Na Grace Semfuko-MAELEZO 

Serikali kupitia Wizara ya Fedha na Mipango imetoa jumla ya shilingi Bilioni 28 kwa Wilaya ya Kinondoni, Jijini Dar Es Salaam kwa ajili ya kuendeleza miradi miwili ikiwepo ujenzi wa soko la Tandale na uboreshaji kwa kuendeleza ufukwe wa Osterbay, maarufu Coco Beach, lengo likiwa ni kulipa thamani eneo hilo na kuongeza watalii wa ndani nan je. 

Utiaji saini kwa ajili ya mkataba wa ujenzi huo ulifanywa February 4 mwaka huu, kati ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dotto James na Mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni, Aron Kagulumjuli, ambapo kati ya fedha hizo shilingi Bilioni 14 zitaendeleza Ufukwe wa Osterbay, eneo la Coco Beach na zingine Bilioni 14 zitajenga Soko la Tandale. 

Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Daniel Chongolo aliyasema hayo wakati wa uzinduzi wa kampeni ya mazingira ya “Mchanga Pekee” iliyo na lengo la kubadilisha mazingira ya fukwe za bahari ya Hindi, jijini Dar Es salaam, iliyofanyika leo asubuhi kwenye ufukwe wa Coco, zoezi lililoambatana na usafi wa mazingira kwenye eneo hilo. 

“Wilaya yangu ya Kinondoni tumekuja na mpango maalum wa kuimarisha mazingira ya Bahari, tunazo Bilioni 28 kwa ajili ya miradi miwili ya kuimarisha mazingira; zikiwemo fukwe za Osterbay zinazojumuisha eneo hili la Coco pamoja na kuimarisha mazingira ya soko la Tandale” Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni Chogolo Wanavikoba wa Buguruni na taasisi mbalimbali zilizofika kushiriki. 

Akisikilizwa na karibu mamia ya watu, wengi wao wakiwa akina mama wa vikoba, Bw. Chongolo alisema zoezi lililopo sasa ni hatua ya kutangaza mzabuni kwa ajili ya ujenzi huo ambapo katika kipindi cha miaka miwili ijayo shughuli hiyo itaanza. 

Mbali na fedha hizo za miradi miwili, Serikali mwaka jana ilitoa zaidi ya shilingi Bilioni 9 kwa ajili ya ukarabati wa soko la Magomeni, Jijini Dar Es Salaam zoezi ambalo linaendeleo mpaka sasa, aidha Chongolo alitoa wito kwa jamii kuhusu kuendeleza na kuzitunza fukwe za bahari ili kutengeneza mazingira mazuri ya wananchi kupumzika pia kubarizi 

Naye Afisa Uhusiano Mkuu wa Bodi ya Utalii Tanzania – TTB, Geofrey Tengeneza alisema fukwe za Bahari ni maeneo muhimu kwani watalii wengi wa ndani na nje ya nchi hutembelea maeneo hayo na hivyo yanahitaji kutunzwa katika hali ya usafi. 

“Fukwe hizi ni muhimu sana kwa utalii katika nchi yetu, hivyo tunahitaji kuzitunza na tusichafue mazingira ya fukwe zetu” alisema Tengeneza na kusisitiza kuwa ufukwe wa Coco ni maarufu kwa watu wote na serikali inatambua hilo na kwamba utaendelea kutumiwa na watu wote kwa ajili ya kupumzika na burudani. 

Kampeni ya “Mchanga pekee” imeanzishwa na Kampuni ya Cocacola kwanza na inalenga kuboresha mazingira ya fukwe za Bahari na kuwa safi na Cocacola inashirikisha Bodi ya Utalii Tanzania pamoja na mashirika na taasisi mbalimbali nchini. 

Kampeni hiyo imekuja kufuatia ripoti ya Shirika la “International Council of Beverages Associations (ICBA)” iliyotolewa mwishoni mwa mwaka 2018 ikionesha uchafuzi mkubwa wa fukwe za bahari duniani kufikia wastani wa vipande vya plastiki kilomita elfu 13 na kubainika kuwepo kwa tani milioni 150 za plastiki kwenye fukwe hizo mpaka leo. 

Mkurugenzi Mkuu wa Cocacola, Bazil Gadzios leo alisisitiza kuwa kampeni hiyo inalenga kufanya usafi kwenye fukwe wa Coco Beach, kukusanya chupa za plasitiki elfu kumi kila mwezi, kutoa elimu kwa jamii kuhusu kuhifadhi mazingira ya fukwe za bahari, kupunguza chupa hizo pamoja na kuhifadhi ekolojia ya viumbe vya Baharini na nchi kavu. 

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...