Na Zainab Nyamka, Globu ya Jamii.
KOCHA Mkuu wa Yanga Mwinyi Zahera amelalamikia ratiba ya Ligi Kuu Tanzania Bara kuwa haiwapi nafasi wachezaji muda wa kupumzika.
Ameyasema hayo baada ya kuwasili Mkoani Singida jana usiku ikiwa ni safari ya masaa 15 kutoka Tanga walipokwenda kucheza na Coastal Union.
Zahera amesema, wachezaji wake wamemaliza kucheza mechi siku ya Jumapili jioni na jana Jumatatu wametoka Tanga na kuanza safari majira ya saa 1 asubuhi na kufika Singida sa 3 usiku ikiwa ni masaa 15 ya safari.
Amesema, katika ratiba ya kawaida wachezaji wake watapata muda mchache sana wa kupumzika na kesho watatakiwa wacheze na Singida United.
"Ratiba ya Ligi sijawahi kuona katika maisha yangu, huwezi kucheza mechi ukasafiri siku masaa 15 kuja Singida ucheze mechi halafu urudi tena masaa 15 Tanga kucheza mechi nyingine," amesema Zahera.
Zahera amesema ratiba imekuwa inamnyima fursa ya kuandaa programu kwa wachezaji wake hususani baada ya kumaliza mechi na pia timu nyingi zimekuwa zikichoka sana kutokana na ratiba kuwa ngumu kwa sababu ya miundo mbinu na jiografia ya nchi.
Yanga inashuka dimbani siku ya Jumatano kucheza na Singida United katika muendelezo wa Ligi kuu Tanzania Bara na kisha itarejea tena Tanga kucheza na JKT Tanzania Februari 9 mwaka huu.
Yanga inaongoza ligi kwa alama 54 akifuatiwa na Azam mwenye alama 47 huku nafasi ya tatu ikiwa ni kwa KMC mwenye alama 35.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...