Na Zainab Nyamka, Globu ya Jamii

KOCHA wa muda wa Azam FC, Idd Nassor Cheche, amefunguka kuwa jambo kubwa linalombeba kila akikabidhiwa timu hiyo, ni kutokana na kuifahamu vema na kutopenda masikhara.

Cheche anayesaidiana na Meja Mstaafu, Abdul Mingange, wote wakiwa makocha wa timu za vijana za Azam FC, wameshika nafasi hizo kwa muda baada ya kusitishiwa mikataba kwa Hans Van Der Pluijm na Msaidizi wake, Juma Mwambusi.

Wawili hao waliiongoza Azam FC jana usiku kuichapa Rhino Rangers mabao 3-0 na kutinga robo fainali ya michuano ya Kombe la Shirikisho (Azam Sports Federation Cup), mabao yakiwekwa kimiani na kiungo mshambuliaji Tafadzwa Kutinyu, kiungo Salum Abubakar ‘Sure Boy’ na mshambuliaji Obrey Chirwa.

Cheche amesema  kuwa kwa sasa walichofanikiwa ni kunyanyua ari za wachezaji na kuwajenga kisaikolojia jambo ambalo limepelekea ushindi huo mnono.

“Mimi huwa ni mshindani, napenda kushindana, sipendi kupoteza, ninapopata nafasi ya kuishika timu huwa sipendi masikhara, kingine naifahamu vizuri Azam FC wachezaji wengi nawajua, nawapongeza vijana kwa kazi nzuri na kubwa waliyofanya na kupata ushindi huu muhimu,” alisema.

Kocha huyo mwenye ushawishi mkubwa ndani ya viunga vya Azam Complex, aliwaomba mashabiki wa timu hiyo kuwapa ushirikiano kwa kipindi hiki kifupi walichokuwa na timu hiyo.

“Nawaahidi mambo mazuri yanakuja kama walivyonizoea, cha muhimu ni mashabiki kutupa ushirikiano kwa kujaa kwa wingi uwanjani na kuisapoti timu pia, hata pale atakapokuwa amepatikana kocha mpya,” alisema.

Mara baada ya mchezo huo, Azam FC inaelekeza nguvu zake zote kwenye mchezo ujao wa Ligi Kuu Tanzania Bara (TPL) dhidi ya African Lyon, utakaofanyika Ijumaa hii.

Mabingwa hao, sasa wamerejea kwenye mwendo wa ushindi ambapo kwa kutoa dozi hiyo kunawafanya kupata ushindi wa kwanza tokea kuanza kwa mwezi huu Februari katika mechi sita ilizocheza.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...