Na Humphrey Shao, Globu ya Jamii
Wizara ya Fedha na Mipango kupitia
Kitengo cha Kudhibiti Fedha Haramu (FIU) imeendesha warsha kuhusu udhibiti wa utakasishaji wa
fedha haramu na ufadhili wa ugaidi kwa wadau wa sekta ya bima (insurance
sector) na masoko ya mitaji na dhamana(capital markets and securities sector)
kwa lengo la kuendelea kuwakumbusha wadau kuhusu umuhimu wa kuendelea
kutekeleza wajibu wao na kuunga mkono
jitihada za Serikali katika kupambana na uhalifu wa kifedha.
Akizungumza
wakati wa ufunguzi wa warsha ya siku mbili juu ya udhibiti wa utakasishaji wa
fedha haramu na ufadhili wa ugaidi inayofanyika katika ukumbi wa Benki Kuu ya Tanzania,
Kamishna na Mtendaji Mkuu wa Kitengo cha Kudhibiti Fedha Haramu Ndugu Onesmo H.
Makombe anasema warsha hii muhimu ni muendelezo wa warsha kuhusu udhibiti wa
utakasishaji wa fedha haramu na ufadhili wa ugaidi katika sekta ya benki.
Alieleza kuwa tatizo la utakasishaji wa fedha haramu ni tatizo kubwa
ulimwenguni kote na katika jamii kwasababu ya kuwepo kwa vitendo mbalimbali vya
uhalifu vinavyowapatia wahalifu pato haramu. Uhalifu huo ni pamoja na ukwepaji
kodi, biashara haramu ya dawa za kulevya, biashara haramu ya watu, biashara
haramu ya silaha, rushwa, kughushi, ujangili, uharamia, uvunaji haramu wa
magogo, uuzaji wa bidhaa bandia, ujambazi na uporaji.
“pamoja na utakasishaji wa fedha haramu na
ufadhili wa ugaidi, kuendelea kujenga na
kuimarisha mifumo ya udhibiti katika taasisi ili kuzuia uwezekano wa sekta za
bima na masoko ya mitaji na dhamana kutumika na wahalifu kama vyombo vya
kutakasisha fedha haramu na kufadhili vitendo vya ugaidi. Kuendelea kuimarisha
mifumo ya udhibiti katika sekta hizi kutasaidia kulinda mfumo wa fedha wa nchi
yetu ili usitumiwe na wahalifu na watu wasio waaminifu”.
Aidha, aliainisha madhara ya utakasishaji
wa fedha haramu kuwa ni ya kiuchumi, kijamii, kisiasa na kiusalama. Madhara
hayo pamoja na uhalifu kuendelea kushamiri
kwa uhalifu na wahalifu kujiimarisha; wahalifu kuwa na nguvu kiuchumi; kuhatarisha utawala wa sheria na usalama (threaten
peace, stability and rule of law) kwani uhalifu unaposhamiri na makundi ya
uhalifu yanapojiimarisha hupata nguvu na kujaribu kudhibiti kushindana na vyombo vya dola; kuharibu
ushindani (ruin competitiveness) wa kibiashara katika uchumi kutokana na
wahalifu kuwa na mitaji inayotokana na fedha haramu, wafanyabiashara halali
hushindwa kuhimili ushindani; kushusha hadhi ya nchi kimataifa (erosion of
country’s integrity) na kusababisha nchi kutonufaika na mfumo wa fedha wa
kimataifa.
Aidha na kushusha imani ya wawekezaji na
kusababisha uwekezaji kupungua na wawekezaji wapya kutotaka kuwekeza kutokana
na kushamiri kwa uhalifu, wawekezaji huwa na hofu kuwa mitaji na mali zao havitakuwa
salama; imani ya washirika wa maendeleo na jumuiya ya kimataifa hupungua na nchi huathirika kiuchumi; kushuka kwa hadhi ya taasisi za fedha na mfumo mzima wa fedha; na nchi kushindwa kufikia
malengo ya maendeleo kwani rasilimali huwa mikononi
mwa wahalifu wachache badala ya kutumika kutekeleza ajenda pana ya maendeleo ya
nchi.
Kamishna wa Kitengo cha Kudhibiti Fedha Haramu amewaasa na kuwakumbusha
washiriki wa warsha hiyo kuendelea kushirikiana na taasisi mbalimbali kutekeleza
wajibu wao wa kisheria kwa uadilifu na uaminifu ili kuendelea kusaidia
katika kubaini wahalifu wanaoweza kutumia mfumo wa fedha wa nchi kutakasisha
fedha haramu na kufadhili vitendo vya kigaidi na kuhatarisha usalama wa nchi.
Kamishna na Mtendaji Mkuu wa Kitengo cha Kudhibiti Fedha Haramu Ndugu Onesmo H. Makombe Akitoa neno wakati wa ufunguzi wa warsha ya siku mbili juu ya udhibiti wa utakasishaji wa fedha haramu na ufadhili wa ugaidi inayofanyika katika ukumbi wa Benki Kuu ya Tanzania Jijini Dar es Salaam,
Kamishna Msaidizi Huduma za Kompyuta kitengo cha kudhibiti fedha haramu(FIU),Gilbert Nyombi akitoa mada juu ya udhibiti wa utakasishaji wa fedha haramu na ufadhili wa ugaidi inayofanyika katika ukumbi wa Benki Kuu ya Tanzania,
Mmoja ya Washiriki wa Warsha hiyo Floransia Mrema akichangia jambo wakati wa Warsha hiyo.
Washiriki wa Warsha hiyo wakimsikiliza kamishna wakati wa ufunguzi wa warsha ya siku mbili juu ya udhibiti wa utakasishaji wa fedha haramu na ufadhili wa ugaidi inayofanyika katika ukumbi wa Benki Kuu ya Tanzania,
Kamishna na Mtendaji Mkuu wa Kitengo cha Kudhibiti Fedha Haramu Ndugu Onesmo H. Makombe, akiwa katika picha ya pamoja na wadau wa sekta ya Bima na Masoko ya Mitaji ya Dhamana, katika Ukumbi wa Benki Kuu ya Tanzania(BOT), Jijini Dar es Salaam
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...