Na Stella Kalinga, Simiyu
Wananchi wa Kata ya Lamadi Wilayani Busega mkoani Simiyu wamepiga kura za siri kwa lengo la kubaini watuhumiwa wa mauaji ya watoto yaliyotokea hivi karibuni wilayani humo. Wakizungumza katika zoezi hilo lililofanyika Februari 14, 2019  katika Kitongoji cha Kisesa Kijiji cha Lamadi wananchi hao wamesema kuwa  wamelipokea vizuri zoezi hilo na kubainisha kuwa kura hizo zitasaidia Vyombo vya Dola katika kufanya uchunguzi na kuwabaini wauaji wa watoto wilayani humo.

“Zoezi hili nimelipokea vizuri na nina imani litatusaidia kuwapata wauaji wa watoto wetu na naishukuru Serikali kuona haja ya kuwashirikisha wananchi maana mauaji haya ya watoto yametusikitisha sana wakazi wa Lamadi” alisema Modesta Andrea mkazi wa Lamadi

“ Tukio hili la kupiga kura za siri mimi naona ni zuri kwa sababu naamini kuna baadhi ya wananchi wanaweza wakawa wanafahamu watu waliofanya mauaji ya watoto na kama ikitokea kuna watu wakaandikwa labda kwa sababu ya fitina tunaamini vyombo vyetu vya dola vitachuja na kuchunguza na mwishowe wauaji watabainika tu; tunaomba wakibainika sheria ifuate mkondo wake” alisema Elisha Daniel mkazi wa Lamadi.

Akizungumza na wananchi wa Lamadi mara baada ya zoezi hilo kukamilika, Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe. Anthony Mtaka amesema kufanyika kwa zoezi hilo hatua ya kwanza ya uchunguzi wa mauaji ya watoto wilayani humo, huku akiwahakikishia wananchi kuwa kura walizopiga zitahesabiwa kwa haki na vyombo vya dola mkoani humo.

“Kupiga kura za siri si kwamba tumeshindwa kufanya upelelezi, hii ni hatua ya kwanza ya sisi kufanya uchunguzi wetu, kura hizi zitahesabiwa na vyombo vya dola mkoani Simiyu ambavyo ni Usalama wa Taifa, Uhamiaji, Jeshi la Magereza, Jeshi la Wananchi JWTZ (Mkoa wa Simiyu), Jeshi la Zimamoto, Jeshi la Polisi na TAKUKURU” alisema Mtaka.

Aidha, Mtaka amesema Serikali mkoani humo itaendelea kutimiza wajibu wake wa kwanza wa kulinda watu wake na kuhakikisha wananchi wanaishi kwa amani ili waweze kufanya vema shughuli za maendeleo.Sambamba na hilo Mtaka amesema Serikali itahakikisha inayafanyia kazi masuala mbalimbali yaliyosemwa na wananchi katika mkutano huo, ikiwa ni pamoja na malalamiko dhidi ya utendaji wa baadhi ya viongozi na watendaji wa Serikali  na kubainisha kuwa  hatua stahiki zitachukuliwa dhidi ya wale wote watakaobainika kwenda kinyume katika kuwatumikia wananchi.

“Niwahakikishie kuwa Serikali itayafanyia kazi yote yaliyosemwa na wananchi katika Mkutano wa hadhara uliofanyika hapa Lamadi, kama kuna wakubadilishwa watabadilishwa, wa kuwajibishwa watawajibishwa, wakuhamishwa watahamishwa naomba mniamini” alisisitiza Mtaka. Kwa upande wake Mbunge wa Busega, Dkt. Raphael Chegeni ametoa pole kwa wazazi wote waliopoteza watoto wao katika mauaji ya watoto na kuahidi kutoa rambirambi shilingi 500,000/= kwa kila familia iliyokutwa na msiba huku akilaani vikali vitendo vya mauaji ya kinyama ambayo yamekatisha ndoto za watoto hao.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Busega, Mhe. Tano Mwera amewashukuru wananchi wa Lamadi kwa  namna walivyojitokeza katika zoezi la kupiga kura za siri na kwa namna walivyolifanya kwa amani na utulivu.
Modesta Andrea kutoka kijiji cha Itongo Kata ya Lamadi wilayani Busega mkoani Simiyu akipiga  kura ya siri katika zoezi maalum la kupiga kura za siri lililowahusisha  wananchi wa Lamadi  lililofanyika katika Kitongoji cha Kisesa Februari 14, 2019  kwa ajili ya kubaini watuhumiwa wa mauaji ya watoto yaliyotokea hivi karibuni wilayani humo.
 Baadhi ya wananchi wa Lamadi wakiweka karatasi zao za kura za siri zilizopigwa katika zoezi maalum la wananchi wa Lamadi  kupiga kura za siri lililofanyika katika Kitongoji cha Kisesa,   kwa ajili ya kubaini watuhumiwa wa mauaji ya watoto yaliyotokea hivi karibuni wilayani humo.
 Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka akizungumza na wananchi wa Lamadi wilayani Busega mara baada ya kukamilika kwa zoaezi la wananchi kupiga kura za siri kubaini watuhumiwa wa mauaji ya watoto yaliyotokea hivi karibuni wilayani humo, ambalo limefanyika katika Kitongoji cha Kisesa Kijiji cha Lamadi Februari 14, 2019.
 Baadhi ya wananchi wa Lamadi wilayani Busega wakiendelea kupiga kura za siri na wengine wakisubiri kauli ya Serikali mara baada ya kupiga kura hizo zilizokuwa na lengo la kubaini watuhumiwa wa maujai ya watoto yaliyotokea hivi karibuni wilayani Busega, zoezi la kupiga kura limefanyika katika Kitongoji cha Kijiji cha Lamadi Februari 14, 2019.
Kutoka kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka, Mkuu wa Wilaya ya Busega, Mhe. Tano Mwera, Mkuu wa Wilaya ya Meatu, Dkt. Joseph Chilongani na Mbunge wa Busega, Dkt. Raphael Chegeni wakiteta jambo katika mkutano maalum ambao wananchi wa Lamadi wilayani Busega, wamepiga kura za siri kubaini watuhumiwa wa mauaji ya watoto yaliyotokea hivi karibuni, zoezi ambalo limefanyika katika Kitongoji cha Kisesa Kijiji cha Lamadi Februari 14,2019.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...