Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola akizungumza na wananchi wa Wilaya ya Kakonko, Mkoani Kigoma wakati alipofanya ziara ya kikazi wilayani humo jana kwa ajili ya kusikiliza kero mbalimbali zinazowakabili wananchi pamoja na Taasisi zilizopo ndani Wizara yake. Lugola aliwataka wananchi hao wawe huru na nchi yao na kuwaruhusu wakulima wilayani humo kulima katika maeneo ya jirani ya Kambi ya Mtendeli ambapo hapo awali walizuiwa kulima katika maeneo hayo bila ya kua na kibali cha ruhusa.

Na Felix Mwagara, MOHA-Kakonko

WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola amewataka wananchi wa Kakonko wanaolima jirani na Kambi ya Wakimbizi ya Mtendeli, pamoja na kambi zingine zote zilizopo mkoani Kigoma waendelee kulima bila kuomba kibali chochote kama ilivyoagizwa awali.

Waziri Lugola amefuta utaratibu huo wa utoaji wa vibali kwa ajili ya kuruhusiwa kwenda kulima katika maeneo hayo, baada ya wananchi wilayani humo kuulalamikia utaratibu huo ambao walisema unawafanya wasiwe huru na unawachelewesha kuendeleza shughuli zao za kilimo kama ilivyokua awali.

Akizungumza katika mkutano wa hadhara uliohudhuriwa na mamia ya wananchi mjini Kakonko, Mkoani Kigoma, jana, Lugola alisema Serikali ya Awamu ya Tano haitaki wananchi wake wanyanyaswe, wananchi wanapaswa kua huru katika nchi yao.

“Naagizia huu utaratibu ufutwe na wananchi wawe huru kwenda kulima katika maeneo ambayo yapo jirani na hiyo kambi pamoja na kambi zinginezo, na pia wasisumbuliwe na mtu yeyote, ” alisema Lugola.

Pia Waziri Lugola alielekeza baadhi ya wananchi ambao hawajalipwa fidia wakati mashamba yao yalipochukuliwa kwa ajili ya kuanzisha kambi hiyo wafanyiwe uhakiki ili waweze kulipwa haki zao.

Hata hivyo, Mratibu wa Idara ya Wakimbizi Kanda ya Kigoma, Tony Laiser ambaye alikuwepo katika mkutano huo alipokea maagizo hiyo na kuahidi kuyatekeleza. Aidha, kabla ya mkutano huo wa hadhara, Waziri Lugola alizungumza na watendaji waliopo katika wizara yake mkoani humo na alisema Serikali imepeleka mafunzoni vijana 1,500 kwaajili ya kujiunga na Jeshi la polisi pamoja na kuagiza magari kwa ajili doria.

Pia aliwataka watendaji hao kufanya kazi kwa bidii kwani serikali yao ipo na inawajali na pia itahakikisha inatatua kero zao ambazo zinawakabili ikiwemo ukosefu wa majengo, upungufu wa vitendea kazi na uhaba wa askari katika sehemu mbalimbali nchini.
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola (kushoto) akiandika malalamiko ya mwananchi wa Mji mdogo wa Kakonko, Mkoani Kigoma, Emili Geofrey, alipokua anatoa kero mbalimbali zinazowakabili ndani ya Wilaya yao. Akizungumza na wananchi hao mjini humo jana, Lugola aliwaruhusu wakulima wilayani humo kulima katika maeneo ya jirani ya Kambi ya Mtendeli ambapo hapo awali walizuiwa kulima katika maeneo hayo bila ya kua na kibali cha ruhusa.
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola, akimuuliza maswali Mratibu wa Idara ya Wakimbizi Kanda ya Kigoma, Tony Laiser (kulia-aliyesimama), baada ya baadhi ya wananchi wa Wilaya ya Kakonko kumlalamikia Waziri huyo kuhusu kuzuiwa kulima katika maeneo jirani ya Kambi ya Wakimbizi ya Mtendeli iliyopo wilayani humo, Mkoa wa Kigoma. Hata hivyo, Lugola aliwaruhusu wakulima hao kuendelea na shughuli za kilimo bila ya kuwa na kibali cha ruhusa kama walivyoelekezwa awali.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...