NA WAMJW-DODOMA
Halmashauri za Miji, Majiji, Wilaya, Vitongoji na Vijiji zilizofanya vibaya katika mashindano ya afya na usafi wa mazingira zimetakiwa kujitathmini na kuhakikisha zinaweka mikakati madhubuti ya utunzaji wa mazingira.
Hayo yamesemwa jana na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu wakati wa kilele cha wiki ya usafi wa mazingira ulioenda sambamba na mkutano uliojumuisha Maafisa Afya nchini na Wadau mbalimbali wa maendeleo kilichofanyika jijini Dodoma.
Waziri Ummy alisema hayo wakati akitaja washindi waliofanya vizuri katika Halmashauri za Miji, Majiji, Wilaya, Vitongoji na Vijiji viliyofanya vizuri katika mashindano ya afya na usafi wa mazingira ambayo Wizara imekuwa ikitekeleza tangu mwaka 1988.
“Mashindano hayo huanza katika ngazi ya Kitongoji na kuhitimishwa kwa kupata washindi wa kitaifa. Kila mwaka tumekuwa tukiboresha mashindano haya ambapo kwa mwaka huu tumeongeza makundi manne kutoka sita ya awali. Makundi yalioongezeka ni; Hospitali za Rufaa za Binafsi, Shule za Msingi za Vijijini, Shule za Sekondari za Bweni za Serikali, na Shule za Sekondari za Bweni za Binafsi”. Alisema Waziri Ummy.
Aidha, waziri huyo alitaja makundi ya washindi waliofanya vizuri na makundi ya Halmashauri, Majiji na Mikoa iliyofanya vibaya.
Katika kundi la Halmashauri za Manispaa na Majiji lilihusisha Manispaa 25, ambapo Halmashauri ya Manispaa ya Iringa ilikua kinara kwa asilimia 92.7, ikifuatiwa na mshindi wa pili Halmashauri ya Jiji la Arusha asilimia 90.5 na mshindi wa tatu ikiwa ni Halmashauri ya Manispaa ya Moshi kwa asilimia 89.7.
Kundi la pili lilikua la Halmashauri za Miji ambapo lilihusisha Halmashauri za miji 22 nchini. Mshindi wa kwanza ni Halmasahuri ya mji wa Njombe asilimia 93.4, Halmashauri ya Mji wa Kahama ikishika nafasi ya pili kwa asilimia 75.0 na Halmashauri ya Mji wa Tunduma ikiwa nafasi ya tatu kwa asilimia 73.5.
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu akizungumza wakati wa kilele cha wiki ya usafi wa mazingira ulioenda sambamba na mkutano uliojumuisha Maafisa Afya nchini na Wadau mbalimbali wa maendeleo kilichofanyika jijini Dodoma.Waziri Ummy amezitaka Halmashauri za Miji, Majiji, Wilaya, Vitongoji na Vijiji zilizofanya vibaya katika mashindano ya afya na usafi wa mazingira kujitathmini na kuhakikisha zinaweka mikakati madhubuti ya utunzaji wa mazingira.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...