makatibu Wakuu wa Wizara mbalimbali zenye majukumu ya kutekeleza
miundombinu wezeshi ya Mradi wa kuzalisha umeme kwa kutumia nguvu
ya maji ya Mto Rufiji, wakimsikiliza Mtaalam Mwelekezi, Prof Raphael
Mwalyosi (aliyesimama), alipokuwa akiwasilisha Tathmini ya Mazingira ya
Mradi husika, Juni 11, 2018 Dodoma.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Dkt. Hamisi Mwinyimvua (kulia) na
Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Prof Simon Msanjila, wakifuatilia
uwasilishwaji wa Tathmini ya Mazingira ya Mradi wa kuzalisha umeme kwa
kutumia nguvu ya maji ya Mto Rufiji, Juni 11, 2018 Dodoma.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...