Na
Veronica Simba – Dodoma
Ujumbe kutoka Kampuni
ya ORASCOM ya Misri, wamemtembelea Waziri wa Nishati Dkt. Medard Kalemani na
kuzungumza naye kuhusu nia yao ya kuwekeza katika miradi ya kuzalisha umeme kwa
kutumia makaa ya mawe pamoja na maporomoko ya maji.
Mazungumzo hayo
yalifanyika Juni 19, 2018 Makao Makuu ya Wizara, jijini Dodoma na
kuwashirikisha pia Kamishna wa Nishati na Masuala ya Petroli, Mhandisi Innocent
Luoga pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO),
Dkt. Tito Mwinuka.
Wakizungumzia uwezo
wao katika kutekeleza nia waliyowasilisha, Mkurugenzi wa kampuni hiyo Bw. Maher Salem alieleza kuwa wao wana uzoefu wa miaka
mingi katika kazi hiyo na kwamba wanatumia teknolojia ya kisasa. Pia, waliongeza
kuwa wanazo fedha za kutosha kuweza kutekeleza miradi husika.
Aidha, waliutaja
Mradi wa kuzalisha umeme kwa kutumia makaa ya mawe wa Kiwira wenye megawati 200
pamoja na Ruhudji wenye megawati 358, kuwa ndiyo hasa ambayo wangependa
kuwekeza.
Waziri Kalemani
aliyapokea mapendekezo ya Kampuni hiyo na kuwataka waendelee kufanya majadiliano
na Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) pamoja na TANESCO kuhusu uwekezaji huo,
wakati Serikali ikikamilisha utaratibu wa kuitangaza miradi husika.
Hata hivyo, Waziri
alieleza bayana kuwa, Kampuni hiyo itatakiwa kushiriki katika ushindani na
wawekezaji wengine wenye nia ya kuwekeza katika miradi husika, baada ya miradi
hiyo kutangazwa rasmi.
Dkt. Kalemani
aliishukuru Kampuni ya ORASCOM kwa kuonesha nia ya kuwekeza Tanzania na
aliwahakikishia kuwa Serikali itawapa ushirikiano stahiki.
Waziri wa Nishati
Dkt. Medard Kalemani (katikati), akizungumza na Ujumbe kutoka Kampuni ya
ORASCOM ya Misri (kulia), waliofika ofisini kwake Dodoma, Juni 19 2018 na
kuwasilisha nia ya kuwekeza katika miradi ya kuzalisha umeme nchini. Kushoto ni
Kamishna wa Nishati na Masuala ya Petroli, Mhandisi Innocent Luoga na
Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Dkt. Tito Mwinuka.
Mkurugenzi wa Kampuni ya ORASCOM ya Misri Bw. Maher Salem akimkabidhi Waziri wa Nishati Dkt. Medard
Kalemani, Kabrasha lenye maombi ya kuwekeza katika miradi ya umeme nchini.
Ujumbe kutoka Kampuni hiyo ulimtembelea Waziri ofisini kwake jijini Dodoma,
Juni 19, 2018.
Waziri wa Nishati
Dkt. Medard Kalemani (wa tatu kutoka kulia), akiwa katika picha ya pamoja na
Ujumbe kutoka Kampuni ya ORASCOM ya Misri, waliofika ofisini kwake Dodoma, Juni
19, 2018 na kuwasilisha nia ya kuwekeza katika miradi ya umeme nchini. Wengine
pichani ni Kamishna wa Nishati na Masuala ya Petroli, Mhandisi Innocent Luoga (wa
kwanza kushoto) na Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Dkt. Tito Mwinuka (wa tatu
kutoka kushoto).
Waziri wa Nishati
Dkt. Medard Kalemani, akiagana na Bw. Maher Selim ambaye ni kiongozi wa ujumbe na Mkurugenzi wa Kampuni ya ORASCOM ya Misri,
waliofika ofisini kwake Dodoma, Juni 19, 2018 na kuwasilisha nia ya kuwekeza
katika miradi ya umeme nchini.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...